Zidi Kufanya Maendeleo ya Kiroho!
Siku ya kubatizwa kwetu ndiyo siku tupaswayo kuithamini sana na kuikumbuka sikuzote. Kwa kuwa, ndiyo siku tujulishapo waziwazi kwamba tumejiweka wakfu ili kumtumikia Mungu.
WATU wengi hujitahidi sana kufikia hatua hiyo—kuacha mazoea mabaya ya muda mrefu, kuepukana na mashirika yasiyofaa, kubadili namna ya kufikiri na mwenendo uliozoewa sana.
Hata hivyo, ingawa ubatizo ni tukio la kufurahisha na la maana maishani mwa Mkristo, bado huo ni mwanzo tu. Mtume Paulo aliwaambia Wakristo waliobatizwa katika Yudea hivi: “Sasa tumeacha fundisho la msingi juu ya Kristo, acheni tuzidi kusonga mbele kwenye ukomavu.” (Waebrania 6:1) Naam, Wakristo wote wanahitaji “[kuufikia] umoja katika imani na katika ujuzi sahihi wa Mwana wa Mungu, kufikia kuwa mwanamume aliyekua kabisa, kufikia kipimo cha kimo ambacho ni cha ujao wa Kristo.” (Waefeso 4:13) Twaweza “kuimarishwa katika imani” ikiwa tu tumefanya maendeleo kufikia hatua ya ukomavu.—Wakolosai 2:7.
Katika kipindi cha miaka michache iliyopita, mamia ya maelfu ya waabudu wapya waliojiweka wakfu wameingia katika kutaniko la Kikristo. Huenda wewe ni mmoja wao. Sawa na ndugu zako wa karne ya kwanza, hutaki kuendelea kuwa mchanga kiroho. Wataka kukua, kufanya maendeleo! Lakini vipi? Na ni zipi baadhi ya njia unazoweza kufanya maendeleo?
Kufanya Maendeleo Kupitia Funzo la Kibinafsi
Paulo aliwaambia Wakristo katika Filipi hivi: “Hili ndilo mimi huendelea kusali, kwamba upendo wenu upate kuzidi bado hata zaidi na zaidi pamoja na ujuzi sahihi na ufahamu kamili.” (Wafilipi 1:9) Kukua katika “ujuzi sahihi” ni jambo la maana sana katika maendeleo yako ya kiroho. ‘Kuendelea kutwaa ujuzi juu ya Yehova Mungu na Yesu Kristo’ ni hatua yenye kuendelea, si jambo ambalo hukoma baada ya ubatizo.—Yohana 17:3.
Dada mmoja Mkristo, tutakayemwita Alexandra, alikuja kung’amua hilo miaka kumi baada ya kubatizwa akiwa na umri wa miaka 16. Alilelewa katika kweli naye alihudhuria mikutano ya Kikristo na kushiriki katika kazi ya kuhubiri kwa ukawaida. Yeye aandika hivi: “Miezi michache ambayo imepita, niling’amua kwamba jambo fulani halikuwa sawa hata kidogo. Niliamua kujichunguza kikweli, ninachohisi juu ya kweli, na kwa nini bado niko katika kweli.” Aligundua nini? Aendelea kusema hivi: “Niligundua kwamba sababu za kuwa kwangu katika kweli zilikuwa zikinisumbua. Nilikumbuka kwamba nilipokuwa nikikua, mikutano na utumishi wa shambani ni mambo yaliyokaziwa. Ilikuwa kana kwamba kwa njia fulani mazoea ya kujifunza kibinafsi na kusali yangejitokeza tu. Lakini nilichanganua hali yangu, nikang’amua kwamba hilo halikutukia.”
Mtume Paulo ahimiza hivi: “Kwa kadiri ambayo tumefanya maendeleo, acheni tuendelee kutembea kwa utaratibu katika kawaida hiyohiyo.” (Wafilipi 3:16) Kufanya jambo kwa ukawaida kwaweza kusitawisha mwendo wa kusonga mbele. Kabla hujabatizwa, bila shaka ulijifunza Biblia kwa ukawaida kila juma na mwalimu anayestahili. Uthamini wako ulipozidi, ulianza kutayarisha somo la kila juma kwa ukawaida, ukisoma katika Biblia maandiko yaliyotajwa, na kadhalika. Tangu ulipobatizwa, je, umeendelea ‘kutembea katika kawaida hiyohiyo’?
