Sababu Inayowafanya Watu Fulani Wabadili Dini Yao
Kwa watu wengi, dini ni kibandiko tu. Huenda kikaonyesha mahali ambapo pindi kwa pindi mtu fulani huenda Jumapili, mahali afungiapo ndoa, na mahali ambapo atazikiwa. Lakini hakisemi yeye ni mtu wa aina gani au yeye anajua na kuamini nini. Kwa kielelezo, uchunguzi mmoja ulifunua kwamba asilimia 50 ya wanaodai kuwa Wakristo hawakujua ni nani aliyetoa Mahubiri ya Mlimani. Lo! kwani hata kiongozi wa India ajulikanaye sana, Mohandas Gandhi, wa dini ya Hindu, alijua jambo hilo!
JE, NI ajabu kwamba watu hupeperuka kutoka katika dini ilhali wengi wao wanajua machache sana juu ya imani yao? La, si ajabu. Hata hivyo, si jambo lisiloweza kuepukwa. Wale ambao wamekubali kujifunza Biblia mara nyingi hushangaa kupata kujua jinsi iwezavyo kuwanufaisha. Biblia yenyewe husema hivi: “Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.”—Isaya 48:17, italiki ni zetu.
Watu wenye njaa ya kiroho isiyotoshelezwa wapaswa kufanya nini? Hawapaswi kuacha kumtumikia Mungu! Badala ya hivyo, wanapaswa kutafuta katika Biblia na kuona kile ambacho Mungu mwenyewe huwezesha kipatikane kwa faida yao.
Majibu ya Maswali Magumu
Akiwa na umri wa miaka saba, Bernd alimtazama mama yake akifa.a Katika maisha yake yote yaliyosalia, alijiuliza, ‘Mama yangu yuko wapi? Mbona nalazimika kukua bila yeye?’ Akiwa tineja, Bernd alikuwa mshiriki-mtendaji wa kanisa. Akihangaishwa na kuteseka kwa binadamu, alitumaini kuwa mfanyakazi wa kusaidia nchi za kigeni. Hata hivyo, alisumbuliwa na maswali ambayo kanisa lake halikuweza kutoa majibu yenye kuridhisha.
Kisha Bernd akazungumza na mwanashule mwenzake ambaye alitukia kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kijana huyo alimwonyesha Bernd kutoka katika Biblia kwamba mama yake hakuwa na fahamu, alikuwa amelala katika kifo. Bernd alijifunza mistari mingi ya Biblia ambayo ilieleza jambo hilo, kama vile Mhubiri 9:5: “Wafu hawajui neno lo lote.” Kwa hiyo Bernd hakuwa na sababu yoyote ya kuwa na wasiwasi juu ya ikiwa mama yake alikuwa akiteseka katika aina fulani ya purgatori—au katika hali mbaya zaidi. Ingawa dini nyingi hufundisha kwamba nafsi haiwezi kufa, Bernd aliona katika Biblia kwamba nafsi ya binadamu ni mtu tu. Mtu afapo, nafsi hufa. “Nafsi inayofanya zambi, itakufa.”—Ezekieli 18:4, Zaire Swahili Bible.
Bernd alipata pia kujua juu ya tazamio la wafu. Alijisomea kitabu cha Biblia cha Matendo: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Alisisimka kama nini kujua kwamba ufufuo huo ungetukia katika dunia ambayo Mungu angeifanya iwe paradiso tena!—Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3, 4.
Upesi mahitaji ya kiroho ya Bernd yakatoshelezwa na ujuzi wa kweli wa Biblia. Bernd hakuiacha dini. Badala ya hivyo, aliacha kanisa ambalo halingeweza kutosheleza njaa yake na kukubali aina ya ibada iliyotegemea Biblia kabisa. Yeye asema hivi: “Hiyo ilikuwa miaka 14 iliyopita, nami sijawahi kujuta kamwe kwamba nilichukua hatua hiyo. Sasa najua kwamba Muumba hasababishi kuteseka. Shetani ndiye mungu wa mfumo huu, naye ndiye husababisha hali zinazotuzunguka. Lakini karibuni Mungu atarekebisha madhara yote ambayo yamefanywa na ulimwengu wa Shetani. Mama yangu pia atafufuka. Hiyo itakuwa shangwe kama nini!”
Bernd amefikia mradi wake wa kufanya kazi ya kusaidia watu katika nchi ya kigeni. Anafanya kazi katika nchi ya kigeni akiwasaidia wengine wajifunze juu ya Ufalme wa Mungu, utatuzi pekee kwa taabu zao. Sawa na Bernd, mamilioni ya watu wamejifunza kwamba karibuni Mungu atakomesha kuteseka kwa binadamu. Wanasisimka kujua kwamba kuna dini inayotosheleza mahitaji yao ya kiroho.—Mathayo 5:3.
Kusudi la Uhai Ni Nini?
Ulimwengu wa Magharibi unapozidi kuiacha dini, watu wengi huuliza, ‘Kusudi la uhai ni nini?’ Jibu lapatikana katika Biblia, kama vile Michael alivyogundua. Miaka ya katikati ya 1970, Michael alitaka kujiunga na kikundi cha magaidi. Alikuwa na kusudi moja tu maishani—kushambulia watu ambao kwa maoni yake ndio waliosababisha ukosefu wa haki katika mfumo wa ubepari. “Sikutoka nyumbani kwangu kamwe bila bunduki yangu,” yeye asema. “Nilipanga kuwaua wanasiasa wa cheo cha juu na wabepari wengi iwezekanavyo. Nilikuwa tayari kufa kwa kusudi hilo.”
