Nina Sababu Nyingi Kama Nini za Kuwa na Shukrani!
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA LOTTIE HALL
ILITOKEA tulipokuwa njiani kutoka Calcutta, India, kwenda Rangoon, Burma, katika 1963. Muda mfupi baada ya kuondoka Calcutta kwa ndege, ndugu mmoja aliona kwamba mafuta yalikuwa yakivuja kwenye bawa. Wafanyakazi wa ndege walipoambiwa juu yalo, walijulisha rasmi kwamba tungeteremka kwa dharura. Kwanza ndege ilihitaji kupunguza mafuta mengi ili iweze kuteremeka. Mtumishi wa abiria alipaaza sauti hivi, “Mkitaka kusali, fanyeni hivyo sasa hivi!” Sisi kwa kweli tulisali kwamba ikiwa yalikuwa mapenzi ya Yehova, tungeweza kuteremka salama, na ilitokea hivyo. Kwa kweli tulikuwa na sababu ya kuwa na shukrani!
NDIYO, na bado nina sababu nyingine nyingi za kuwa na shukrani. Nikiwa na miaka 79, bado nina kiasi cha afya njema na nguvu, ambazo ninatumia katika utumishi wa wakati wote. Tena, kuongezea mibaraka hiyo ambayo ni ya kawaida kwa watu wote wa Yehova, nimekuwa na maono mengi yenye kutokeza. Kwa ujumla, imekuwa katiba yangu yenye thamani kumtumikia Yehova kwa zaidi ya miaka 60, na zaidi ya nusu ya wakati huo nimekuwa mhudumu wa wakati wote, au painia.
Yote hayo yalianza na baba yangu tulipokuwa tukiishi Carbondale, Illinois. Yeye alishiriki na madhehebu ya Wanafunzi wa Kristo naye alipendezwa na kuwa mhudumu. Hata hivyo, ono lake pamoja na vyuo viwili vya Biblia lilimwacha amevurugika, kwa kuwa alikuwa na mawazo yake mwenyewe juu ya Utatu, kutokufa kwa nafsi, na kuteseka milele.
Hatimaye, alitosheka na ukweli wa Biblia alioletewa na Mwanafunzi wa Biblia aliyekuwa kolpota (mhubiri wa wakati wote) katika 1924, nilipokuwa na umri wa miaka 12 tu. Baba yangu aliterema kujifunza kwamba kulikuwa na wengine walioona mambo jinsi alivyoyaona, kwamba Utatu, moto wa mateso, na kutokufa kwa nafsi ya binadamu yalikuwa mafundisho bandia. Baada ya muda mfupi familia yetu ilikuwa ikikutana kwa kawaida na Wanafunzi wa Biblia, jinsi Mashahidi wa Yehova walivyokuwa wakiitwa wakati huo. Kujifunza ukweli juu ya Yehova na Neno lake ni jambo ambalo lilinifanya niwe na shukrani kweli kweli.
Hata hivyo, kabla ya muda mrefu kupita, afa lilitokea. Mwanamume aliyemletea baba yangu kweli hizi aligeuka kuwa asiyefuata haki na asiye na adili pia. Alimkwaza baba yangu lakini si mama yangu na mimi. Sasa nikiwa na miaka 15, ni mimi niliyekuwa na umri mkubwa zaidi kati ya watoto sita, na pamoja na mama yangu nilishikamana na ukweli.
Katika kiangazi cha 1927, tangazo lilitolewa kwamba mkusanyiko mkubwa wa Wanafunzi wa Biblia ungefanywa Toronto, Kanada. Baba alisema yeye hakuwa na uwezo wa kwenda, lakini mama alikuwa mwanamke mwenye nia thabiti. Alianza kuchuuza vyombo vya namna mbalimbali vya nyumbani, na wakati mkusanyiko ulipofika, yeye alikuwa amekusanya dola nane. Tukiwa na fedha hizo yeye nami tulianza safari ya miguu na kusimamisha magari kwenda Toronto, umbali wa kilometa 1,600. Ilikuwa muda wa siku tano na mara 37 za kwenda na gari kabla ya kufika mwishowe, tukiwasili huko siku ile ya kabla ya mkusanyiko kuanza. Kwa sababu fedha zetu hazikuwa nyingi, tuliomba mahali pa kulala tukapapokea bila malipo. Ndugu A. H. Macmillan aliposikia juu ya safari yetu, aliandika juu yayo ili itiwe katika gazeti la habari za mkusanyiko chini ya kichwa: “Ongezeko Lolote Katika Bei ya Usafirishaji wa Reli Halihangaishi Hawa Wanafunzi wa Biblia.”