Ikiwa sivyo, huenda ukahitaji kuchunguza tena mambo unayotanguliza, “[uki]hakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Wafilipi 1:10) Katika maisha yetu yenye shughuli nyingi, twahitaji kujidhibiti ili kutenga wakati wa kusoma na kujifunza Biblia. Lakini jitihada hizo si za bure, kuna manufaa. Fikiria tena kisa cha Alexandra. “Lazima niseme kwamba nimeendelea kuwa katika kweli kwa miaka 20 hivi iliyopita kwa kwenda kwenye mikutano na kushiriki katika huduma ya shambani tu,” yeye akiri. Hata hivyo, aendelea kusema, “nimekata kauli kwamba ingawa mambo yote hayo ni ya maana, hayawezi kuniendeleza mambo yaanzapo kuwa magumu. Nimepata kung’amua yote hayo kwa kuwa sina mazoea yoyote ya kujifunza kibinafsi, nazo sala zangu hazina mbele wala nyuma na ni za kijuujuu tu. Nang’amua kwamba lazima sasa nibadili kufikiri kwangu na kuanza programu yenye maana ya kujifunza ili niweze kumjua Yehova kwelikweli na kumpenda na kuthamini kile ambacho Mwana wake ametupatia.”
Ikiwa wahitaji msaada katika kusitawisha kawaida nzuri ya kujifunza kibinafsi, wazee na Wakristo wengine wakomavu katika kutaniko lako watafurahi kukusaidia. Kwa kuongezea, makala katika Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 1995; la Agosti 15, 1993; na la Mei 15, 1986, zina madokezo yenye kusaidia.
Uhitaji wa Kumkaribia Mungu
Eneo jingine upaswalo kujitahidi kufanya maendeleo ni katika uhusiano wako na Mungu. Katika visa fulani huenda hata kukawa na uhitaji mkubwa kwa habari hii. Mfikirie Anthony, aliyebatizwa akiwa mchanga. “Nilikuwa mtoto wa kwanza katika familia yetu kubatizwa,” yeye asimulia. “Baada ya kubatizwa, nilikumbatiwa kwa shauku na mama yangu. Sikuwa nimewahi kumwona akiwa mwenye furaha hivyo. Kulikuwa na shangwe nyingi kwelikweli, nami nilijihisi mwenye nguvu sana.” Hata hivyo, kulikuwepo na sababu nyingine ya kuwepo na shangwe nyingi hivyo. “Kwa muda mrefu, hakukuwa vijana wowote waliobatizwa katika kutaniko letu,” Anthony aendelea. “Kwa hiyo nilijivuna sana. Pia nilijivunia maelezo yangu na hotuba zangu mikutanoni. Kusifiwa na kukubaliwa na watu kukawa jambo la maana zaidi kuliko kumletea Yehova sifa. Kwa kweli sikuwa na uhusiano wa karibu naye.”
Sawa na Anthony, huenda watu fulani wakawa wamejiweka wakfu, wakitaka kuwapendeza watu wengine badala ya kutaka kumpendeza Yehova. Ingawa hivyo, Mungu huwatarajia watu hao watimize ahadi yao ya kumtumikia. (Linganisha Mhubiri 5:4.) Mara nyingi ni vigumu kwao kufanya hivyo ikiwa hawampendi Mungu kibinafsi. Anthony akumbuka: “Ile shangwe kubwa niliyokuwa nayo nilipobatizwa ilikuwa ya punde tu. Mwaka mmoja haukupita kabla sijafanya kosa zito na kukaripiwa na wazee wa kutaniko. Kurudia-rudia mwenendo mbaya kulinifanya nitengwe na ushirika wa kutaniko. Miaka sita baada ya kujiweka wakfu kwa Yehova, nilikamatwa na kufungwa kwa sababu ya kuua kimakusudi.”
Kusitawisha Uhusiano wa Karibu na Yehova
Hata hali yako mwenyewe iweje, Wakristo wote wanaweza kuitikia mwaliko huu wa Biblia: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia.” (Yakobo 4:8) Bila shaka ulisitawisha kiasi fulani cha ukaribu na Mungu ulipojifunza Biblia mara ya kwanza. Ulijifunza kwamba Mungu si yule mungu wa kuwaziwa tu anayeabudiwa katika Jumuiya ya Wakristo, bali ni mtu mwenye jina, Yehova. Pia, ulijifunza kwamba yeye ni “mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli.”—Kutoka 34:6.
