Tumeandaliwa Kikamili Kuwa Walimu wa Neno la Mungu
“Mungu . . . ametustahilisha vya kutosha kuwa wahudumu.”—2 WAKORINTHO 3:5, 6.
1, 2. Ni jitihada gani za kuhubiri ambazo hufanywa mara nyingine, lakini ni kwa nini kwa kawaida jitihada hizo hazifaulu?
UNGEHISIJE kama ungepewa kazi ambayo huna sifa za kustahili kuifanya? Hebu fikiria: Umepewa vifaa vyote unavyohitaji. Lakini huna ujuzi hata kidogo wa kufanya kazi hiyo. Isitoshe, kazi hiyo inatakiwa ifanywe haraka. Watu wanakutegemea. Inavunja moyo kama nini!
2 Lakini hali hiyo ngumu si ya kuwaziwa tu. Fikiria mfano mmoja. Mara kwa mara, kanisa fulani la Jumuiya ya Wakristo limejaribu kupanga na kufanya huduma ya nyumba hadi nyumba. Kwa kawaida jitihada hizo hazifaulu na hufifia kabisa baada ya muda wa majuma au miezi kadhaa. Kwa nini? Jumuiya ya Wakristo haijawasaidia wafuasi wake kuwa na sifa za kuwastahilisha kufanya kazi hiyo. Hata makasisi wenyewe hawana sifa za kuwastahilisha kuhubiri, licha ya kujifunza kwa miaka mingi kwenye shule za ulimwengu na vyuo vya mafunzo ya kidini. Kwa nini tuseme hivyo?
3. Ni semi gani ambazo zimetumiwa mara tatu katika 2 Wakorintho 3:5, 6, nazo zinamaanisha nini?
3 Neno la Mungu huonyesha sifa ambazo humstahilisha mtu kuwa mhubiri wa kweli wa habari njema za Kikristo. Mtume Paulo alipuliziwa kuandika: “Si kwamba sisi wenyewe tuna sifa za ustahili wa kutosha kuhesabu jambo lolote kuwa latoka kwetu wenyewe, bali kuwa kwetu na sifa za ustahili wa kutosha kwatoka kwa Mungu, ambaye kwa kweli ametustahilisha vya kutosha kuwa wahudumu.” (2 Wakorintho 3:5, 6) Ona semi zenye kutia moyo ambazo zimetumiwa mara tatu kwenye andiko hilo— ‘sifa za ustahili wa kutosha.’ Semi hizo zinamaanisha nini? Kamusi iitwayo Vine’s Expository Dictionary of Biblical Words yasema: “[Neno la awali la Kigiriki] linapotumiwa kurejezea vitu linamaanisha ‘-tosha’ . . . ; linapotumiwa kurejezea watu, linamaanisha ‘hodari,’ ‘-enye kustahili.’” Hivyo, mtu aliye na ‘sifa za ustahili wa kutosha’ ni hodari naye anastahili kufanya kazi anayopewa. Naam, wahudumu wa kweli wa habari njema wana sifa zinazowastahilisha kufanya kazi hiyo. Wao ni hodari, wanafaa, au wanastahili kuhubiri.
4. (a) Mfano wa Paulo unaonyeshaje kwamba si watu wachache tu maarufu walio na sifa za kustahili kufanya huduma ya Kikristo? (b) Yehova hutumia njia gani tatu kutustahilisha kuwa wahudumu?
4 Lakini sifa hizo za ustahili hutoka wapi? Je, hutokana na uwezo wa mtu binafsi? Je, hutokana na akili nyingi? Je, hutokana na elimu ya kipekee ya shule fulani maarufu? Yaonekana mtume Paulo alikuwa na vitu hivyo vyote. (Matendo 22:3; Wafilipi 3:4, 5) Hata hivyo, alikiri kwa unyenyekevu kwamba sifa zilizomstahilisha kuwa mhudumu zilitoka kwa Yehova Mungu wala si katika shule fulani za elimu ya juu. Je, ni watu wachache tu mashuhuri walio na sifa hizo? Paulo alipuliziwa kuandikia kutaniko la Korintho juu ya “kuwa kwetu na sifa za ustahili wa kutosha.” Jambo hilo linadokeza kwamba Yehova huhakikisha kwamba watumishi wake wote waaminifu wana sifa za ustahili na wanaweza kufanya kazi aliyowapa. Yehova huwasaidiaje Wakristo wa kweli wawe na sifa za ustahili leo? Na tuzungumzie njia tatu anazotumia: (1) Neno lake, (2) roho yake takatifu, na (3) tengenezo lake la kidunia.