Mama aliendelea kumpasha baba habari kupitia postikadi. Kwa hiyo, mwishowe aliamua kuja na akawasili kwa gari kabla tu ya hotuba ya watu wote siku ya mwisho ya mkusanyiko. Sasa hatukuhitaji kurudi nyumbani kwa safari ya miguu na ya kusimamisha magari. Lo, huo ulikuwa mkusanyiko wa ajabu kama nini! Nilikuwa na shukrani kama nini kwamba tuliweza kuuhudhuria, na nilikuwa na shukrani kama nini kwamba ulimsaidia baba yangu apate tena usawaziko wake wa kiroho!
Kwa miaka mingi nilipoulizwa dini yangu ni gani, nilijibu, “IBSA,” herufi ambazo zilisimamia International Bible Students Association. Lakini sikuzote sikufurahia jina hilo. Kwa hiyo, nilikuwa na shukrani, wakati tulipokubali jina Mashahidi wa Yehova kwenye mkusanyiko wa 1931 huko Colombus, Ohio.
Kazi Maisha Yangu ya Shule
Miongoni mwa mibaraka mingi ambayo imefanya maisha yangu yatajirike ni ile iliyohusika na muziki. Nilipenda muziki sana na nilijifunza kupiga kinanda [piano] mapema. Kwa miaka mingi nilikuwa na pendeleo la kufuata uimbaji wa kundi kwa kupiga muziki. Kabla ya Watch Tower Society kuanza kurekodi nyimbo za Ufalme, ndugu misionari aliyetumikia Papua New Guinea aliniomba nirekodi baadhi ya nyimbo zetu ili Wapapua waweze kujifunza kuziimba. Hilo lilikuwa jambo ambalo nilionea shangwe kweli kweli kulifanya.
Hata hivyo, ala ya muziki iliyonipendeza sana ilikuwa klarineti. Nilipenda kuipiga katika okestra ya chuo kikubwa. Profesa wa chuo kikubwa alipendezwa sana na upigaji wangu wa muziki hivi kwamba akaniomba nipige muziki katika bendi ya wanaume. Katika siku hizo hakuna mwanamke yeyote aliyepiga muziki katika bendi ya wanaume, kwa hiyo washirika wa bendi waliposikia vile profesa alikuwa amependekeza, walipanga kugoma. Walighairi walipojulishwa kwamba kama wangegoma, wangefukuzwa. Mapokeo mengine yalivunjwa nilipotakiwa kutembea kigwaride pamoja na bendi katika andamano la mchana kutwa. Gazeti la habari lililikadiri kuwa jambo la kushtua na lililiripoti kwa kichwa chenye herufi kubwa: “Mwanamuziki Msichana Katika Bahari ya Wanaume.”
Hatimaye, nilihojiwa kwa ajili ya kuwa profesa wa muziki. Hata hivyo, nilipofikiria juu ya masuala yote ambayo yangeweza kutokeza ikiwa ningefundisha muziki, kama vile kuombwa kufundisha au kupiga muziki wa kidini na wa kitaifa, niliamua kufuatia kitu kingine na nikapewa mgawo wa kufundisha historia ya ulimwengu. Lakini badilisho hilo halikunifanya niache kupiga klarineti yangu miaka ya baadaye katika okestra za mkusanyiko katika mabara mengi nilipokuwa nikisafiri kwenda kwenye mikusanyiko ya kimataifa ya Mashahidi wa Yehova.
Baada ya muda, nikawa mfunzi katika historia ya ulimwengu katika shule ya juu katika kiunga cha Detroit, na kwa hiyo, wakati mmoja niliombwa na mkuu wa shule nipendekeze kimoja cha vitabu kadhaa vya mafundisho. Nilipokuwa ninapitia hivyo, nilishangazwa na ukweli wa kwamba ingawa kitabu kilichokuwa kikitumika sasa kilitaja jina la Yehova mara nane, vile vipya viliacha Mungu wa Waebrania bila jina, ingawa viliipa majina miungu mingi ya mataifa ya kipagani, kama vile Ra, Moleki, Zeu, na Yupita. Mchuuzi alipokuja, nilimwuliza ni kwa sababu gani Yehova hakutajwa katika kitabu chake cha mafundisho, naye akasema hivi: “La, sisi hatutaweka jina hilo katika maandishi yetu kwa sababu ya Mashahidi wa Yehova.” Kwa hiyo nikamwambia hivi: “Vema basi! Kwa hiyo mimi sitapendekeza maandishi yako.” Yeye alifunga kitabu kwa kishindo mfukoni mwake na kuondoka upesi kupitia mlango.