Hata hivyo, ili utimize wakfu wako wa kumtumikia Mungu, wapaswa kumkaribia hata zaidi! Vipi? Mtunga-zaburi alisali hivi: “Ee BWANA, unijulishe njia zako, unifundishe mapito yako.” (Zaburi 25:4) Kujifunza Biblia kibinafsi na vichapo vya Sosaiti kwaweza kukusaidia umjue Yehova vizuri zaidi. Pia kusali kutoka moyoni kwa ukawaida ni kwa maana. “Ifunueni mioyo yenu mbele zake,” ahimiza mtunga-zaburi. (Zaburi 62:8) Uonapo sala zako zikijibiwa, utahisi kwamba Mungu anapendezwa nawe kibinafsi. Hilo litakusaidia kuhisi ukiwa karibu zaidi naye.
Majaribu na matatizo hutoa fursa nyingine ya kumkaribia Mungu. Huenda ukakabili magumu na mitihani ya imani, kama vile ugonjwa, mikazo shuleni na kazini, au ugumu wa kiuchumi. Huenda hata ikawa kwamba lile zoea la kawaida la kushiriki katika huduma, kuhudhuria mikutano, au kujifunza Biblia na watoto wako ni gumu kwako. Usikabili matatizo hayo ukiwa peke yako! Msihi Mungu akuongoze na kukuelekeza. (Mithali 3:5, 6) Mwombe akupe roho yake takatifu! (Luka 11:13) Uonapo Mungu akikusaidia kwa upendo, utavutwa karibu zaidi naye. Kama vile mtunga-zaburi Daudi alivyosema, “Onjeni mwone ya kuwa BWANA yu mwema; heri mtu yule anayemtumaini.”—Zaburi 34:8.
Namna gani Anthony? “Nilianza kufikiria wakati nilipokuwa na miradi mingi kwelikweli ya kiroho iliyohusisha kufanya mapenzi ya Yehova,” yeye akumbuka. “Hilo liliumiza. Lakini kupitia maumivu hayo yote na kutamaushwa, niliukumbuka upendo wa Yehova. Ilichukua muda fulani kabla sijaweza kusali kwa Yehova, lakini nilisali, nikamfunulia moyo wangu wote, na kumwomba msamaha. Pia nilianza kujifunza Biblia nami nilishangaa kujua kadiri nilivyokuwa nimeisahau na jinsi kwa kweli nilijua machache sana juu ya Yehova.” Ingawa bado Anthony hajamaliza kifungo chake kwa sababu ya uhalifu wake, yeye husaidiwa na Mashahidi wenyeji naye anaelekea kupona kiroho. Kwa shukrani, Anthony asema hivi: “Kwa sababu ya Yehova na tengenezo lake, nimeweza kuuvua utu wa hapo zamani, nami najitahidi kuuvaa utu mpya kila siku. Uhusiano wangu na Yehova ni wa maana zaidi kwangu sasa.”
Maendeleo ya Kiroho Katika Huduma Yako
Yesu Kristo aliamuru wafuasi wake wawe wahubiri wa ‘habari njema ya ufalme.’ (Mathayo 24:14) Ukiwa mhubiri mpya wa habari njema kwa kulinganishwa, huenda usiwe na uzoefu sana katika huduma. Basi, waweza kufanyaje maendeleo ili ‘utimize kikamili huduma yako?’—2 Timotheo 4:5.
Njia moja ni kusitawisha mtazamo ufaao. Jifunze kuona kazi ya kuhubiri kuwa “hazina,” kuwa ni pendeleo. (2 Wakorintho 4:7) Ni fursa ya kuonyesha upendo wetu, uaminifu-mshikamanifu wetu, na uaminifu-maadili wetu kwa Yehova. Hutuwezesha pia kuonyesha kwamba twawahangaikia jirani zetu. Kujitoa bila ubinafsi katika huduma kwaweza kutokeza furaha ya kweli.—Matendo 20:35.
