Mashahidi wa Yehova Tengenezo Linalotegemeza Jina
KATIKA Oktoba 6, 1990, ule umati wa karibu 5,000 uliokusanyika katika Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova katika Jersey City, New Jersey, U.S.A., kwa ajili ya ule mkutano wa kila mwaka wa Watch Tower Bible and Tract Society ulikuwa karibu kupata mshangao. Mwenyekiti, John E. Barr, aliwaarifu wasikilizaji juu ya toleo la vidio ya dakika 55 yenye kichwa Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name (Mashahidi wa Yehova—Tengenezo Linalotegemeza Jina). Hiyo ilikuwa vidio ya kwanza iliyopata kutokezwa na Sosaiti, lakini kwa hakika si ya mwisho.
Vidio hiyo huonyesha jinsi watu wa Yehova walivyopangwa kitengenezo ili kushuhudia jina la Mungu na kutangaza “habari njema ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Makao makuu huko Brooklyn, New York, na majengo ya Watchtower Farms huonyeshwa. Nakala zaidi ya 500,000 katika Kiingereza zimefanyizwa, na sasa inapatikana (au itapatikana hivi karibuni) katika lugha nyinginezo 26.a
Itikio Limekuwa Nini?
Watu ambao si Mashahidi wa Yehova wameitikiaje vidio hiyo? Mfanya biashara mmoja aliandika hivi:
“Niliiona vidio hiyo kuwa ya hali ya juu sana. Nilivutiwa hasa na uangavu na utengenezaji mzuri sana wa picha zayo. Nilikuwa nikisahau-sahau kwamba ilikuwa vidio na kuifikiria mara nyingi kuwa sinema. Vidio hiyo ni lazima itakuwa yenye kutumika sana katika kueleza kusudi la makao makuu yenu ya New York. Pongezi kwa kifaa hicho chenye kutokeza.”—J. J.
Wale wanaojifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova wamenufaika na kuiona vidio hiyo. Yafuatayo hueleza kwa nini:
“Mimi hujifunza Biblia na kijana mwenye umri wa miaka 20 na ambaye huhudhuria chuo kikuu cha mahali hapa. Amekuwa akihangaikia hali ya ulimwengu inayozidi kuwa mbaya. Lakini, baada ya kuiona vidio hiyo na kuona ndugu wale wachanga wa Betheli wote wakiwa na kusudi la kweli maishani, mtazamo wake mzima ulibadilika. Alihudhuria Siku ya Kusanyiko la Pekee letu akaomba kujifunza Biblia mara mbili kwa juma. Mwanafunzi mwingine wa Biblia, mwalimu wa shule ya upili, aliazima vidio hiyo ili kuwaonyesha watu wake wa ukoo. Walifikiri kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa tu tengenezo dogo, dhaifu, lisilopendwa na wengi. Walishtuka kuona jinsi kazi yetu ilivyo ya duniani pote na mafanikio tunayopata, kwa msaada wa Yehova.”—J. B.
“Maneno hayawezi kuonyesha ile shangwe niliyohisi wakati mwanamke ninayejifunza naye Biblia alipoanza kutoa machozi ya shangwe na ya uthamini baada ya kuona vidio hiyo. Alisema hivi akiwa na machozi: ‘Mtu anaweza kukosaje kuona kwamba hili ndilo tengenezo la Mungu wa kweli Yehova? Sikujua kamwe kwamba watu hawa walikuwako.’ Kisha akasema: ‘Ninataka kubatizwa.’”—C. D.
“Tumekuwa na mafanikio mengi kwa kutumia vidio hiyo na wanafunzi wa Biblia. Usiku uliopita mume wa mmoja wa wanafunzi wa mke wangu alitutembelea. Alikuwa amepinga sana. Aliitazama vidio hiyo. Baadaye aliuliza maswali akaondoka hapa akiwa na Biblia na kile kitabu cha kujifunza Biblia Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. Mbeleni alikuwa amevichoma vichapo vyote vya mke wake!”—D. H.
