Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
“Kondoo Humsikia Sauti Yake”
◻ YESU alisema: “Kondoo humsikia sauti yake [mchungaji]; naye huwaita kondoo wake kwa majina yao, na kuwapeleka nje.” (Yohana 10:3) Yeye aliongeza zaidi hivi: “Walio wangu nawajua; nao walio wangu wanijua mimi.” (Yohana 10:14) Walio kama kondoo husikia sauti ya Yesu akisema nao kupitia Biblia. Angalia jinsi watu wawili wenye mioyo yenye kufuatia haki walifuata mwendo huu.
Hatimaye Alisikia
◻ Alberto aandika hivi: “Nilikuwa na miaka 16 nilipoanza kuvuta marihuana (kasumba) na kutumia LSD, na nilipofika miaka 18 nilianza kutumia heroini. Nilifanya jambo lolote liwezekanalo, ili niweze kupata dawa za kulevya. Niliiba, niliuza dawa za kulevya, nilipunja, niliuza vitu vyangu vyote. Singeweza kuacha hata kidogo. Kwenda ng’ambo likizoni, kukaa wakati mrefu sehemu za mashambani, au kuhusika katika mambo ya kisiasa pamoja na vikundi vya watu wanaoshikilia maoni yasiyo ya kiasi ya kushindana na uonevu—mambo yote hayo hayakusaidia. Nilijaribu ndoa, lakini baada ya muda mchache nilirudia jinsi nilivyokuwa. Hata kuzaliwa kwa mtoto kischana hakukunifanya niache kutumia dawa za kulevya. Kwa hakika, mambo yalizidi kuharibika, kwa kuwa sasa nilihitaji pesa nyingi zaidi. Halafu mke wangu akaniacha, na katika miaka miwili ya kuishi peke yangu, nilimwona binti yangu mara mbili tu. Nilikuwa nikiwakimbia wauzaji wa dawa za kulevya kwa kuwa walinidai pesa, na nyakati nyingi niliteseka kwa maumivu ya kujaribu kuziacha.
“Halafu nikakumbuka kitabu ambacho Mashahidi wa Yehova walikuwa wamenipatia miaka ya mapema. Bado nilikuwa nacho na nikaanza kukisoma pamoja na Biblia. Kwa njia hii nikaja kumjua Mungu wa kweli, Yehova, na nikasali kwake anisaidie. Nilipokuwa nikizoea yale nilikuwa nikijifunza hatua kwa hatua, maumivu yangu kwa sababu ya kuacha dawa za kulevya yakaanza kupunguka. Nilipata kazi, na kwa msaada wa Yehova nikaunganisha familia yangu tena. Nilikwenda kwenye Jumba la Ufalme, na hapo nikatambua kwamba Mashahidi wa Yehova ndio wenye ukweli. Tukiwa pamoja tena, mke wangu nami tukajifunza Biblia pamoja na Mashahidi na hatimaye tulibatizwa. Sasa, ni shangwe kama nini kushiriki na wengine tumaini letu tukiwa mapainia wa kawaida!”
Sala za Mwanamke Mwenye Kumcha Mungu Zajibiwa
◻ Mwanamke mmoja aripoti hivi: “Katika 1958, nilihusika kwa bidii katika utendaji wa mtaa, hasa katika ziara za kwenda kwenye Patakatifu pa Madonna wa Upendo wa Kimungu katika Roma. Baada ya muda nikawa rafiki wa karibu wa kadinali aliyekuwa vikari wa Roma, na nilikuwa na mazungumzo mengi ya faraghani pamoja na Mapapa Paul 6 na John Paul 2. Baada ya miaka 25 ya kupanga kitengenezo ziara, nilipokea diploma ya ustahili. Hata hivyo, wakati ulipopita imani yangu nikiwa Mkatoliki mwenye bidii ikaanza kuyumbayumba. Niliona wizi, upunjaji, ukabila, na uchuuzi wa kiajabu. Maoni yangu ya kanisa yakaanza kuwa tofuati nilipoona kwamba mara nyingi sheria ya Mungu ilipuuzwa. Mambo kama haya yalinisumbua, na nikamwomba Mungu anisaidie kwa sababu nilikuwa nikipoteza imani yangu. Nililia mara nyingi.
“Halafu, miaka minne iliyopita, mwana wangu akaniletea baadhi ya nakala za Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ambazo alikuwa amepata kutoka kwa Mashahidi wa Yehova. Magazeti hayo yalipendeza sana hivi kwamba nilimwomba aniletee nyingine zaidi. Muda mfupi baada ya hapo nilipata Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova na nikaacha barua fupi kuomba kwamba mtu anitembelee. Mashahidi walikuja baada ya muda wa siku nne. Nilianza funzo la Biblia na nikafanya maendeleo kufikia kiwango cha kubatizwa. Sasa nina uhakika kwamba hatimaye nimepata kile ambacho nimekuwa nikikitafuta sikuzote—ukweli!”
Watu hawa mmoja mmoja walisikia sauti ya Mchungaji Mwema, Yesu Kristo, na ‘hiyo kweli ikawaweka huru.’—Yohana 8:32.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 14]
Garo Nalbandiany