Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 11/15 kur. 21-24
  • Je, Ungeuzima Utambi Ufukao Moshi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Ungeuzima Utambi Ufukao Moshi?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuutazama Unabii
  • Matokeo ya Uchambuzi
  • Vipi Kulinganisha?
  • Njia Kadhaa za Kujenga
  • Sikuzote Uwe Mwenye Kujenga
  • Kutimiza Unabii wa Isaya
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Kutimiza Unabii wa Isaya
    Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
  • Atimiza Unabii wa Isaya
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
  • Sehemu Mpya ya Mkutano wa Katikati ya Juma
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2017
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 11/15 kur. 21-24

Je, Ungeuzima Utambi Ufukao Moshi?

YESU KRISTO alitangaza habari njema za Ufalme wa Mungu kwa watu wa namna zote. Wengi wao walikuwa wameonewa na kuvunjika moyo. Lakini Yesu aliwapa ujumbe wenye kutia moyo. Aliwaonea huruma watu wenye kuteseka.

Mathayo, mwandikaji wa Gospeli alikazia huruma ya Yesu kwa kuelekeza fikira kwa unabii ulioandikwa na Isaya. Akinukuu maneno yaliyotimizwa na Kristo, Mathayo aliandika: “Hakuna tete lililochubuliwa ambalo ataliponda, na hakuna utambi wa kitani-ghafi unaofuka moshi atakaouzima, mpaka atakapoipeleka haki kwa fanikio.” (Mathayo 12:20, NW; Isaya 42:3) Maneno haya yamaanisha nini, naye Yesu alitimizaje unabii huu?

Kuutazama Unabii

Kwa kawaida tete humea katika bwawa nalo si mmea wenye nguvu na uthabiti. “Tete lililochubuliwa” lingekuwa dhaifu kwelikweli. Hivyo linaonekana linawakilisha watu walioonewa na wanaoteseka kama yule mtu mwenye mkono uliopooza ambaye Yesu alimponya siku ya Sabato. (Mathayo 12:10-14) Lakini vipi kuhusu rejezo la kiunabii juu ya utambi wa taa?

Taa ya kawaida ya nyumbani ya karne ya kwanza W.K. ilikuwa chombo kidogo cha udongo kilichofanana na mtungi chenye kishikio kilichopinda. Kwa kawaida taa ilijazwa mafuta ya zeituni. Kwa uvutano, utambi uliotengenezwa kwa kitani ulivuta mafuta ili uendelee kuwaka. Bila shaka, ‘utambi ufukao moshi’ ungekuwa uliokaribia kuzimika.

Yesu alitangaza ujumbe wake wenye kutia moyo kwa wengi waliokuwa kama tete lililochubuliwa, lililopindika na kutupwa huku na huku. Watu hawa pia walikuwa kama utambi wa kitani-ghafi unaofuka moshi kwa sababu uhai wao wa mwisho ulikuwa karibu umekwisha. Kwa kweli walikuwa wameonewa na kuvunjika moyo. Hata hivyo, Yesu hakuponda tete la mfano lililochubuliwa au kuzima utambi wa ufananisho ufukao moshi. Maneno yake yenye upendo, wororo na huruma, hayakuendelea kuwavunja moyo na kuwashusha moyo watu waliokuwa wakiteseka. Badala ya hilo, maneno yake na jinsi alivyoshughulika nao yaliwatia moyo.—Mathayo 11:28-30.

Leo, pia, wengi wahitaji huruma na kitia-moyo kwa sababu wakabili matatizo yenye kuvunja moyo. Hata watumishi wa Yehova si wenye nguvu sikuzote chini ya matatizo. Nyakati nyingine wengine hufanana na tambi zifukazo moshi. Hivyo Wakristo wapaswa wawe wenye kutia moyo—wakichochea moto, kwa kitamathali—hivyo wakiimarishana.—Luka 22:32; Matendo 11:23.

Tukiwa Wakristo tunataka kuwa wenye kutiana moyo. Hatungejaribu kimakusudi kudhoofisha yeyote atafutaye msaada wa kiroho. Kwa kweli, tunatamani kuiga kielelezo cha Yesu katika kuwaimarisha wengine. (Waebrania 12:1-3; 1 Petro 2:21) Uhakika wa kwamba tungeweza kumponda bila kujua yeyote anayetutazamia kumtia moyo ni sababu nzuri ya kufikiria kwa uzito jinsi tunavyoshughulika na wengine. Kwa hakika hatutaki ‘kuuzima utambi ufukao moshi.’ Ni miongozo gani ya Kimaandiko inayoweza kutusaidia katika jambo hili?