Baadaye, niliripoti kwa mkuu wa shule kwamba kwa kweli hatukuhitaji kitabu kipya cha mafundisho na nikampa sababu nzuri mbalimbali. Alikubaliana nami. Wote walifurahia uamuzi huo wakati mfulizo wa somo la historia ya ulimwengu ulipoondolewa kwenye taratibu ya shule ya juu, miezi michache baadaye. Mfulizo mpya, ulioitwa mafunzo ya jamii ya watu, ulichukua mahali pao kotekote katika ule mfumo wa shule 14. Kama shule ingalinunua vitabu vipya vya historia, hiyo ingalifanyiza hasara kama nini!
Nilikuwa na maono mengi yenye kuleta shangwe nilipokuwa ninafundisha shule na nilikuwa mwenye kushikisha nidhamu sana. Hilo lilinipa manufaa za kuwa na rafiki wengi wa maisha. Pia nilikuwa na nafasi ya kufanya ushahidi wa vivi hivi. Lakini hatimaye wakati na hali ziliniongoza kwenye utumishi wa wakati wote.
Mikusanyiko ya Kimataifa
Baada ya kufundisha kwa miaka 20, macho yangu yakaanza kukosa nguvu. Zaidi ya hayo, wazazi wangu waliona kwamba walinihitaji, kwa hiyo baba yangu akaniomba niende nyumbani, akisema kwamba kulikuwa kazi ya kufundisha iliyo muhimu zaidi, na Yehova angeangalia kwamba singekuwa na njaa. Niliacha kufundisha katika 1955, na miongoni mwa mibaraka yangu ya kwanza baadaye ilikuwa kuhudhuria mifululizo ya mikusanyiko ya “Ufalme Wenye Ushindi” katika Ulaya. Nilikuwa na shukrani kama nini kuwa na ndugu zetu katika Ulaya, wengi ambao walikuwa wameteseka sana wakati wa vita ya ulimwengu ya pili! Ilikuwa baraka hasa kuwa miongoni mwa wale 107,000 waliojaza Zeppelinwiese, au Konde-Majani la Zeppelin, katika Nuremburg, mahali ambapo Hitler alipanga kuwa na msafara wa ushindi baada ya Vita ya Ulimwengu 2.
Hiyo ilikuwa ya kwanza tu ya safari nyingi za ulimwengu ambazo nimependelewa kufanya. Katika 1963 mama yangu nami tulikuwa miongoni mwa wakusanyiki 583 kusafiri kuzunguka ulimwengu pamoja na makusanyiko “Habari Njema za Milele.” Safari hiyo ilitupeleka kutoka New York hadi Ulaya, halafu kwenda hadi Esia na visiwa vya Pasifiki kabla ya kumalizia katika Pasadena, Kalifornia. Ilikuwa wakati wa safari hiyo tulipokuwa na ono lenye kuogopesha linalosimuliwa katika utangulizi. Safari za baadaye zilitupeleka kwenye mikusanyiko katika Amerika ya Kusini, Pasifiki ya Kusini, na Afrika. Kwa kweli safari hizi zilitajirisha maisha yangu, na kuweza kupiga muziki katika okestra za mkusanyiko katika pengi pa mahali hapa, kulikuwa ongezeko zaidi kwa mpenda muziki.
Kuingia Katika Hesabu ya Wapainia
Katika 1955, baada ya kutoka Ulaya, nilijiunga na mama yangu katika kazi ya kupainia kwa mwaka mmoja, na halafu Sosaiti ikaniomba nifanye kazi pamoja na kundi dogo huko Apalachicola katika Florida ya magharibi. Kwa miaka saba dada mwingine na mimi tulisaidia kazi huko, na baada ya muda mfupi kundi liliweza kujenga Jumba la Ufalme ili kuratibu ongezeko. Maendeleo yaliendelea, na kabla ya muda mrefu kundi lingine lilifanyizwa katika Port Saint Joe. Nilitumia miaka 11 nikifanya kazi pamoja na makundi matatu katika Florida ya magharibi.
Wakati mmoja niliombwa na mwangalizi wa mzunguko kutafuta mahali pa kusanyiko la mzunguko. Niliweza kupata utumizi wa Centennial Building yenye fahari katika Port Saint Joe kwa dola 10 tu. Lakini tulihitaji kafeteria pia, na tulifikiria kutumia kifaa cha shule. Hata hivyo, nilipata kwamba msimamizi wa shule alipinga, na alisema ningepaswa kukutana pamoja na baraza la shule. Jumbe wa mji pia alikuja kwenye mkutano huo, kwa kuwa alitaka sisi tupate utumizi wa kafeteria. Alipouliza makatazo ya sisi kuitumia yalikuwa gani, mkuu wa baraza la shule alisema kwamba lingekuwa jambo jipya kwa kundi la kidini kutumia vifaa vya shule. Jumbe wa mji akageukia kwangu kupata jibu. Mimi nilikuwa na vikaratasi vya mwaliko vilivyoonyesha kwamba tulikuwa tumetumia vifaa vya shule kwa ajili ya mikutano yetu katika miji mingine, halafu nikaelekeza kwenye Matendo 19:9, ambalo lilisema kwamba mtume Paulo alihubiri kwenye darasa la shule. Hilo lilimaliza yote. Baraza lilikubali pamoja na jumbe wa mji kutupatia kafeteria—kwa dola 36.