Yesu mwenyewe aliiona kazi ya kuhubiri kwa njia inayofaa. Kuwaambia wengine kweli za Biblia kulikuwa sawa na “chakula” kwake. (Yohana 4:34) Kwa hiyo, kilichomchochea kuwasaidia wengine chaweza kuelezwa kifupi kwa alilosema, “nataka.” (Mathayo 8:3) Yesu aliwahurumia watu, hasa waliokuwa “[wa]mechunwa ngozi na kutupwa huku na huku” na ulimwengu wa Shetani. (Mathayo 9:35, 36) Je, wewe vilevile ‘wataka’ kusaidia walio gizani kiroho na wanaohitaji kuelimishwa juu ya Neno la Mungu? Basi utahisi ukishurutishwa kuitikia amri hii ya Yesu: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” (Mathayo 28:19) Kwa kweli, utachochewa kushiriki kikamili katika kazi hii kwa kadiri afya na hali zako zikuruhusuvyo.
Ufunguo mwingine wa kufanya maendeleo ni kushiriki kwa ukawaida katika huduma—kila juma ikiwezekana. Kufanya hivyo kwaweza kukusaidia kuondolea mbali wasiwasi na hofu iwezayo kumzuia mtu ambaye huhubiri pindi kwa pindi tu. Kushiriki kwa ukawaida katika utumishi wa shambani kutakunufaisha katika njia nyingine pia. Kutakufanya uthamini kweli zaidi, usitawishe upendo wako kwa Yehova na kwa jirani, na kukusaidia kuendelea kukaza fikira kwenye tumaini la Ufalme.
Hata hivyo, vipi ikiwa hali yako ya sasa yapunguza sana kushiriki kwako katika kazi ya kuhubiri? Ikiwa kwa wazi hakuna mabadiliko yoyote uwezayo kufanya, basi farijika kwa kujua kwamba Mungu anapendezwa na lolote uwezalo kufanya, maadamu u mwenye nafsi yote katika utumishi wako. (Mathayo 13:23) Huenda waweza kufanya maendeleo katika njia nyingine, kama vile katika kuboresha stadi zako za kuhubiri. Kutanikoni, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi huandaa mazoezi mazuri kuhusiana na hilo. Kwa kawaida, kadiri tunavyozidi kuwa hodari katika huduma, ndivyo tutakavyoionea shangwe na kupata matokeo.
Basi, ni wazi kwamba, mtu hapaswi kukoma kufanya maendeleo ya kiroho abatizwapo. Mtume Paulo aliandika hivi kuhusu tumaini lake la kupata uhai usioweza kufa katika mbingu: “Akina ndugu, bado mimi sijifikirii mwenyewe kuwa nimekwisha kulishika hilo; bali kuna jambo moja juu ya hilo: Nikisahau mambo ya nyuma na kujinyoosha mbele kwenye mambo ya mbele, ninafuatilia sana kuuelekea mradi kwa ajili ya tuzo la mwito wa Mungu wa kwenda juu kwa njia ya Kristo Yesu. Basi, acheni wengi wetu kadiri tulivyo wakomavu, tuwe na mtazamo huu wa akili; na mkiwa na mwelekeo wa akili ulio tofauti katika jambo lolote, Mungu atawafunulia nyinyi mtazamo huo.”—Wafilipi 3:13-15.
Naam, Wakristo wote, iwe tumaini lao ni uhai usioweza kufa katika mbingu au uhai udumuo milele katika Paradiso duniani, lazima ‘wajinyooshe mbele—kana kwamba wanajikaza ili kufikia mradi wa uhai! Ubatizo wako ulikuwa mwanzo mzuri, lakini huo ni mwanzo tu. Endelea kujitahidi kufanya maendeleo ya kiroho. Kupitia mikutano na kujifunza kibinafsi, ‘uwe mtu mzima katika nguvu za kuelewa.’ (1 Wakorintho 14:20) Uwe mwenye “kuweza kufahamu kiakili . . . upana na urefu na kimo na kina” cha kweli. (Waefeso 3:18) Maendeleo unayofanya yatakusaidia kudumisha shangwe na furaha sasa na pia yatakusaidia kupata mahali salama katika ulimwengu mpya wa Mungu, ambapo chini ya utawala wa Ufalme wake wa kimbingu, utaweza kufanya maendeleo milele!
[Picha katika ukurasa wa 29]
Kupata wakati wa kujifunza kibinafsi hutaka kujidhabihu
[Picha katika ukurasa wa 31]
Kuwa na mtazamo ufaao kwaweza kutusaidia kupata shangwe katika huduma