Mashahidi wa Yehova Ulimwenguni Pote—Nigeria
NIGERIA imejibana katika mpindo wa chini wa mbenuko wa magharibi ya Afrika. Ikiwa katika Ghuba ya Guinea, iko kaskazini tu mwa ikweta nayo ina wakazi zaidi ya milioni 88.a
Katika miaka miwili ya utumishi iliyopita, ofisi ya tawi ya Nigeria ya Watch Tower Society imetoa uangalifu wa pekee kwa vijana. Uchunguzi uliofanywa katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ulionyesha kwamba asilimia 80 ya wale walioanza kuhubiri habari njema katika Nigeria katika kipindi cha 1992 walikuwa na umri kati ya miaka 10 na 20. Kati ya wale waliobatizwa katika mwaka huo, asilimia 63 walikuwa wa rika hilo.
Vijana Wafikia Upainia
Vijana wengi wanaingia katika kazi ya kuhubiri wakati wote wakiwa mapainia. Painia mmoja aitwaye Hannah asema: “Nilipokaribia kumaliza shule, niliwatembelea wale waliohudhuria Shule ya Utumishi wa Painia, nilikokutana na dada wawili wazee-wazee. Nikawaza, ‘Ikiwa hawa wawili waweza kupainia, kwa nini mimi nisiweze?’
“Kwa hiyo baada ya kumaliza shule, nikawa painia. Miezi mitatu baadaye nilikutana na Josephine mwenye umri wa miaka 26, aliyekuwa mwabudu wa uchawi. Yeye alisema: ‘Nyinyi Mashahidi wa Yehova ni watu wabaya. Hamsherehekei Krismasi wala hamtumii hirizi.’ Nilijibu kwamba kama angeniruhusu nisome naye Biblia, yeye angejifunza sababu inayofanya tusifanye mambo hayo. Yeye aliniambia nirudi. Upesi alianza kuhudhuria mikutano naye alifanya mabadiliko mengi maishani mwake. Mnamo Desemba 1990 alibatizwa. Tangu Agosti 1991, Josephine amekuwa painia. Alipohudhuria Shule ya Utumishi wa Painia mwaka uliopita, yeye alinijulisha kwa wanadarasa wenzake kuwa mama yake wa kiroho!”
Video na Jumba la Ufalme
Mojapo mirekodi ya video ya Sosaiti imesaidia kutaniko moja dogo kupata ardhi ya kujengea Jumba la Ufalme. Wakitafuta kununua ardhi, ndugu wanne walimwendea Onojie, kiongozi wa kidesturi wa eneo hilo. Aliwatolea ploti kwa naira 20,000 (dola 1,025, za Marekani). Kutaniko halingeweza kulipa kiasi hicho cha fedha, kwa kuwa kulikuwa wahubiri 17 tu wa kugharamia mradi huo kifedha. Onojie huyo akasema atafikiria mahali pengine.
Miezi kadhaa baadaye, mmoja wa wazee wa kutaniko alitembelea makao ya Onojie. Onojie alikuwa akitazama video ya kutawazwa kwake. Yule mzee akasema: “Nina video ambayo ningependa uone. Yaitwa Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name.”
Baadaye, huyo mzee alimwuliza Onojie aliionaje video hiyo. “Niliitazama mara tano,” akasema Onojie. Huyo mzee akamkumbusha Onojie juu ya Majumba ya Ufalme ambayo alikuwa ameona katika video na kueleza kwamba kutaniko la mahali hapo walitaka kujenga kama hayo. Kisha mzee huyo akauliza kama kutaniko lingeweza kununua ardhi inayopakana na ploti ndogo ambayo tayari lilikuwa limemiliki. Onojie akajibu: “Jana usiku baada ya kutazama video hiyo, nilifikiria jambo hilo.” Basi akapima ploti yenye upana wa meta 6 kando ya ploti ya kutaniko. “Mwaweza kuchukua hii,” yeye akasema. “Kwa urefu, mwaweza kuchukua kiasi mnachotaka. Tayarisha hati za kisheria, nami nitazitia sahihi.”
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari zaidi, ona 1994 Calendar of Jehovah’s Witnesses.
[Sanduku katika ukurasa wa 9]
HABARI ZA NCHI
Mwaka wa Utumishi wa 1993
KILELE CHA WANAOTOA USHAHIDI: 174,582
UWIANO: Shahidi 1 kwa watu 507
HUDHURIO LA UKUMBUSHO: 473,245
WASTANI WA WAHUBIRI WALIO MAPAINIA: 19,777
WASTANI WA MAFUNZO YA BIBLIA: 242,028
IDADI YA WALIOBATIZWA: 8,888
IDADI YA MAKUTANIKO: 3,289
OFISI YA TAWI: BENIN CITY, EDO STATE