Nilipokuwa na miaka 13 tu, umri nilipobatizwa, nilisali hivi: “Ee, Mungu, niache tu nilete mtu mmoja katika ukweli.” Sala hiyo ilikuwa sasa ikijibiwa mara nyingi sana kwa kuwa nilibarikiwa na kusaidia watu wengi kuchukua msimamo wao kwa Yehova na Ufalme wake. Hata hivyo, tena na tena, kabla tu ya mwanafunzi wa Biblia kufikia hatua ya kujiweka wakfu na kubatizwa, nilipewa mgawo wa kundi lingine. Hata hivyo, nilikuwa na pendeleo la kupanda na kutia maji, na wengi wa wanafunzi hawa wamethibitika kuwa marafiki wa maisha. Kushiriki katika utendaji kama huo wenye matokeo kuliniletea sababu nyingi za kuwa na shukrani.
Waenezaji Habari Wasaidia
Ingawa waenezaji habari mahali pengi wameripoti vibaya juu ya utendaji wa Mashahidi wa Yehova, ninafurahi kusema kwamba waenezaji habari katika eneo la De Land, Florida—mahali ninapotumikia sasa—wamenisaidia kutoa ushahidi. Kwa mfano, wakati mmoja tulipokuwa katika zile safari za mkusanyiko wa ulimwengu, mama wangu na mimi tulipelekea gazeti la habari la kwetu nyaraka ndefu, na hizi zilitangazwa upesi, pamoja na picha. Ripoti hizo zilikuwa kwa namna ya masimulizi juu ya kusafiri, lakini sikuzote tuliweza kuyatumia katika ushahidi wetu juu ya jina na Ufalme wa Yehova.
Imekuwa vivyo hivyo na ushahidi wangu wa barabarani. Nina kona moja barabarani ambapo nina viti viwili vya bustani, kimoja ninaketia na kingine ninafanyia wonyesho wa fasihi zetu. Wakati mmoja, makala ya nusu ukurasa pamoja na picha ilionekana katika gazeti la kwetu chini ya elezo hili fupi: “Lottie wa Deland Aendelea na Kazi ya Wazazi Wake Mashahidi.” Hivi karibuni zaidi, katika 1987, gazeti lingine lilikuwa na makala ya nusu ukurasa iliyokuwa na picha kubwa ya rangi chini ya kichwa hiki: “Lottie Hall Ana Kona Yake Mwenyewe Ambayo Amemwekea Kristo.” Mwaka uliofuata gazeti lingine lilikuwa na picha yangu kwenye ukurasa wa kwanza pamoja na maneno kama, “Yeye sikuzote yuko huko” na “Akiketia kiti cha bustani, mwalimu huyu wa shule aliyestaafu atumia mahali pake kwenye kona ya barabara kufanya kazi ya umisionari ya Mashahidi wa Yehova.” Pia, mara nne stesheni ya televisheni ya kwetu imetoa picha juu ya ushahidi wangu. Mimi huendelea kushiriki kwa kadiri ndogo katika sehemu zote za huduma ya Ufalme: kuhubiri nyumba kwa nyumba, ziara za kurudia, na mafunzo ya Biblia nyumbani. Hata hivyo, kwa sababu ya kuongezeka kwa umri na udhaifu wa kimwili, sasa ninatumia wakati mwingi katika kazi ya barabarani.
Nikikumbuka wakati uliopita ni lazima niseme kwamba kwa kweli ninazo sababu nyingi kuwa na shukrani. Kuongezea mibaraka ile iliyo ya kawaida kwa watu wote wa Yehova, nikiwa mwalimu wa shule nimekuwa na pendeleo la kuwavutia vijana wengi; nimekuwa na shangwe ya kuhudhuria mikusanyiko mingi ulimwenguni pote; nimekuwa na utumishi wa painia wenye mazao mengi; na pia nimebarikiwa kuhusiana na muziki. Tena, kulikuwako ushahidi ambao niliweza kufanya kupitia waenezaji habari. Kwa kweli, ninaweza kusema pamoja na Daudi mtunga zaburi hivi: “Nitalisifu jina la Mungu kwa wimbo, nami nitamtukuza kwa shukrani.”—Zaburi 69:30.