Vijana pia wameona vidio hiyo kuwa yenye kuvutia, kama vile maelezo yafuatayo yanavyoonyesha:
“Mimi ni mwenye umri wa miaka sita na nusu. Nilipenda ile sehemu juu ya Biblia na wakati mabweta yaliposonga kwa kasi.”—K. W.
“Watoto wetu wachanga walisema kwamba ilikuwa bora kuliko kipindi chochote ambacho wameona kwenye televisheni.”—R. C.
“Baada ya kutazama vidio hiyo kwa mara ya pili, mwana wetu mwenye umri wa miaka mitano, aliyeitazama kwa makini muda wote, aliuliza hivi, ‘Je! twaweza kuiona kila siku?’ Binti yetu mwenye umri wa miaka mitatu akasema hivi kwa kupatana na hilo, ‘Ninataka kwenda Betheli na kutengeneza vitabu!’”—M. E.
“Watoto wangu Robin na Shannan, wenye miaka 12 na 9, hucheza vidio hiyo tena na tena. Binti yangu mchanga zaidi baada ya kuona vidio hiyo alitangaza hivi, ‘Ninapenda kwenda kwenye utumishi wa shambani. Ni jambo lenye kufurahisha sana.’ Tunahisi kwamba vidio hiyo imeathiri maisha ya familia yetu moja kwa moja. Inaburudisha kama nini kufungua kipindi cha televisheni ambacho wahisi ni salama kukitazama!”—N. B.
“Nina umri wa miaka 13 1/2. Vidio hiyo mpya ilinifanya nitambue jinsi ninavyopuuza yale maandalizi mazuri ajabu kutoka kwa Yehova. Ni pendeleo kuwa mmoja wa watu wa Mungu.”—K. W.
“Nina umri wa miaka 16, na vidio hiyo imesaidia kukazia upya akilini mwangu kwamba hiyo kazi inayofanywa ni ya duniani pote.”—A. M.
“Watoto wetu walisema kwamba vipindi vya kawaida vya televisheni viliacha kuwavutia kwa sababu ya kuona vile kitumbuizo cha kitheokrasi cha kweli kiwezavyo kuwa. Hiyo pia iliimarisha tamaa yao ya kuingia katika utumishi wa wakati wote.”—L. M.
Hata wale ambao wamekuwa Mashahidi wa Yehova kwa muda wa miaka mingi wamesukumwa na yale ambayo wameona.
“Ikiwa vidio hiyo inatuvutia jinsi hiyo tukiwa watu wa Yehova, itaweza kuwaathiri wengine zaidi kadiri gani? Mfumo huu unapokuwa mgumu sana kushughulikia, mimi huchukua muda wa saa moja ya wakati wangu na kuizuru Betheli nikiwa starehe ndani ya sebule yangu!”—K. B.
“Nilipoona ule uangalifu na ustadi unaopewa kila kazi, nilihisi kwenda chumbani mwangu na kukumbatia fasihi zangu za Biblia.”—L. P.
Tunakutia moyo pia, uchukue wakati ili kuona ile vidio Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name. Itakupa wewe maoni tofauti juu ya maisha na kukusaidia uwe na uhakika katika wakati ujao wenye usalama.
[Maelezo ya Chini]
a Lugha ya ishara ya Amerika, Kiarabu, Kibaske, Kikantonesia, Kikatalani, Kikroashia, Kicheki (cha Bohemia), Kidenmarki, Kiholanzi, Kifinlandi, Kifaransa, Kijerumani, Kigiriki, Kihangari, Kiitaliano, Kijapani, Kikorea, Kimandarini, Kinorwei, Kipolandi, Kireno (cha Brazili), Kireno (cha Ulaya), Kiromania, Kislovaki, Kihispania, Kiswede.