Sitawisha Moyo wa Kumhofu Yehova
“Laiti wangekuwa na moyo kama huu ndani yao sikuzote, wa kunicha [“kunihofu” “NW”], na kushika amri zangu zote sikuzote.”—KUMBUKUMBU LA TORATI 5:29.
1. Tunawezaje kuwa na hakika kwamba siku moja watu wataishi bila hofu?
WANADAMU wamesumbuliwa na hofu kwa karne nyingi. Mamilioni ya watu wanaendelea kusumbuka kwa sababu ya hofu inayosababishwa na njaa, magonjwa, uhalifu, au vita. Kwa sababu hiyo dibaji ya Azimio la Haki za Binadamu inatangaza nia ya kutokeza ulimwengu ambao wanadamu wote wataishi bila hofu.a Jambo la kufurahisha ni kwamba, Mungu mwenyewe anatuhakikishia kuwa ulimwengu huo utatokea—lakini si kwa jitihada za wanadamu. Kupitia nabii wake Mika, Yehova anaahidi kwamba katika ulimwengu wake mpya wenye uadilifu, ‘hapana mtu atakayewatia watu wake hofu.’—Mika 4:4.
2. (a) Maandiko hutuhimizaje tumhofu Mungu? (b) Ni maswali gani yanayozuka tunapofikiria wajibu wetu wa kumhofu Mungu?
2 Kwa upande mwingine, hofu yaweza kuwa na matokeo mazuri. Katika Maandiko, watumishi wa Mungu wanahimizwa tena na tena wamhofu Yehova. Musa aliwaambia Waisraeli hivi: “Mche [“mhofu,” NW] BWANA, Mungu wako; ndiye utakayemtumikia.” (Kumbukumbu la Torati 6:13) Karne kadhaa baadaye, Solomoni aliandika hivi: “Mche [“mhofu,” NW] Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu.” (Mhubiri 12:13) Kupitia kazi yetu ya kuhubiri inayofanywa chini ya mwongozo wa malaika, sisi pia tunawahimiza watu ‘wamhofu Mungu na kumpa yeye utukufu.’ (Ufunuo 14:6, 7) Mbali na kumhofu Yehova, Wakristo wanapaswa kumpenda kwa moyo wao wote. (Mathayo 22:37, 38) Tunawezaje kumpenda Mungu na wakati uleule tumhofu? Kwa nini ni muhimu kumhofu Mungu mwenye upendo? Tunapata manufaa gani kwa kusitawisha hofu ya kimungu? Ili kujibu maswali hayo, kwanza twapaswa kujua maana ya kumhofu Mungu na jinsi hofu hiyo ilivyo muhimu katika uhusiano wetu na Yehova.
Kicho, Staha Kubwa, na Hofu
3. Kumhofu Mungu kunamaanisha nini?
3 Wakristo wanapaswa kumhofu Mungu kwa kuwa yeye ndiye Muumba wao. Ufafanuzi mmoja wa hofu hiyo ni “kicho na staha kubwa sana kwa Muumba na hofu inayofaa ya kutompendeza.” Hivyo, kumhofu Mungu huathiri maisha yetu katika njia mbili: mtazamo wetu kumwelekea Mungu na mtazamo wetu kuelekea mwenendo anaochukia. Bila shaka, njia hizo mbili ni muhimu na zahitaji kufikiriwa kwa makini. Kichapo Expository Dictionary of New Testament Words cha Vine chasema kwamba hofu hii yenye staha ‘ndiyo huwaongoza Wakristo maishani katika mambo ya kiroho na ya kiadili.’