Neno la Yehova Hutustahilisha
5, 6. Maandiko Matakatifu huwa na matokeo gani kwa Wakristo wa kweli?
5 Kwanza, Neno la Mungu hutusaidiaje tustahili kuwa wahudumu? Paulo aliandika: “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu apate kuwa hodari, aliyeandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Timotheo 3:16, 17) Kwa hiyo, Maandiko Matakatifu hutusaidia ‘kuwa watu hodari, walioandaliwa vifaa kikamili’ ili kutimiza “kazi njema” ya kufundisha watu Neno la Mungu. Namna gani wafuasi wote wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo? Wana Biblia. Kitabu hicho kinawezaje kusaidia watu fulani wawe wahudumu hodari na kikose kuwasaidia wengine? Hilo lategemea mtazamo wetu kuelekea Biblia.
6 Inasikitisha kwamba watu wengi ambao huenda makanisani hawaukubali ujumbe wa Biblia ‘kama ulivyo kwa kweli, kama neno la Mungu.’ (1 Wathesalonike 2:13) Jumuiya ya Wakristo imekuwa na sifa mbaya kuhusiana na jambo hilo. Baada ya kujifunza kwa miaka mingi katika vyuo vya mafunzo ya kidini, je, makasisi wameandaliwa kikamili kuwa walimu wa Neno la Mungu? La. Kwani, wanafunzi fulani huanza masomo yao ya kidini wakiwa na imani katika Biblia lakini huhitimu wakiwa wenye kuitilia shaka! Kwa hiyo, badala ya kulihubiri Neno la Mungu, ambalo wengi wao hawaliamini tena, wao huzingatia mambo mengine. Wao huunga mkono pande mbalimbali katika majadiliano ya kisiasa na kuendeleza ile iitwayo injili ya kijamii, au kukazia falsafa za ulimwengu huu katika mahubiri yao. (2 Timotheo 4:3) Tofauti nao, Wakristo wa kweli hufuata kielelezo cha Yesu Kristo.
7, 8. Maoni ya Yesu kuhusu Neno la Mungu yalitofautianaje na ya viongozi wa kidini wa siku zake?
7 Yesu hakuwaruhusu viongozi wa kidini wa siku zake wabadili maoni yake. Yesu alitumia maandiko matakatifu ifaavyo, iwe alikuwa akifundisha kikundi kidogo, kama vile mitume wake, au umati mkubwa. (Mathayo 13:10-17; 15:1-11) Kufanya hivyo kulimtofautisha na viongozi wa kidini wa wakati huo. Viongozi hao waliwavunja moyo kabisa watu wa kawaida wasiyachunguze mambo yenye kina ya Mungu. Lilikuwa jambo la kawaida kwa mwalimu wa Neno la Mungu wa wakati huo kuamini kwamba maandiko fulani katika Biblia yalikuwa na mambo mazito sana hivi kwamba hangeweza kuyazungumzia na wengine ila tu mwanafunzi wake wa karibu zaidi. Tena, angezungumza naye kwa sauti ya chini huku amefunika kichwa. Ushirikina wa hao viongozi wa kidini uliwazuia kuzungumzia maandiko fulani ya Biblia na hata kulitamka jina la Mungu!
8 Kristo hakuwa hivyo. Aliamini kwamba watu wote, na si watu wachache tu waliochaguliwa, walihitaji kuzingatia “kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.” Yesu hakutaka kuwapa tu wasomi fulani mashuhuri pendeleo la kuwajulisha watu Maandiko. Aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Lile niwaambialo nyinyi katika giza, lisemeni katika nuru; na lile msikialo lanong’onwa, lihubirini kutoka paa za nyumba.” (Mathayo 4:4; 10:27) Yesu alitaka sana kuwafundisha watu wengi iwezekanavyo kuhusu Mungu.
9. Wakristo wa kweli huitumiaje Biblia?
9 Twapaswa kukazia hasa Neno la Mungu tunapofundisha. Kwa mfano, tunapotoa hotuba kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova, haitoshi kusoma tu mistari fulani iliyoteuliwa katika Biblia. Huenda tukahitaji kueleza, kutoa mfano, na kuonyesha jinsi andiko tunalosoma linavyoweza kutumika. Lengo letu linapasa kuwa kutumia ujumbe wa Biblia kufikia mioyo ya wasikilizaji wetu. (Nehemia 8:8, 12) Inapohitajika kutoa ushauri au nidhamu, Biblia inapaswa kutumiwa. Ingawa watu wa Yehova huzungumza lugha mbalimbali na ni wa malezi mbalimbali, wote wanaheshimu Biblia—kitabu kisicho na kifani.
