Fanya Ndoa Yako Iwe Muungano Wenye Kudumu
“Aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe.”—MATHAYO 19:6.
1. Ni nini msingi wa mafanikio ya ndoa miongoni mwa Wakristo wa kweli leo?
MAELFU mengi ya watu wa Yehova leo hufurahia ndoa zenye kuridhisha na zenye kudumu. Lakini mafanikio hayo mengi hayakuja yenyewe tu. Ndoa za Kikristo husitawi wakati wenzi wote wawili (1) wanastahi maoni ya Mungu juu ya ndoa na (2) wanajitahidi kuishi kulingana na kanuni za Neno lake. Ni Mungu mwenyewe aliyeanzisha mpango wa ndoa. Ni kwa kupitia Yeye ‘kila familia mbinguni na duniani hupata jina layo.’ (Waefeso 3:14, 15, NW) Na kwa sababu Yehova ajua kile kinachohitajiwa ili ndoa ifanikiwe, twajinufaisha tukifuata mwongozo wake.—Isaya 48:17.
2. Matokeo ya kutotumia kanuni za Biblia katika ndoa ni gani?
2 Kwa upande mwingine, kukosa kutumia kanuni za Biblia kwaweza kutokeza ndoa yenye huzuni. Wastadi fulani waamini kwamba watu wengi wapatao theluthi-mbili ya wale wanaofunga ndoa Marekani hatimaye watapata talaka. Hata Wakristo hupatwa na mibano na mikazo ya “nyakati [hizi] za hatari.” (2 Timotheo 3:1) Magumu ya kiuchumi na mikazo ya kazini yaweza kuathiri ndoa yoyote. Wakristo fulani pia wamevunjika moyo sana kwa sababu wenzi wao hawatumii kanuni za Biblia. “Nampenda Yehova,” asema mke mmoja Mkristo, “lakini ndoa yangu imejaa matatizo kwa miaka 20. Mume wangu ni mchoyo na hataki kufanya mabadiliko yoyote. Nahisi nimenaswa.” Waume au wake wengi Wakristo wamekuwa na maoni kama hayo. Mambo huharibikia wapi? Na ni nini kiwezacho kuzuia ndoa isiingie katika hali ya kutojaliana au hata chuki ya moja kwa moja?
Udumifu wa Ndoa
3, 4. (a) Ni nini kiwango cha Mungu cha ndoa? (b) Kwa nini udumifu wa ndoa ni jambo lenye kufaa na kunufaisha?
3 Hata ndoa iwe katika hali bora zaidi, hiyo ni muungano wa watu wasiokamilika. (Kumbukumbu la Torati 32:5) Kwa hiyo, mtume Paulo alisema kwamba “watu kama hao [wanaooa] watakuwa na dhiki katika mwili.” (1 Wakorintho 7:28) Hali fulani zilizo mbaya sana zaweza hata kutokeza kutengana au talaka. (Mathayo 19:9; 1 Wakorintho 7:12-15) Hata hivyo, katika visa vingi Wakristo hutumia shauri la Paulo: “Mke asiachane na mumewe . . . , tena mume asimwache mkewe.” (1 Wakorintho 7:10, 11) Kwa kweli, ndoa ilikusudiwa iwe muungano wenye kudumu, kwa kuwa Yesu Kristo alitangaza hivi: “Aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe.”—Mathayo 19:6.
4 Kwa mtu anayehisi amenaswa katika ndoa yenye chuki au isiyo na upendo, kiwango kilichowekwa na Yehova huenda kikaonekana kuwa kikali na kisichofaa. Lakini sivyo. Udumifu wa muungano wa ndoa huwafanya wenzi wenye kumcha Mungu wakabili na kutafuta kusuluhisha matatizo yao, badala ya kutoroka wajibu wao kwa kuona tu ishara ya kwanza ya tatizo. Mtu mmoja ambaye alikuwa amefunga ndoa kwa zaidi ya miaka 20 alisema hivi kuhusu jambo hilo: “Huwezi kuepuka pindi za matatizo. Hamtafurahiana nyakati zote. Wakati huo ndio kujitoa kwawa muhimu kwelikweli.” Bila shaka, waume na wake Wakristo wanahisi wana wajibu wa kwanza kwa Yehova Mungu, Mwanzilishi wa ndoa.—Linganisha Mhubiri 5:4.