4. Tunaweza kusitawisha kicho na staha kubwa kwa Muumba wetu jinsi gani?
4 Tunaweza kusitawisha kicho na staha kubwa kwa Muumba wetu jinsi gani? Sisi huhisi kicho na mshangao tunapoona mandhari yenye kupendeza, maporomoko ya maji yenye kuvutia, au machweo yanayovutia sana. Kicho hicho huongezeka tunapotambua kwa macho ya imani, kwamba Mungu ndiye aliyeumba vitu hivyo. Isitoshe, kama Mfalme Daudi, tunatambua jinsi tulivyo wadogo mno tunapojilinganisha na uumbaji wa ajabu wa Yehova. “Nikiziangalia mbingu zako, kazi ya vidole vyako, mwezi na nyota ulizoziratibisha; mtu ni kitu gani hata umkumbuke?” (Zaburi 8:3, 4) Kicho hicho kikubwa hufanya tuwe na staha kubwa, ambayo hutuchochea kumshukuru na kumsifu Yehova kwa mambo yote anayotufanyia. Pia Daudi aliandika hivi: “Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, na nafsi yangu yajua sana.”—Zaburi 139:14.
5. Kwa nini tumhofu Yehova, na tuna mfano gani mzuri kuhusiana na kumhofu?
5 Kicho na staha kubwa hutokeza hofu inayofaa na yenye heshima kwa nguvu za Mungu ambaye ni Muumba na kwa mamlaka yake akiwa Mtawala halali wa ulimwengu wote mzima. Katika maono ambayo mtume Yohana aliona, “wale watokeao wakiwa washindi kutoka kwa hayawani-mwitu na kutoka kwa sanamu yake” yaani, wafuasi watiwa-mafuta wa Kristo wakiwa mbinguni—hutangaza hivi: “Ni kubwa na za ajabu sana kazi zako, Yehova Mungu, Mweza-Yote. Ni za uadilifu na za kweli njia zako, Mfalme wa umilele. Ni nani ambaye kwa kweli hatakuhofu wewe, Yehova, na kulitukuza jina lako?” (Ufunuo 15:2-4) Kumhofu Mungu, ambako hutokana na staha kubwa kwa ajili ya utukufu wake, huchochea watawala hao wenzi wa Kristo katika Ufalme wa mbinguni wamheshimu Mungu kuwa mwenye mamlaka kuu zaidi. Tunapofikiria mambo yote ambayo Yehova ametimiza na jinsi anavyotawala ulimwengu wote mzima kwa uadilifu, je, hatuna sababu ya kutosha kumhofu?—Zaburi 2:11; Yeremia 10:7.
6. Kwa nini tuwe na hofu inayofaa ya kutompendeza Yehova?
6 Mbali na kicho na staha kubwa, kumhofu Mungu kwapaswa kutia ndani hofu inayofaa ya kutompendeza au kutomtii. Kwa nini? Kwa sababu ingawa Yehova “si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa fadhili,” twapaswa kukumbuka kwamba ‘hataacha kumwadhibu mwenye hatia.’ (Kutoka 34:6, 7, Biblia Habari Njema) Ingawa ni mwenye upendo na rehema, Yehova haachilii ukosefu wa uadilifu na makosa ya kukusudia. (Zaburi 5:4, 5; Habakuki 1:13) Wale wanaompinga Yehova na wanaozoea kufanya maovu machoni pake kwa kukusudia na bila kutubu, wataadhibiwa. Kama mtume Paulo alivyosema, “ni jambo lenye kuhofisha kuanguka katika mikono ya Mungu aliye hai.” Kuwa na hofu hiyo inayofaa ya kuanguka mikononi mwake ni ulinzi kwetu.—Waebrania 10:31.
‘Shikamaneni Naye’
