Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Kwa kuwa Wakristo hawabahatishi fedha, je! wanaweza kukubali tikiti au kushiriki katika droo, ambayo katika hiyo huenda wakashinda zawadi?
Hilo ni swali ambalo limetokea mara kwa mara, kwa hiyo limezungumziwa tayari katika vichapo vyetu. Katika lugha nyingine, tumewezesha faharisi za vichapo vyetu zipatikane, kama vile Watch Tower Publications Index 1930-1985 (na nyingine kama hiyo ya miaka 1986-1990). Ikiwa Mkristo ana faharisi kama hizo katika lugha yake zinaweza kuthibitika kuwa zenye mafaa sana katika kupata upesi majibu yenye kuridhisha.
Swali lililoulizwa juu ni kielelezo kimoja. Kwa kuchunguza katika Index ya 1930-1985 chini ya kichwa “Maswali Kutoka kwa Wasomaji,” mtu apata kichwa kidogo “‘droo,’ je! Mkristo aweza kupokea tikiti ya?” Msomaji aelekezwa kwenye sehemu “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika Mnara wa Mlinzi la Kiingereza la Februari 15, 1973, ukurasa 127.a Kwa kuwa mabuku ya wakati uliopita ya Mnara wa Mlinzi yamechapishwa tena, ndugu wengi sasa wana lile la 1973, au laweza kupatikana kwenye maktaba ya Majumba ya Ufalme mengi.
Habari iliyochapishwa katika 1973 ilionyesha kwamba Wakristo kwa kufaa huepuka michezo yoyote ya bahati-nasibu au droo zinazohusiana na kununua tikiti za michezo hiyo au kutoa fedha ili kubahatisha kushinda zawadi fulani. Kwa ufupi, sisi huepuka kucheza kamari, ambayo kwa hakika huonyesha pupa.—1 Wakorintho 5:11; 6:10; Waefeso 4:19; 5:3, 5.
Hata hivyo, huenda duka au kampuni fulani ya kibiashara ikatumia upigaji droo kuwa njia ya utangazaji. Mtu analotakiwa kufanya tu ni kutoa jina lake au kupeleka fomu au tikiti, bila kununua chochote. Droo hiyo ni sehemu tu ya shughuli ya utangazaji; imekusudiwa kuwa njia isiyopendelea upande wowote ya kuamua ni nani atakayepewa zawadi moja au zawadi nyingi. Wakristo fulani huenda wakahisi kwamba wangeweza kupokea zawadi hiyo katika droo isiyohusiana na kamari, kama vile ambavyo wangepokea bidhaa za bure za sampuli au zawadi nyinginezo ambazo kampuni ya kibiashara au duka fulani laweza kutumia katika programu yayo ya utangazaji.
Hata hivyo, Wakristo wengine wangeepuka kitu chochote kama hicho, kwa sababu hawataki kuwakwaza au kuwavuruga wengine na pia wakijitahidi kuwa mbali na ushawishi wowote wa kumtumainia yule aitwaye eti Bibi Bahati. Kama vile Isaya 65:11, NW lionyeshavyo, watumishi wa Mungu hawajifungamanishi na “mungu wa Bahati Njema” au “mungu wa Ajali.” Huenda pia wakahisi kwamba wasingetaka kuwa sehemu yoyote ya sherehe za kujulishwa peupe ambamo huenda washindi wakatakiwa washiriki. Bila shaka, wale wanaohisi hivyo hawapaswi kuchambua Mkristo au Wakristo ambao dhamiri yao inawaruhusu kujihusisha na droo kama hizo.—Linganisha Warumi 14:1-4.
[Maelezo ya Chini]
a Habari iyo hiyo imeorodheshwa chini ya vichwa “Utangazaji,” “Biashara,” na “Kucheza Kamari,” kwa hiyo matumizi mbalimbali ya Index humsaidia mtu apate habari.