10. Ujumbe wa Biblia uliopuliziwa unaweza kuwa na matokeo gani juu yetu?
10 Ujumbe wa Biblia una nguvu unapotumiwa kwa heshima jinsi hiyo. (Waebrania 4:12) Huchochea watu kufanya mabadiliko katika maisha yao na kuacha mazoea yasiyo ya Kimaandiko kama vile uasherati, uzinzi, ibada ya sanamu, ulevi, na wizi. Imesaidia wengi wavue utu wa zamani na kuvaa utu mpya. (Waefeso 4:20-24) Naam, iwapo tunaiheshimu Biblia kuliko maoni yoyote ya kibinadamu na tunaitumia kwa uaminifu, inaweza kwa kweli kutusaidia tuwe watu hodari walioandaliwa kikamili kuwa walimu wa Neno la Mungu.
Roho ya Yehova Hutustahilisha
11. Kwa nini inafaa kuiita roho takatifu ya Yehova “msaidiaji”?
11 Pili, na tuzungumzie jinsi ambavyo roho takatifu, au nguvu ya utendaji ya Yehova, hutuandaa kikamili. Haitupasi kamwe kusahau kwamba roho ya Yehova ndiyo nguvu kuu kupita zote. Yehova amemwezesha Mwanawe mpendwa atumie nguvu hiyo kuu kwa niaba ya Wakristo wote wa kweli. Basi, kwa kufaa Yesu aliiita roho takatifu “msaidiaji.” (Yohana 16:7) Aliwasihi wafuasi wake wamwombe Yehova roho hiyo na kuwahakikishia kwamba Yehova angewapa kwa wingi.—Luka 11:10-13; Yakobo 1:17.
12, 13. (a) Kwa nini ni muhimu kuomba roho takatifu itusaidie katika huduma yetu? (b) Mafarisayo walionyeshaje kwamba roho takatifu haikuwa inafanya kazi ndani yao?
12 Tunahitaji kusali kila siku ili tupate roho takatifu, hasa itusaidie katika huduma. Nguvu hiyo ya utendaji inaweza kuwa na matokeo gani juu yetu? Inaweza kutenda kazi katika akili na mioyo yetu na kutusaidia kufanya mabadiliko, kukua kiroho, na kuvua utu wa kale na kuvaa utu mpya. (Wakolosai 3:9, 10) Inaweza kutusaidia tusitawishe sifa zenye thamani kama za Kristo. Wengi wetu tunaweza kukariri andiko la Wagalatia 5:22, 23. Mistari hiyo inaorodhesha matunda ya roho ya Mungu. Tunda la kwanza ni upendo. Sifa hiyo ni muhimu katika huduma yetu. Kwa nini?
13 Upendo huchochea sana. Wakristo wa kweli huchochewa na upendo kwa Yehova na kwa wanadamu wenzao kuhubiri habari njema. (Marko 12:28-31) Bila upendo huo, hatuwezi kustahili kikweli kuwa walimu wa Neno la Mungu. Ona tofauti kati ya Yesu na Mafarisayo. Andiko la Mathayo 9:36 lasema hivi kuhusu Yesu: “Alipouona umati alihisi sikitiko kwa ajili yao, kwa sababu ulikuwa umechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” Mafarisayo waliwaonaje watu wa kawaida? Walisema: “Umati huu usiojua Sheria ni watu waliolaaniwa.” (Yohana 7:49) Mafarisayo hao hawakuwapenda watu bali waliwadharau sana. Ni wazi kwamba roho ya Yehova haikuwa inatenda kazi ndani yao.
14. Kielelezo cha Yesu cha kuonyesha upendo katika huduma yake chapasa kutuchocheaje?
14 Yesu aliwahurumia watu. Alijua jinsi walivyoteseka. Alijua kwamba walikuwa wametendewa vibaya, wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji. Andiko la Yohana 2:25 linatuambia kwamba Yesu “alijua kile kilichokuwa katika binadamu.” Yesu anaelewa vizuri sana hali halisi ya wanadamu kwa kuwa alikuwa Stadi wa Kazi wa Yehova wakati wa uumbaji. (Mithali 8:30, 31) Uelewevu huo unafanya awapende zaidi. Upendo huo na utuchochee sikuzote kufanya kazi yetu ya kuhubiri! Iwapo tunahisi kwamba tunahitaji kufanya maendeleo kuhusiana na kazi hiyo, na tusali ili tupate roho takatifu ya Yehova, kisha tutende kupatana na sala zetu. Yehova atatujibu kwa kutuma nguvu hiyo isiyoweza kuzuiliwa itusaidie kumwiga Kristo hata zaidi, ambaye ndiye aliyekuwa na sifa za juu zaidi za ustahili wa kuhubiri habari njema.