7. Tuna sababu gani za kutumaini nguvu za Yehova za kuokoa?
7 Hofu yenye staha kwa Mungu na kutambua kabisa mamlaka yake ya kustaajabisha ni mambo ya msingi yanayofanya tuwe na tumaini na uhakika katika Yehova. Kama vile mtoto huhisi akiwa salama anapokuwa karibu na babake, ndivyo tunavyohisi tukiwa salama na tukiwa na uhakika chini ya uongozi wa Yehova. Ona jinsi Waisraeli walivyotenda baada ya Yehova kuwatoa Misri: “Israeli akaiona ile kazi kubwa aliyoifanya BWANA juu ya Wamisri, ndipo hao watu wakamcha [“wakamhofu,” NW] BWANA, wakamwamini BWANA.” (Kutoka 14:31) Pia jambo aliloona Elisha lathibitisha kwamba “malaika wa BWANA hufanya kituo, akiwazungukia wamchao [“wanaomhofu,” NW] na kuwaokoa.” (Zaburi 34:7; 2 Wafalme 6:15-17) Historia ya kisasa ya watu wa Yehova na labda mambo ambayo yametupata yanathibitisha kwamba Mungu hudhihirisha nguvu zake kwa niaba ya wale wanaomtumikia. (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Kwa hiyo tunafahamu kwamba “kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA ni tumaini imara.”—Mithali 14:26.
8. (a) Kwa nini kumhofu Mungu hutuchochea kutembea katika njia zake? (b) Eleza jinsi tunavyopaswa “kushikamana” na Yehova.
8 Hofu inayofaa ya kimungu hutokeza tumaini na uhakika katika yeye na pia hutuchochea kutembea katika njia zake. Solomoni alipozindua hekalu, alisali hivi kwa Yehova: “Ili [Israeli] wakuche [“wakuhofu,” NW] wewe, waziendee njia zako, siku zote watakazoishi katika nchi uliyowapa baba zetu.” (2 Mambo ya Nyakati 6:31) Hapo awali, Musa aliwahimiza Waisraeli hivi: “Tembeeni kwa kumfuata BWANA, Mungu wenu; mcheni [“mhofuni,” NW] na kushika maagizo yake na kuisikia sauti yake, nanyi mtumikieni na kushikamana naye.” (Kumbukumbu la Torati 13:4) Kama inavyoonyeshwa waziwazi na mistari hiyo, tamaa ya kutembea katika njia za Yehova na “kushikamana” naye hutokana na kuwa na tumaini na uhakika katika Mungu. Naam, hofu ya kimungu hutuchochea kumtii Yehova, kumtumikia, na kushikamana naye, kama vile mtoto hushikamana kihalisi na baba yake na kumtumaini na kuwa na uhakika naye kabisa.—Zaburi 63:8; Isaya 41:13.
Kumpenda Mungu Ni Kumhofu
9. Kuna uhusiano gani kati ya kumpenda Mungu na kumhofu Mungu?
9 Kulingana na Maandiko, kumhofu Mungu hakumaanishi kwa vyovyote kwamba haiwezekani kumpenda. Kinyume cha hilo, Waisraeli waliagizwa ‘wamhofu Yehova ili kwenda katika njia zake zote, na kumpenda.’ (Kumbukumbu la Torati 10:12) Kwa hiyo, kumhofu Mungu na kumpenda Mungu ni mambo yanayohusiana kwa ukaribu. Kumhofu Mungu hutuchochea kutembea katika njia zake, na jambo hilo huthibitisha kwamba tunampenda. (1 Yohana 5:3) Jambo hilo linapatana na akili kwa kuwa tunapompenda mtu, kwa kufaa tunahofu kumhuzunisha. Waisraeli walimhuzunisha Yehova walipoasi huko nyikani. Bila shaka, hatungependa kufanya jambo lolote linaloweza kumhuzunisha Baba yetu wa kimbingu. (Zaburi 78:40, 41) Kwa upande mwingine, kwa kuwa “BWANA huwaridhia wao wamchao [“wanaomhofu,” NW],” tunapomtii na kuwa waaminifu kwake, tunafurahisha moyo wake. (Zaburi 147:11; Mithali 27:11) Kumpenda Mungu hutuchochea tumfurahishe, na kumhofu Mungu hutuzuia tusimhuzunishe. Hizo ni sifa zinazoambatana.