Michael alikuwa mwenda-kanisani, lakini hakuna yeyote kanisani kwake angeweza kueleza kusudi halisi la uhai. Kwa hiyo Mashahidi wa Yehova walipomtembelea nyumbani na kumwonyesha majibu ya maswali yake kutoka katika Biblia, Michael alisikiliza kwa makini. Alianza kuhudhuria mikutano ya ibada kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova lililokuwa mahali hapo.
Rafiki za Michael walitaka kujua juu ya upendezi wake mpya katika Biblia. “Njooni kwenye mkutano Jumapili hii,” Michael akawahimiza. “Kaeni kwa muda fulani. Msipopendezwa na mnayosikia, basi mwende nyumbani.” Ndivyo ilivyotukia, baada ya hotuba yenye kutegemea Biblia ya dakika 45, wengi wa rafiki zake waliondoka. Isipokuwa mmoja—Susan—alibaki. Mwanamke huyo mchanga alivutiwa sana na yale aliyokuwa amesikia. Baadaye Michael na Susan walioana nao wakabatizwa wakiwa Mashahidi wa Yehova. “Sasa najua ni kwa nini tuko hapa duniani,” asema Michael. “Tuliumbwa na Yehova. Kusudi letu halisi maishani ni kupata kumjua na kufanya mapenzi yake. Hilo ndilo jambo ambalo huleta uradhi wa kweli!”
Mamilioni ya watu wana usadikisho kama wa Michael. Wao huzingatia maneno haya ya Biblia: “Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; Mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu.”—Mhubiri 12:13.
Kukabiliana na Matatizo ya Maisha
Sisi sote hujionea kutimizwa kwa unabii upatikanao kwenye 2 Timotheo 3:1: “Siku za mwisho nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa.” Hakuna awezaye kuponyoka matatizo ya “nyakati [hizi] zenye hatari.” Lakini Biblia hutusaidia kukabiliana nazo.
Wafikirie Steven na Olive, wenzi wa ndoa. Walipoanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, wao, kama wengine, walikuwa na matatizo ya ndoa. “Pengo kati yetu lilikuwa likiongezeka,” aeleza Steven. “Tulikuwa na miradi tofauti na mapendezi tofauti.” Ni nini kilichowasaidia kukaa pamoja? “Mashahidi wa Yehova walituonyesha jinsi ambavyo tungeweza kutumia kanuni za Biblia maishani mwetu,” Steven aendelea kusema. “Kwa mara ya kwanza, tukapata kujua maana ya kutokuwa na ubinafsi na kuwa wenye kujali. Kutumia kanuni za Biblia kulituunganisha. Sasa twafurahia ndoa yenye furaha na iliyo thabiti.”
Uhusiano wa Karibu Pamoja na Mungu
Kulingana na uchunguzi wa majuzi uliofanywa na shirika la Gallup, asilimia 96 ya Wamarekani humwamini Mungu, na wengi wao humwomba. Hata hivyo, mahoji mengine yaliyofanywa yalionyesha kwamba hudhurio katika kanisa na sinagogi sasa limefikia kiwango cha chini zaidi kwa muda wa nusu karne. Asilimia 58 ya Wamarekani husema kwamba wao huenda kanisani mara moja kwa mwezi au baada ya muda mrefu zaidi. Ni dhahiri kwamba dini haijawavuta watu karibu zaidi na Mungu. Na tatizo hilo haliko Marekani peke yake.
Linda alikulia Bavaria. Alikuwa Mkatoliki naye alisali kwa ukawaida. Wakati uo huo, aliogopa wakati ujao. Hakujua lolote juu ya kusudi la Mungu kwa mwanadamu. Alipokuwa na umri wa miaka 14 tu, Linda alikutana na Mashahidi wa Yehova, naye aripoti hivi: “Mambo waliyoniambia yalikuwa yenye kuvutia, kwa hiyo nikachukua vichapo viwili vya kujifunza Biblia nami nikavisoma mara tu nilipovipata.” Miaka miwili baadaye, Linda alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. “Kila kitu nilichojifunza kuhusu Mungu katika Biblia kilieleweka,” yeye asema. Linda alijiuzulu kutoka katika kanisa lake, akabatizwa kuwa Shahidi wa Yehova akiwa na umri wa miaka 18.
Ni nini kilichomsukuma Linda abadili dini yake? Yeye aeleza hivi: “Kanisa langu lilinisaidia kujua kwamba kuna Mungu, nami nilijifunza kuwa na imani kwake. Lakini Mungu hakuwa halisi. Kujifunza kwangu Biblia kulithibitisha imani yangu katika Mungu na pia kulinisaidia kumjua na kumpenda. Sasa nina uhusiano wenye thamani sana pamoja na Mungu, jambo ambalo ni lenye thamani sana kuliko kitu kingine chochote.”
Dini ya Kweli Yafaa!
Je, dini yako hukupa mwongozo wa kiroho na kukuonyesha jinsi Biblia iwezavyo kukusaidia kukabiliana na matatizo ya maisha? Je, dini hiyo hufundisha tumaini la Biblia juu ya wakati ujao? Je, hiyo hukuleta kwenye uhusiano wa karibu na wa kibinafsi pamoja na Muumba, kwa kutegemea ujuzi sahihi juu ya Biblia? Ikiwa sivyo, usikate tamaa. Badala ya kuiacha dini, tafuta aina ya ibada ambayo hutegemea Biblia kabisa. Kisha utakuwa sawa na wale waliotabiriwa katika kitabu cha Biblia cha Isaya: “Bwana MUNGU asema hivi, Tazama, watumishi wangu watakula . . . watumishi wangu watakunywa . . . watumishi wangu watafurahi . . . watumishi wangu wataimba kwa furaha ya moyo.”—Isaya 65:13, 14.
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.
[Picha katika ukurasa wa 4, 5]
Biblia hutusaidia kupata kumjua Mungu na kumpenday