Ukichwa na Unyenyekeo
5. Ni yapi baadhi ya mashauri ya Paulo kwa waume na wake?
5 Kwa hiyo, matatizo yatokeapo, ni wakati wa kutafuta njia bora zaidi ya kutumia shauri la Neno la Mungu badala ya kutafuta njia ya kutorokea. Kwa kielelezo, fikiria maneno haya ya Paulo, yanayopatikana kwenye Waefeso 5:22-25, 28, 29: “Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu. Kwa maana mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa; naye ni mwokozi wa mwili. Lakini kama vile Kanisa limtiivyo Kristo, vivyo hivyo wake nao wawatii waume zao katika kila jambo. Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake. Vivyo hivyo imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe. Maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza, kama Kristo naye alivyolitendea Kanisa.”
6. Waume Wakristo wapaswa kuwaje tofauti na wanaume wa ulimwengu?
6 Mara nyingi waume wametumia vibaya mamlaka yao ya kuwa waume na kuwatawala wake zao. (Mwanzo 3:16) Lakini, Paulo alihimiza waume Wakristo wawe tofauti na wanaume wa ulimwengu, wawe kama Kristo, wala si wadhalimu wanaotawala kila kitu katika maisha za wake zao. Kwa hakika, yule mwanaume Yesu Kristo hakuwa mkali wala hakuwa mwenye kupiga ubwana. Alitendea wafuasi wake kwa heshima na staha, akisema: “Njoni kwangu, nyinyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo.”—Mathayo 11:28, 29.
7. Mwanaume aweza kumheshimuje mkewe iwapo ni lazima mke huyo afanye kazi ya kimwili?
7 Mume Mkristo humheshimu mke wake kama chombo dhaifu. (1 Petro 3:7) Kwa kielelezo, tuseme ni lazima mke afanye kazi ya kimwili. Mume atafikiria jambo hilo kwa uzito, akiwa mwenye kutoa msaada na mwenye kujali kadiri iwezekanavyo. Sababu moja kubwa inayofanya wanawake wachukue talaka ni waume zao kupuuza watoto ama makao. Kwa hiyo, mume Mkristo hutafuta kusaidia mke wake nyumbani kwa njia zifaazo zinazonufaisha familia nzima.
8. Ujitiisho wahusisha nini kwa wake Wakristo?
8 Kutendewa kwa heshima hufanya iwe rahisi kwa wake Wakristo wajitiishe kwa waume zao. Hata hivyo, hilo halimaanishi kuwa mtumwa kabisa. Mungu aliamuru kwamba mke hangekuwa mtumwa, bali “msaidizi” (“kifani,” kielezi-chini, NW), jambo linaloonyesha kitu chenye kumkamilisha mwanaume. (Mwanzo 2:18) Kwenye Malaki 2:14, mke husemwa kuwa ‘mwenzi’ wa mwanaume. Kwa hiyo, wake katika nyakati za Biblia walikuwa na uhuru mwingi na hiari nyingi. Kuhusu “mke mwema,” Biblia yasema hivi: “Moyo wa mumewe humwamini.” Kwa kweli, ameaminishwa mambo kama vile usimamizi wa ujumla wa nyumba, kusimamia ununuzi wa chakula, kushughulikia ununuzi wa mali, na kuendesha biashara ndogo.—Mithali 31:10-31.
9. (a) Wanawake wenye kumhofu Mungu katika nyakati za Biblia walionyeshaje unyenyekeo wa kweli? (b) Ni nini kiwezacho kumsaidia mke Mkristo anyenyekee leo?