10. Yesu alionyeshaje kwamba alifurahia kumhofu Yehova?
10 Maisha ya Yesu Kristo yanaonyesha waziwazi jinsi tunavyoweza kumpenda na kumhofu Mungu wakati uleule. Nabii Isaya aliandika hivi kuhusu Yesu: ‘Roho ya BWANA itakaa juu yake, roho ya hekima na ufahamu, roho ya shauri na uweza, roho ya maarifa na ya kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA; na furaha yake itakuwa katika kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA.’ (Isaya 11:2, 3) Kulingana na unabii huo, roho ya Mungu ilimchochea Yesu kumhofu Baba yake wa kimbingu. Isitoshe, tunaona kwamba hofu hiyo badala ya kuwa mzigo, ilitokeza uradhi. Yesu alifurahia kufanya mapenzi ya Mungu na kumpendeza, hata chini ya hali ngumu kabisa. Alipokaribia kuuawa kwenye mti wa mateso, alimwambia Yehova hivi: “Si kama mimi nipendavyo, bali kama wewe upendavyo.” (Mathayo 26:39) Kwa sababu ya hofu hiyo ya kimungu, Yehova alijibu sala za Mwana wake, akamwimarisha, na kumwokoa na kifo.—Waebrania 5:7.
Kujifunza Kumhofu Yehova
11, 12. (a) Kwa nini tujifunze kumhofu Mungu? (b) Yesu hutufundishaje kumhofu Yehova?
11 Tofauti na kicho tunachohisi tunapoona uwezo na fahari ya uumbaji, ni lazima tujitahidi kusitawisha hofu ya Mungu. Ndiyo sababu Daudi Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo, anatoa mwaliko huu wa kiunabii: “Njoni, enyi wana, mnisikilize, nami nitawafundisha kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA.” (Zaburi 34:11) Yesu hutufundishaje kumhofu Yehova?
12 Yesu hutufundisha kumhofu Yehova kwa kutusaidia tuelewe utu mzuri wa Baba yetu wa kimbingu. (Yohana 1:18) Mfano wa Yesu unaonyesha jinsi Mungu anavyofikiri na jinsi anavyoshughulika na wengine, kwa kuwa Yesu anadhihirisha utu wa Baba yake kikamili. (Yohana 14:9, 10) Isitoshe, kupitia dhabihu ya Yesu, tunaweza kumfikia Yehova tunaposali tusamehewe dhambi zetu. Rehema hizo nyingi za Mungu zapaswa kutuchochea vya kutosha tumhofu. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Lakini kwako kuna msamaha, ili wewe uogopwe [“uhofiwe,” NW].”—Zaburi 130:4.
13. Ni hatua gani zinazoonyeshwa katika kitabu cha Mithali ambazo hutusaidia kumhofu Yehova?
13 Kitabu cha Mithali kinaonyesha mfululizo wa hatua ambazo hutuwezesha kusitawisha hofu ya kimungu. “Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, na kuyaweka akiba maagizo yangu; hata ukatega sikio lako kusikia hekima, ukauelekeza moyo wako upate kufahamu; naam, ukiita busara, na kupaza sauti yako upate ufahamu, . . . ndipo utakapofahamu kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA, na kupata kumjua Mungu.” (Mithali 2:1-5) Kwa hiyo, ili kumhofu Mungu, lazima tujifunze Neno lake, tujitahidi kuelewa maagizo yake, na kusikiliza shauri lake kwa makini.
14. Tunawezaje kuiga shauri lililotolewa kwa wafalme wa Israeli?
14 Kila mfalme wa Israeli la kale aliagizwa afanye nakala ya Sheria na “asome humo sikuzote atakazoishi; ili apate kujifunza kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA, Mungu wake, ayashike maneno yote ya torati hii.” (Kumbukumbu la Torati 17:18, 19) Ili kujifunza kumhofu Yehova, ni muhimu tusome na kujifunza Biblia. Tunapotumia kanuni za Biblia maishani mwetu, hatua kwa hatua tunajipatia hekima na ujuzi wa kimungu. Tunapata ‘kufahamu kumhofu Yehova’ kwa kuona jinsi kufanya hivyo kunavyoboresha maisha yetu, na kuthamini uhusiano wetu pamoja na Mungu. Isitoshe, kwa kukutanika kwa ukawaida na waabudu wenzetu, sote—wachanga kwa wakubwa—tunaweza kusikiliza mafundisho ya Mungu, kujifunza kumhofu Mungu, na kutembea katika njia zake.—Kumbukumbu la Torati 31:12.
