Wapiga-mbiu wa Ufalme Waripoti
Kutumia Kila Fursa
MASHAHIDI WA YEHOVA wanajulikana ulimwenguni pote kwa sababu ya kazi yao ya kufundisha watu Biblia. Lakini wao pia huongoza programu ambazo huletea jamii manufaa zilizo tofauti. Utumishi huo wa umma umepokewa vizuri, kama vile ionyeshwavyo na mambo yaliyoonwa ya Ekuado yafuatayo.
◻ Wasimamizi wa kiwanda fulani kikubwa cha kutengeneza vioo walitaka kuandaa mtaala kuhusu maadili ya kifamilia kwa ajili ya waajiriwa wao. Mkurugenzi wa mali za kibinadamu aliwaalika makasisi kadhaa wa Kikatoliki washiriki, lakini hakupata itikio lolote. Kasisi mmoja alimwambia kwamba, makasisi waliostahili kuzungumzia habari hiyo walikuwa wachache sana hivi kwamba, yaelekea hakuna yeyote angepatikana. Aliposikia jambo hilo, mwajiriwa fulani Shahidi alifanya mipango ili ndugu ambaye mara nyingi huhubiri maeneo ya biashara aweze kuzuru kiwanda hicho.
Siku ileile iliyofuata, huyo Shahidi alimfikia mkurugenzi wa mali za kibinadamu akiwa na mtaala wa funzo ulionuiwa kufanywa. Orodha ya habari ilikusanywa kutoka katika vichapo mbalimbali vya Watch Tower Society. Huyo mkurugenzi alivutiwa. Akachagua vichwa vitatu kwa ajili ya mazungumzo—uhusiano wa kibinadamu, maadili kazini, na maadili katika familia. Kisha mipango ikafanywa ili hiyo habari ichunguzwe pamoja na wafanyakazi wote.
Waajiriwa waligawanywa katika vikundi vya watu 30 kila kimoja, na baadaye ndugu watatu wenye kustahili wakawatolea hiyo habari. Matokeo yakawa nini? Hesabu kubwa ya waajiriwa waliomba watembelewe nyumbani mwao, na vichapo vya kujifunzia Biblia 216 vikaangushwa. Wasimamizi walivutiwa sana hivi kwamba waliomba kama hao Mashahidi wangeweza kutayarisha mfululizo mwingine wa hotuba.
◻ Hivi karibuni, Ekuado ilipitisha sheria ambayo huruhusu dini ifunzwe shuleni. Dada fulani mishonari alimzuru msimamizi wa kike wa shule fulani ya msingi na kumwuliza jinsi hiyo sheria mpya ilivyokuwa ikifanya kazi. Huyo msimamizi alieleza kwamba jaribio lilifanywa kuanzisha programu ya ibada ya Maria lakini jambo hilo halikufaulu kamwe. Wakati dada aliposema kwamba ibada ya namna hiyo ingetokeza matatizo kwa watoto wasio Wakatoliki, huyo msimamizi alikubali. “Hata hivyo,” huyo mishonari akasema, “tuna programu ya kufundisha kanuni za adili kutoka katika Biblia ambayo hailazimishi mtu kukubali dini fulani mahususi.” Huyo msimamizi alijibu kwa kuuliza hivi: “Waweza kuja lini? Kesho-kutwa?” Baada ya huyo mishonari kumwonyesha kitabu Kumsikiliza Mwalimu Mkuu, iliamuliwa kwamba wangechunguza sura “Wenye Furaha Ni Wenye Amani.”
Aliporudi, huyo mishonari alitumia muda wa saa tatu akizuru madarasa saba tofauti, huyo msimamizi akisikiliza. Baada ya kipindi cha mazungumzo na darasa la tano, mwanafunzi mmoja alisema hivi: “Bi., tafadhali hakikisha unazuru darasa la sita. Sikuzote wao hujaribu kutupiga ili kuanzisha pigano!” Mwalimu mmoja alisema hivi: “Jeuri ni mazungumzo muhimu sana. Twahitaji muda zaidi kuzungumzia habari hiyo.”
Mipango ilifanywa kwa ajili ya kufanya ziara za kurudia kwenye hiyo shule ili kuzungumzia vichwa kama utii na kusema uwongo. Kufikia sasa, matokeo yamekuwa yenye kuridhisha sana. Sasa huyo dada mishonari atembeapo barabarani, watoto huja mbio kumsalimu na kumwuliza maswali ya Biblia. Kwa fahari wengine humjulisha kwa wazazi wao. Kwa kuongezea hayo, funzo la Biblia nyumbani limeanzishwa pamoja na watoto wawili wa shule.