9 Hata hivyo, mke mwenye kumhofu Mungu alitambua mamlaka ya mume wake. Kwa kielelezo, Sara ‘alimtii Abrahamu, akimwita Bwana.’ Si tu kwa kufuata adabu, bali ikiwa wonyesho wa unyoofu wa unyenyekeo wake. (1 Petro 3:6; Mwanzo 18:12) Pia kwa hiari aliacha makao yenye starehe katika jiji la Uru ili aishi katika mahema na mume wake. (Waebrania 11:8, 9) Lakini unyenyekeo haukumaanisha kwamba mke asichukue hatua itakikanayo ilipohitajika. Musa alipokosa kutii sheria ya Mungu juu ya tohara, mke wake, Sipora, aliepusha msiba kwa kuchukua hatua mara moja. (Kutoka 4:24-26) Mengi yanahusika kuliko kumpendeza mwanaume asiyekamilika. Ni lazima wake ‘watii waume zao kama kumtii Bwana.’ (Waefeso 5:22) Mke Mkristo awaziapo kwa kufikiria uhusiano wake pamoja na Mungu, jambo hilo humsaidia kuachilia mambo madogo-madogo yasiyofaa na mapungufu ya mume wake, jinsi tu ambavyo mume vilevile apaswa kufanya ashughulikapo na mkewe.
Mawasiliano—Uhai wa Ndoa
10. Mawasiliano ni muhimu kadiri gani katika ndoa?
10 Wakili mmoja wa talaka alipoulizwa sababu kubwa zaidi inayofanya mume na mke waachane, alijibu hivi: “Kushindwa kuzungumziana kwa unyoofu, kufunuliana mawazo yao ya ndani na kutendeana kama marafiki wa karibu zaidi.” Naam, mawasiliano ni uhai wa ndoa imara. Ni kama Biblia isemavyo, “pasipo mashauri makusudi hubatilika.” (Mithali 15:22) Waume na wake wahitaji kuwa ‘marafiki wa usiri,’ wanaofurahia uhusiano wa karibu wenye uchangamfu. (Mithali 2:17) Lakini, waume na wake wengi hushindwa kuwasiliana, na hivyo uchungu huongezeka mpaka mlipuko wa hasira wenye madhara sana utokeapo. Ama mume na mke wanaweza kujifanya kuwa wenye adabu, lakini wakitengana kihisia-moyo.
11. Mawasiliano kati ya mume na mke yawezaje kufanywa yawe bora?
11 Sehemu ya tatizo yaonekana kuwa kwamba wanaume na wanawake mara nyingi wana njia tofauti za kuwasiliana. Wanawake wengi hufurahia kuzungumzia hisia, huku wanaume kwa kawaida wakipendelea kuzungumzia mambo hakika. Wanawake wanaelekea kuonyesha hisia-mwenzi na kutoa utegemezo wa kihisia-moyo, na wanaume huelekea kutafuta na kutoa masuluhisho ya matatizo. Lakini bado uwezekano wa kuwa na mawasiliano mazuri upo iwapo mume na mke wameazimia kuwa ‘wepesi wa kusikia, bali si wepesi wa kusema.’ (Yakobo 1:19) Angalianeni kwa macho na kusikiliza kabisa. Jaribuni kufanya kila mmoja wenu aseme yaliyo moyoni mwake kwa kuulizana maswali yenye fadhili. (Linganisha 1 Samweli 1:8; Mithali 20:5.) Badala ya kujaribu kutoa suluhisho la haraka mwenzi wako afunuapo tatizo fulani, sikiliza kwa makini mjitahidipo kutatua matatizo. Na msali pamoja kwa unyenyekevu mkitafuta mwongozo wa kimungu.—Zaburi 65:2; Warumi 12:12.
12. Wenzi Wakristo waweza kununuaje wakati kwa ajili ya mmoja na mwenzake?
12 Nyakati nyingine mibano na mikazo ya maisha huonekana kufanya mume na mke wakose wakati au nguvu ya kuweza kuwa na mazungumzo yafaayo. Lakini ikiwa Wakristo watadumisha ndoa yao ikiwa yenye heshima na kuilinda dhidi ya uchafuzi, ni lazima wawe na ukaribiano sana. Wao wapaswa kuuona muungano wao kuwa kitu chenye thamani na tunu, na ni lazima wanunue wakati kwa ajili ya muungano huo na kwa ajili ya mmoja na mwenzake. (Linganisha Wakolosai 4:5.) Katika hali nyinginezo suluhisho la kupata wakati wa mazungumzo mazuri laweza kuwa jambo rahisi tu kama kuzima televisheni. Kuketi pamoja kwa ukawaida na kunywa kikombe cha chai au kahawa kwaweza kusaidia mume na mke kuwasiliana kihisia-moyo. Katika pindi kama hizo wao waweza ‘kushauriana’ juu ya masuala kadhaa ya familia. (Mithali 13:10) Na ni jambo la hekima kama nini kusitawisha tabia ya kuzungumzia pamoja mambo yanayoudhi na kutoelewana juu ya mambo madogo-madogo kabla yawe visababishi vikubwa vya mikazo!—Linganisha Mathayo 5:23, 24; Waefeso 4:26.