15. Maneno ya Isaya 61:1-3 yalimhusuje Yesu na wakati huohuo kuwafichua waandishi na Mafarisayo?
15 Yesu alipata wapi sifa za ustahili? “Roho ya Yehova iko juu yangu,” akasema. (Luka 4:17-21) Naam, Yehova mwenyewe alimweka Yesu rasmi kupitia roho takatifu. Yesu hakuhitaji hati za ziada za utambulisho. Je viongozi wa kidini wa wakati wake walikuwa wamewekwa rasmi na roho takatifu? La. Wala hawakuwa wameandaliwa kikamili kutimiza unabii wa Isaya 61:1-3, ambao Yesu alisoma kwa sauti kubwa na kusema ulimhusu. Tafadhali soma mistari hiyo na utajionea kwamba waandishi na Mafarisayo wanafiki hawakutimiza maneno hayo. Hawakuwa na habari njema za kuwatangazia maskini. Nao wangewezaje kuhubiri kuachiliwa kwa mateka na kuhubiri kupata kuona tena kwa vipofu? Katika maana ya kiroho, wao wenyewe walikuwa vipofu na watumwa wa mapokeo ya wanadamu! Tofauti na watu hao, je tuna sifa zinazotustahilisha kufundisha watu?
16. Watu wa Yehova wanaweza kuwa na uhakika gani leo kuhusiana na kustahili kwao kuwa wahudumu?
16 Ni kweli kwamba hatukujifunza kwenye vyuo vya kidini vya Jumuiya ya Wakristo. Vyuo hivyo havituweki rasmi kuwa walimu. Basi je, tunakosa sifa za ustahili? La! Sisi huwekwa rasmi na Yehova kuwa Mashahidi wake. (Isaya 43:10-12) Tukisali kupata roho yake na kutenda kupatana na sala yetu, tutakuwa na sifa za ustahili za juu zaidi. Kwa uhakika, sisi si wakamilifu na hushindwa kufuata kikamili kielelezo kilichowekwa na Mwalimu Mkuu, Yesu. Hata hivyo, je, hatushukuru kwamba Yehova hutumia roho yake kutustahilisha na kutuandaa kuwa walimu wa Neno lake?
Tengenezo la Yehova Hutustahilisha
17-19. Mikutano mitano ambayo imeandaliwa na tengenezo la Yehova hutusaidiaje tustahili kuwa wahudumu?
17 Sasa na tuzungumzie njia ya tatu ambayo Yehova hutumia kutuandaa kikamili kuwa walimu wa Neno lake. Njia hiyo ni kutaniko, au tengenezo lake la kidunia ambalo hutuzoeza kuwa wahudumu. Jinsi gani? Fikiria programu za mafundisho tulizo nazo! Sisi huhudhuria mikutano mitano ya Kikristo kila juma. (Waebrania 10:24, 25) Tunakusanyika katika vikundi vidogo kwenye Funzo la Kitabu la Kutaniko ili kufurahia funzo lenye kina la Biblia kupitia kitabu kilichoandaliwa na tengenezo la Yehova. Kwa kusikiliza na kutoa maelezo, sisi hujifunza na kutiana moyo. Pia mwangalizi wa funzo la kitabu humpa kila mmoja wetu maagizo na uangalifu wa kibinafsi. Kwenye Mkutano wa Watu Wote na Funzo la Mnara wa Mlinzi, sisi hupata chakula kingi cha kiroho chenye kujenga.
18 Shule yetu ya Huduma ya Kitheokrasi imekusudiwa kutuzoeza jinsi ya kufundisha. Kwa kutayarisha hotuba za wanafunzi, sisi hujifunza jinsi ya kutumia Neno la Mungu kufundisha mambo mbalimbali. (1 Petro 3:15) Je, umewahi kupewa mgawo wa kutoa hotuba ambayo uliona kana kwamba unaifahamu sana ila tu kugundua kwamba kuna jambo fulani jipya unaloweza kujifunza kutokana na hotuba hiyo? Hilo ni jambo la kawaida. Kufunza wengine habari fulani hutusaidia kuijua hata zaidi. Hata ikiwa hatuna mgawo katika Shule, bado tunaweza kujifunza kuwa walimu bora. Kila mwanafunzi ana sifa nzuri, nasi tunaweza kufikiria jinsi tunavyoweza kuiga sifa hizo.