Mwenye Furaha Ni Mtu Anayemhofu Yehova
15. Kumhofu Mungu kunahusiana na ibada yetu katika njia gani?
15 Kutokana na mambo yaliyotangulia kutajwa, tunaweza kuona kwamba kumhofu Mungu ni mtazamo unaofaa ambao sote twahitaji kusitawisha, kwa kuwa huo ni sehemu muhimu ya ibada yetu kwa Yehova. Hutuongoza tumtumaini kabisa, tutembee katika njia zake, na kushikamana naye. Kama vile Yesu Kristo, kumhofu Mungu kwaweza kutuchochea pia tutimize nadhiri yetu ya wakfu sasa na kwa umilele.
16. Kwa nini Yehova anatutia moyo tumhofu?
16 Hofu ya kimungu si hofu isiyofaa wala haina vizuizi visivyo vya lazima. “Heri kila mtu amchaye [“amhofuye,” NW] BWANA, aendaye katika njia yake,” yatuhakikishia Biblia. (Zaburi 128:1) Yehova hututia moyo tumhofu kwa sababu anajua kwamba sifa hiyo itatulinda. Twaona hangaiko lake lenye upendo katika maneno haya aliyoambia Musa: “Laiti wangekuwa na moyo kama huu ndani yao sikuzote, wa kunicha [“kunihofu,” NW], na kushika amri zangu zote sikuzote, wapate kufanikiwa wao na watoto wao milele!”—Kumbukumbu la Torati 5:29.
17. (a) Tunapata manufaa gani kwa kumhofu Mungu? (b) Ni mambo gani yanayohusu hofu ya kimungu yatakayozungumziwa katika makala inayofuata?
17 Vivyo hivyo, tukisitawisha moyo wa kumhofu Mungu, tutafanikiwa. Katika njia gani? Kwanza kabisa, mtazamo huo utampendeza Mungu na utatuvuta karibu naye. Kutokana na mambo yaliyompata, Daudi alijua kwamba “atawafanyia wamchao [“wanaomhofu,” NW] matakwa yao, naye atasikia kilio chao na kuwaokoa.” (Zaburi 145:19) Pili, hofu ya kimungu itatunufaisha kwa sababu itabadili mtazamo wetu kuelekea lililo ovu. (Mithali 3:7) Makala inayofuata itaonyesha jinsi hofu hii inavyotulinda kutokana na hatari za kiroho, nayo itaonyesha mifano ya watu fulani katika Maandiko ambao walimhofu Mungu na kuepuka kutenda maovu.
[Maelezo ya Chini]
a Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilipitisha Azimio la Haki za Binadamu, Desemba 10, 1948.
Je, Unaweza Kujibu Maswali Yafuatayo?
• Kumhofu Mungu kunamaanisha nini, na hofu hiyo inakuwa na matokeo gani juu yetu?
• Kuna uhusiano gani kati ya kumhofu Mungu na kutembea pamoja na Mungu?
• Mfano wa Yesu unaonyeshaje kwamba kumhofu Mungu kunahusiana na kumpenda Mungu?
• Ni katika njia gani tunaweza kusitawisha moyo wa kumhofu Yehova?
[Picha katika ukurasa wa 17]
Wafalme wa Israeli waliagizwa wafanye nakala ya Sheria na kuisoma kila siku
[Picha katika ukurasa wa 18]
Kumhofu Yehova hufanya tumtumaini kama vile mtoto humtumaini babake
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 15]
Nyota: Photo by Malin, © IAC/RGO 1991