13. (a) Yesu aliweka kielelezo gani juu ya kuwa wazi na mwenye unyoofu? (b) Ni zipi baadhi ya njia zinazoweza kufanya mume na mke wakaribiane?
13 Mtu mmoja alikiri hivi: “Mara nyingi inakuwa vigumu kwangu kueleza kwelikweli maoni yangu na kumwambia [mke wangu] jinsi ninavyohisi hasa.” Lakini, kufunua mambo yako ndio ufunguo wa kusitawisha ukaribiano. Ona jinsi Yesu alivyokuwa mnyoofu na mwenye kufunua mambo kwa wale waliotazamia kuwa washiriki wa jamii ya bibi-arusi wake. Yeye alisema hivi: “Siwaiti tena watumwa, kwa maana mtumwa hajui atendalo bwana wake; lakini ninyi nimewaita rafiki; kwa kuwa yote niliyoyasikia kutoka kwa baba yangu nimewaarifu.” (Yohana 15:15) Kwa hiyo, ona mwenzi wako kama rafiki. Mweleze mwenzi wako hisia zako. Jitahidi kusema “maneno ya mapenzi” yaliyo rahisi na yenye unyoofu. (Wimbo Ulio Bora 1:2, NW) Nyakati nyingine huenda mawasiliano ya wazi yakaonekana kuwa magumu, lakini wote wawili mume na mke watiapo jitihada za kutosha, mambo mengi sana yatatimizwa katika kufanya ndoa yao iwe muungano wenye kudumu.
Kushughulikia Kutoelewana
14, 15. Magomvi yaweza kuepukwaje?
14 Kwa hakika kutoelewana kwa mambo ya haki kutatokea mara kwa mara. Lakini nyumba yako isigeuke iwe ‘yenye magomvi.’ (Mithali 17:1) Uwe mwangalifu usizungumzie masuala yanayohitaji uangalifu watoto wasikiapo, na uonyeshe fadhili kwa hisia za mwenzi wako. Raheli aliposononeka juu ya hali yake ya kuwa tasa na kumwuliza Yakobo amzalie watoto, Yakobo alijibu hivi kwa hasira: “Je! mimi ni badala ya Mungu, aliyekuzuilia uzao wa mimba?” (Mwanzo 30:1, 2) Matatizo ya kinyumbani yatokeapo, shambulia tatizo lenyewe, wala usimshambulie mwenzi wako. Wakati wa mazungumzo ya faragha, epukeni ‘kunena bila kufikiri’ au kukatizana-katizana isivyofaa.—Mithali 12:18.
15 Ni kweli kwamba huenda ukaona kwamba ni maoni yako tu ndiyo yafaayo, lakini waweza kuyasema bila “uchungu wote na ghadhabu na hasira na kelele na matukano.” (Waefeso 4:31) “Zungumzieni matatizo yenu kwa sauti ya kawaida,” asema mume mmoja. “Sauti ya mmoja wenu ikiinuka, acheni mazungumzo. Rudini baada ya muda mfupi. Kisha mwanze tena.” Mithali 17:14, NW, yatoa shauri hili zuri: “Kabla ya ugomvi kufoka, ondoka.” Jaribuni kuzungumzia mambo tena wakati nyote wawili mmetulia.
Mdumishe Uaminifu Kati Yenu Wawili
16. Kwa nini uzinzi ni jambo zito sana?
16 Waebrania 13:4 laeleza hivi: “Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu.” Uzinzi ni dhambi dhidi ya Mungu. Pia unaharibu ndoa. (Mwanzo 39:9) Mshauri mmoja wa mambo ya ndoa aandika hivi: “Baada ya kugunduliwa, uzinzi hupiga familia nzima kama kimbunga, ukiharibu nyumba, ukivunjilia mbali tumaini na kujistahi, ukidhuru watoto kabisa.” Mimba au maradhi ya kupitishwa kingono yaweza kutokea pia.