19 Mkutano wa Utumishi pia unakusudiwa kutuandaa kuwa walimu wa Neno la Mungu. Juma baada ya juma sisi hufurahia hotuba zenye kusisimua, mazungumzo, na maonyesho yanayokusudiwa kutusaidia katika huduma yetu. Tutatumia utangulizi gani? Tunaweza kushughulikiaje magumu ya pekee katika huduma yetu ya hadharani? Ni njia zipi tunazoweza kutumia katika mahubiri ambazo huenda tukahitaji kuzichunguza zaidi? Ni nini kitakachotusaidia tuwe walimu wenye matokeo zaidi tunapofanya ziara za kurudia na kuongoza mafunzo ya Biblia? (1 Wakorintho 9:19-22) Maswali hayo hushughulikiwa na kuzungumziwa kwa undani zaidi kwenye Mkutano wa Utumishi. Sehemu nyingi za mkutano huo hutoka katika makala za Huduma Yetu ya Ufalme, ambacho ni kifaa kingine kilichoandaliwa kwa ajili ya kazi yetu muhimu.
20. Tunawezaje kunufaika kikamili kutokana mikutano na makusanyiko?
20 Tunapata mazoezi mengi kwa kujitayarisha kwa ajili ya mikutano, kuihudhuria, kisha kutumia yale ambayo tumejifunza katika kazi yetu tukiwa walimu. Lakini tunaweza pia kupata mazoezi zaidi kwenye mikutano mikubwa zaidi kama makusanyiko yanayokusudiwa kutuandaa kuwa walimu wa Neno la Mungu. Tunatazamia kwa hamu kama nini kusikiliza kwa makini na kutumia ushauri tunaopata!—Luka 8:18.
21. Ni uthibitisho gani unaoonyesha kwamba mazoezi tunayopata yamekuwa na matokeo, na sifa zinamwendea nani?
21 Je, mazoezi ambayo Yehova ametoa yamekuwa na matokeo? Na tuchunguze hali ilivyo kwa kweli. Kila mwaka, mamia kwa maelfu ya watu wanasaidiwa kujua mafundisho ya msingi ya Biblia na kuishi kulingana na vile Mungu atakavyo. Tunazidi kuongezeka, lakini hakuna hata mmoja wetu anayeweza kujisifu kwa ajili ya ongezeko hilo. Lazima tuone mambo kihalisi, kama Yesu alivyoyaona. Alisema: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute yeye.” Kama mitume walioishi zamani, wengi wetu tu watu wa kawaida na hatujasoma sana. (Yohana 6:44; Matendo 4:13) Tunafanikiwa kwa sababu tunamtegemea Yehova, ambaye huwavuta watu wenye mioyo minyofu kwenye ile kweli. Paulo alieleza jambo hilo vizuri: “Mimi nilipanda, Apolo akatia maji, lakini Mungu akafuliza kuikuza.”—1 Wakorintho 3:6.
22. Kwa nini hatupaswi kamwe kuvunjika moyo kupita kiasi kuhusu kushiriki kikamili katika huduma ya Kikristo?
22 Naam, Yehova Mungu anahusika sana katika kazi yetu tukiwa walimu wa Neno lake. Huenda sikuzote tusihisi kwamba tuna sifa zinazotustahilisha kuwa walimu. Lakini kumbuka kwamba Yehova ndiye huvuta watu kwake na kwa Mwanawe. Kupitia Neno lake, roho yake takatifu, na tengenezo lake la kidunia, Yehova hutustahilisha kuwahudumia watu hao wapya. Na tukubali kuzoezwa na Yehova kwa kutumia mambo mazuri ambayo Mungu ametupatia sasa ili kutuandaa kikamili kuwa walimu wa Neno Lake!
Ungejibuje?
• Biblia hutuandaaje kwa ajili ya kazi ya kuhubiri?
• Roho takatifu hutustahilishaje kuwa wahudumu?
• Tengenezo la Yehova la kidunia limekusaidia katika njia zipi ili ustahili kuwa mhubiri wa habari njema?
• Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika tunaposhiriki katika huduma?
[Picha katika ukurasa wa 25]
Akiwa mwalimu wa Neno la Mungu, Yesu aliwapenda watu