Matokeo ya Uchambuzi

Mkristo ‘akichukua hatua fulani yenye kosa, wale walio na sifa za ustahili wa kiroho wapaswa kujaribu kumrekebisha upya mtu wa namna hiyo katika roho ya upole.’ (Wagalatia 6:1, NW) Hata hivyo, je, ingefaa kutafuta makosa madogo katika wengine na kuchukua kila fursa kuyarekebisha? Au je, ingefaa kuwasukuma wafanye vema zaidi kwa kudokeza kwamba jitihada zao za sasa hazitoshi, labda tukiwafanya wawe na hisia zenye hatia? Hakuna ushuhuda wa kwamba Yesu alifanya jambo la aina hiyo. Ingawa ni kusudi letu kusaidia wengine wafanye maendeleo, wale wanaochambuliwa bila fadhili huenda wakahisi kudhoofika badala ya kuimarika. Hata shauri lifaalo laweza kuwa lenye kuvunja moyo kwelikweli likitolewa kupita kiasi. Ikiwa jitihada zote za Mkristo mwenye kufanya yote apaswayo zingekosa kibali kila wakati, yaelekea aweza kuchoka na kusema, ‘Hakuna haja ya kujaribu?’ Kwa kweli, yaelekea aweza kukata tamaa kabisa.

Ingawa kutoa shauri la Kimaandiko ni jambo la maana, hakupaswi kuwe na mwelekeo unaowatambulisha wazee waliowekwa rasmi au wengine kutanikoni. Mikutano ya Kikristo haifanywi hasa ili kutoa na kupokea shauri. Badala ya hivyo, tunakutana kwa ukawaida ili kuimarishana na kutiana moyo ili kwamba wote wafurahie ushirika wao na utumishi wao mtakatifu kwa Mungu. (Warumi 1:11, 12; Waebrania 10:24, 25) Ni vema kama nini tunapofahamu tofauti kati ya kosa zito na kutokamilika ambako ni jambo la hekima na lenye upendo kuachilia!—Mhubiri 3:1, 7; Wakolosai 3:13.

Watu huitikia kitia-moyo haraka zaidi kuliko wanavyoitikia uchambuzi. Kwa kweli, watu mmoja-mmoja wahisipo wamechambuliwa isivyofaa, huenda wakashikilia hata zaidi tabia inayochambuliwa! Lakini wanaposifiwa ifaavyo, wanatiwa moyo, nao huchochewa kufanya maendeleo. (Mithali 12:18) Kama vile Yesu, acheni basi tuwe wenye kutia moyo na kamwe ‘tusiuzime utambi unaofuka moshi.’

Vipi Kulinganisha?

Kusikia mambo mazuri yaliyoonwa ya Wakristo wengine kwaweza kuwa jambo lenye kuchochea sana. Yesu mwenyewe aliona shangwe aliposikia juu ya mafanikio ya wanafunzi wake katika kuhubiri ujumbe wa Ufalme. (Luka 10:17-21) Vilevile, tusikiapo juu ya mafanikio, kielelezo chema, au uaminifu-maadili wa wengine walio katika imani, sisi twatiwa moyo na azimio letu la kushikilia mwendo wetu wa Kikristo latiwa nguvu.

Lakini, vipi ikiwa ripoti ilitolewa kwa njia inayodokeza, ‘Wewe si mwema kama Wakristo hawa, na unapaswa kufanya vizuri zaidi kuliko unavyofanya’? Je, inaelekea kwamba msikilizaji atafanya jitihada yenye bidii ya kufanya maendeleo? Inawezekana kwamba atavunjika moyo na labda kukata tamaa, hasa ikiwa mara nyingi milinganisho inafanywa au kudokezwa. Jambo hilo lingefanana sana na mzazi anayemuuliza mtoto wake, ‘Kwa nini usiwe kama ndugu yako?’ Maneno kama hayo huenda yakatokeza udhiko na kuvunjika moyo, na hayaelekei kupendekeza tabia njema. Milinganisho yaweza kuwa na matokeo kama hayo kwa watu wazima, hata ikiwafanya wawe na hali fulani ya kuwaudhikia wale wanaolinganishwa nao.

Hatuwezi kutazamia wote wafanye utumishi wa Mungu kwa kadiri moja. Katika mojapo la vielezi vya Yesu, bwana-mkubwa fulani aliwapa watumishi wake ama talanta moja, mbili, ama tano za fedha. Hizo zilipewa “kila mtu kwa kadiri ya uwezo wake.” Watumwa wawili waliozifanyiza talanta zao kazi kwa hekima na kuziongeza walisifiwa kwa sababu walikuwa waaminifu, ingawa kazi yao ilikuwa na matokeo tofauti-tofauti.—Mathayo 25:14-30.

Kwa kufaa mtume Paulo aliandika hivi: “Kila mtu na aipime kazi yake mwenyewe, ndipo atakapokuwa na sababu ya kujisifu ndani ya nafsi yake tu, wala si kwa mwenzake.” (Wagalatia 6:4) Basi, ili tuwe wenye kutia moyo wengine kihalisi, twapaswa kujaribu kuepuka kufanya milinganisho isiyofaa.