17. Mielekeo ya uzinzi yaweza kuepukwaje au kukataliwaje?
17 Watu fulani husitawisha mielekeo ya uzinzi kwa kusitawisha maoni ya ulimwengu yaliyopotoka juu ya ngono kama ionyeshwavyo katika vitabu, kwenye televisheni, na katika sinema. (Wagalatia 6:8) Hata hivyo, watafiti wasema kwamba uzinzi mara nyingi hutokea kwa sababu ya mtu kutaka kujithibitisha kuwa angali mwenye kuvutia au kutokana na tamaa ya kutaka kupendwa zaidi bali si kutokana na tamaa ya ngono tu. (Linganisha Mithali 7:18.) Hata visababishi viwe nini, ni lazima Mkristo akatae mawazo yasiyo ya kiadili. Zungumzia hisia zako kwa unyoofu pamoja na mwenzi wako. Ikihitajika, tafuta msaada kwa wazee wa kutaniko. Kufanya hivyo kwaweza kuzuia usitumbukie kwenye dhambi. Isitoshe, Wakristo wahitaji kutahadhari wanaposhughulika na watu wa jinsia tofauti. Ingekuwa kinyume cha kanuni za Kimaandiko kufunga ndoa na mtu fulani lakini atazame mwingine kwa tamaa. (Ayubu 31:1; Mathayo 5:28) Wakristo hasa wanapaswa kuwa waangalifu wasisitawishe mahusiano ya kihisia-moyo pamoja na wafanyakazi wenzi. Acha mahusiano kama hayo yawe ya hali ya kirafiki lakini ya kikazi.
18. Mara nyingi chanzo cha matatizo ya kingono katika ndoa ni nini, nayo yaweza kusuluhishwaje?
18 Tahadhari kubwa hata zaidi iwezayo kuchukuliwa ni kuwa na uhusiano mchangamfu na ulio wazi pamoja na mwenzi wako. Watafiti wengi husema kwamba matatizo ya kingono katika ndoa mara nyingi hayatokani na mambo ya kimwili bali mara nyingi hutokana na kukosa kuwasiliana. Matatizo ya aina hiyo ni haba mume na mke wawasilianapo waziwazi na kupeana haki ya ndoa ikiwa wonyesho wa upendo badala ya kuiona kuwa wajibu.a Chini ya hali kama hizo zifaazo, mahusiano yaweza kuimarisha kifungo cha ndoa.—1 Wakorintho 7:2-5; 10:24.
19. Ni nini “kifungo cha ukamilifu,” nacho chaweza kuwa na uvutano gani katika ndoa?
19 Upendo “ndio kifungo cha ukamilifu” katika kutaniko la Kikristo. Kwa kusitawisha upendo, mume na mke wenye kumcha Mungu waweza ‘kuchukuliana na kusameheana.’ (Wakolosai 3:13, 14) Upendo unaofuata kanuni hutafuta hali-njema ya wengine. (1 Wakorintho 13:4-8) Kuza upendo kama huo. Utakusaidia kuimarisha kifungo cha ndoa yako. Tumia kanuni za Biblia katika maisha yako ya ndoa. Ukifanya hivyo, hakika ndoa yako itakuwa muungano wenye kudumu nayo italeta sifa na heshima kwa Yehova Mungu.
[Maelezo ya Chini]
a Makala “Uwasiliano—Si Maongezi Tu,” katika Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 1993, ilionyesha jinsi mume na mke wawezavyo kushinda matatizo katika hali hiyo.
Ungejibuje?
◻ Kwa nini ndoa yapaswa kuwa muungano wenye kudumu?
◻ Ni nini maoni ya Biblia juu ya ukichwa na unyenyekeo?
◻ Mume na mke waweza kufanyaje mawasiliano yawe bora?
◻ Wenzi waweza kushughulikiaje kutoelewana kwa njia ya Kikristo?
◻ Ni nini kitakachosaidia kuimarisha kifungo cha ndoa?
[Picha katika ukurasa wa 12]
Ikiwa ni lazima mke wake afanye kazi ya kimwili, mume Mkristo hatamruhusu alemewe na mizigo