Wapiga-Mbiu wa Ufalme Waripoti
“Acheni Nuru Yenu Ing’ae Mbele ya Watu”
KATIKA Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Nyinyi ndio nuru ya ulimwengu.” Yeye aliendelea kuwasihi sana hivi: “Acheni nuru yenu ing’ae mbele ya watu, ili wapate kuona kazi zenu bora na kumpa utukufu Baba yenu aliye katika mbingu.”—Mathayo 5:14-16.
Katika Italia kazi bora za Mashahidi wa Yehova zimeonekana. Kwa kielelezo, mwenendo wao mzuri wahudhuriapo mikusanyiko yao ya kila mwaka humletea Mungu sifa, kama ripoti zifuatazo zinavyothibitisha:
▪ Kwa miaka mingi mwanamke mmoja katika Terni, Italia, alisaidia bintiye kusimamia mkahawa uliokuwa karibu na stediamu jijini humo. Yeye asimulia hivi: “Niliona tofauti kubwa kati ya wale waliokuja hapo kwa ajili ya michezo ya soka na wajumbe kwenye mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova huko. Mashahidi walikuwa wenye kiasi zaidi katika mavazi yao, na walikuwa wenye kufuatia haki na wenye heshima. Nilikuwa najiuliza mara nyingi jinsi watu wa jamii mbalimbali walivyoweza kupatana vizuri hivyo.
“Siku moja Shahidi alinisimamisha barabarani naye akaniuliza kama nilijua jina la Mungu. Sikulijua, na kwa kuwa nilijua Mashahidi wa Yehova ni watu wema, nilikubali anitembelee. Nilikuwa na maswali juu ya hali ya wafu, aliyonijibu kutoka Biblia. Bila kukawia, nilikubali funzo la Biblia, na majuma mawili baadaye nilianza kuhudhuria mikutano.
“Mwanzoni binti yangu alinipinga, lakini mwenendo na azimio langu zilibadili mtazamo wake. Nilianza kujifunza miezi minane iliyopita. Leo binti yangu na mumeye hutoa maelezo yenye uthamini kwa Mashahidi wanaonunua vitu katika mkahawa wao. Kwa habari yangu, nilibatizwa kwenye mkusanyiko mmoja katika stediamu hiyo.”
▪ Baada ya mkusanyiko katika Roseto degli Abruzzi, meneja wa mahali pa kambi alisema hivi: “Nimeona kwamba Mashahidi wa Yehova ni watu wenye kufuatia haki sana katika lolote wafanyalo. Juma lililopita, nilikuwa na 40 wao mahali pangu pa kambi, na hawakusababisha matatizo yoyote. Tofauti na hilo, ni wao tu ambao huja na kukuambia ikiwa wana mtu wa ziada anayekaa katika trela au hema lao. Kwa upande wangu, wao ni wateja wazuri zaidi uwezao kupata.”
▪ Baada ya mkusanyiko huohuo, meneja wa hoteli alitaarifu hivi: “Mashahidi wa Yehova wote ni wenye amani. Wao si wenye mchafuko, na hulala mapema. Wao ni wenye fadhili kwa kweli, wenye kufuatia haki, na wenye tabia nzuri. Lingalikuwa jambo zuri ajabu kama kila mtu angalikuwa kama wao. Wengine huiba kila kitu—chupa za kutilia maua ya mapambo, visahani vya majivu, hata karatasi ya choo na sukari! Hakuna jambo kama hilo ambalo limetukia kwenu. Wakati watoto wenu wachukuapo aisikirimu kutoka katika friji jioni, sijisumbui kwenda kuchunguza kile ambacho wamechukua. Wao huhesabu kile niwadaicho na kuja kulipa mara moja. Nina itibari kamili katika wao. Jinsi lingalikuwa jambo zuri ajabu kama wengine wangalikuwa hivyo! Laiti wageni wangu wote wangalikuwa Mashahidi wa Yehova.”
Mashahidi wa Yehova wanajulikana sana Italia, kama ilivyo katika sehemu nyingine nyingi za dunia. Wao ‘hudumisha mwenendo wao ukiwa bora miongoni mwa mataifa,’ na hivyo kumletea sifa Mungu wa kweli, ambaye wanaitwa kwa jina lake.—1 Petro 2:12.