Njia Kadhaa za Kujenga

Tunaweza kufanya nini ili kujenga waliovunjika moyo na kuepuka ‘kuuzima utambi unaofuka moshi’? Kuandaa kitia-moyo si jambo la kufuata njia fulani hususa. Hata hivyo, yaelekea kwamba maneno yetu yatajenga wengine ikiwa tutatumia kanuni za Biblia. Ni zipi baadhi yazo?

Uwe mnyenyekevu. Kwenye Wafilipi 2:3, Paulo alitutolea shauri la upole kwamba ‘tusitende neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno.’ Badala ya hivyo, twapaswa kuzungumza na kutenda kwa unyenyekevu. ‘Kwa unyenyekevu, twapaswa kuwahesabu wengine kuwa bora kuliko nafsi yetu.’ Paulo hakusema kwamba tujione kuwa hatuna thamani. Lakini, tujue kwamba kila mtu ni bora kuliko sisi kwa njia fulani. Neno la Kigiriki hapa linalotafsiriwa “bora” hudokeza kwamba mtu “huacha kuangalia mapendeleo yake mwenyewe, na kwa bidii hufikiria uwezo wa mwingine ambao katika huo huyo ni bora.” (New Testament Word Studies, cha John Albert Bengel, Buku la 2, ukurasa 432) Tukifanya hivyo na kufikiria wengine kuwa bora, tutashughulika nao kwa njia ya unyenyekevu.

Onyesha heshima. Kwa kujieleza kwa unyofu, tunaweza kufanya iwe wazi kwamba tuna hakika na waamini wenzetu waaminifu, tukiwaona kuwa watu mmoja-mmoja watamanio kumpendeza Mungu. Lakini vipi wakihitaji msaada wa kiroho. Basi, acheni tuandae msaada kwa njia ya heshima na adabu. Paulo alieleza mambo hivi: “Katika kuonyeshana heshima nyinyi kwa nyinyi ongozeni.”—Warumi 12:10, NW.

Uwe msikilizaji mzuri. Ndiyo, ili kutia moyo wale ambao huenda wanakabili matatizo yenye kuvunja moyo, twahitaji kuwa wasikilizaji wazuri, si wenye kusema kwa njia ya kukemea. Badala ya kutoa madokezo ya haraka, ya kijuujuu tu, acheni tujipatie wakati unaohitajiwa ili kuandaa miongozo ya Kimaandiko inayotimiza mahitaji halisi yaliyopo. Ikiwa hatujui la kusema, utafiti wa Biblia utatusaidia kuzungumza kwa kufariji na kuimarisha wengine.

Uwe mwenye upendo. Tunahitaji kuhisi upendo kwa wale tunaotaka kutia moyo. Unapoelekezwa kwa watumishi wa Yehova wenzetu, upendo wetu unapaswa upite zaidi ya kuwatendea tu mema. Ni lazima uhusishe hisi za ndani. Ikiwa tuna upendo kama huo kwa watu wote wa Yehova, maneno yetu yatawatia moyo kikweli. Hata ikiwa tunahitaji kutoa dokezo fulani juu ya jambo la kufanyia maendeleo, haielekei kwamba tutakayosema yataeleweka vibaya au yasababishe dhara huku nia yetu ikiwa si kutoa maoni tu bali kutoa msaada wenye upendo. Kama Paulo alivyosema kwa kufaa, “upendo hujenga.”—1 Wakorintho 8:1; Wafilipi 2:4; 1 Petro 1:22.

Sikuzote Uwe Mwenye Kujenga

Katika hizi “siku za mwisho” zilizo hatari watu wa Yehova hukabili majaribu mengi. (2 Timotheo 3:1-5) Si ajabu kwamba nyakati nyingine wanavumilia hadi ule uonekanao kuwa ukomo wa uvumilivu wao. Tukiwa watumishi wa Yehova, kwa kweli hatungetaka kusema au kufanya mambo ambayo yaelekea kusababishia yeyote wa waabudu wenzetu kuhisi kama tambi zinazofuka moshi zilizo karibu kuzimika.

Basi, ni muhimu kama nini kwamba tutiane moyo! Acheni tufanye kila jitihada ili tuwe wenye kujenga kwa kuwa wanyenyekevu na wenye heshima kwa waabudu wenzetu waliovunjika moyo. Na tusikilize kwa makini watuambiapo mambo yao ya siri na sikuzote tutafute kuwasaidia kwa kuelekeza fikira zao kwa Neno la Mungu, Biblia. Zaidi ya yote, acheni tuonyeshe upendo, kwa kuwa tunda hili la roho takatifu ya Yehova litatusaidia kuimarishana. Kamwe tusizungumze au kutenda kwa njia yoyote iwezayo ‘kuuzima utambi ufukao moshi.’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki