Usijidanganye Mwenyewe kwa Mawazo Yasiyo ya Kweli
BAADA ya Hawa kula tunda la mti uliokatazwa, Mungu alimuuliza hivi: “Ni nini hili ulilofanya?” Hawa akajibu: “Yule nyoka—alinidanganya nami nikala.” (Mwa. 3:13) Shetani, yule nyoka mjanja, ambaye alimshawishi Hawa kutomtii Mungu, baadaye aliitwa “yule nyoka wa zamani, . . . anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa.”—Ufu. 12:9.
Masimulizi hayo ya kitabu cha Mwanzo yanaonyesha kwamba Shetani ni mjanja, na kwamba anatumia uwongo kwa kusudi la kuwadanganya watu wasio waangalifu. Bila shaka Hawa alipotoshwa na uwongo wake. Hata hivyo, hatupaswi kufikiri kwamba Shetani peke yake ndiye anayeweza kutupotosha. Biblia inatuonya pia kuhusu hatari ya ‘kujidanganya wenyewe kwa mawazo yasiyo ya kweli.’—Yak. 1:22.
Huenda wazo la kujidanganya wenyewe likaonekana kuwa lisiloaminika au hata lisilowezekana kamwe. Hata hivyo, bila shaka Mungu ametoa onyo hilo kwa kusudi fulani. Basi ni vyema tufikirie jinsi tunavyoweza kujidanganya wenyewe na aina ya mawazo ya uwongo ambayo yanaweza kutupotosha. Mfano mmoja wa Kimaandiko unaweza kutusaidia.
Watu Fulani Waliojidanganya Wenyewe
Karibu mwaka wa 537 K.W.K., Koreshi Mkuu wa Uajemi alitoa amri ili Wayahudi waliokuwa uhamishoni huko Babiloni warudi Yerusalemu na kulijenga upya hekalu. (Ezra 1:1, 2) Mwaka uliofuata, kupatana na kusudi la Yehova, watu hao waliweka msingi wa hekalu jipya. Wayahudi waliorudi walishangilia na kumsifu Yehova kwa sababu alibariki kazi ya kuweka msingi wa mradi huo wa maana. (Ezra 3:8, 10, 11) Lakini muda si muda, kazi ya kujenga upya hekalu ilianza kupingwa na watu wakavunjika moyo. (Ezra 4:4) Baada ya miaka 15 hivi kupita tangu waliporudi, Waajemi wenye mamlaka walipiga marufuku kazi yote ya ujenzi huko Yerusalemu. Ili kutekeleza amri hiyo ya marufuku, viongozi wa majimbo walifika Yerusalemu na ‘kuwakomesha Wayahudi kwa kutumia nguvu za silaha.’—Ezra 4:21-24.
Wayahudi walipokabili kizuizi hicho kikubwa, walijidanganya wenyewe kwa mawazo yasiyo ya kweli. Walijiambia hivi: “Wakati haujaja, wakati wa kujengwa kwa nyumba ya Yehova.” (Hag. 1:2) Walikata kauli kwamba Mungu hakutaka hekalu lijengwe wakati huo. Badala ya kutafuta njia ya kufanya mapenzi yake, waliacha mgawo wao mtakatifu na kutumia wakati na nguvu zao kurekebisha nyumba zao. Hagai, nabii wa Mungu aliwauliza hivi waziwazi: “Je, huu ni wakati wa ninyi kukaa katika nyumba zenu zilizofunikwa kwa mbao, huku nyumba hii [hekalu la Yehova] ikiwa imeharibika?”—Hag. 1:4.
Je, unajifunza jambo fulani katika mfano huo? Kuwa na maoni yasiyofaa kuhusu wakati wa kutimizwa kwa kusudi la Mungu kunaweza kutufanya tuone kwamba utendaji wetu wa kiroho si wa maana na hivyo tukengeushwe kwa kufuatia mapendezi yetu wenyewe. Kwa mfano, wazia kwamba unangojea wageni. Hamu ya kutembelewa na wageni hao inaweza kukuchochea ujitahidi kabisa kufanya kazi za maana za nyumbani kwa ajili ya ziara yao. Hata hivyo, kwa ghafula unapata habari kwamba wageni hao watachelewa. Je, utaacha kufanya matayarisho?
Hata hivyo, kumbuka kwamba Hagai na Zekaria waliwasaidia Wayahudi kuelewa kwamba bado Yehova alitaka hekalu hilo lijengwe upya bila kuchelewa. Hagai aliwahimiza hivi: “Iweni na nguvu, ninyi nyote watu wa nchi, . . . na mfanye kazi.” (Hag. 2:4) Walihitaji kuendelea na kazi hiyo, wakiwa na hakika kwamba roho ya Mungu ingewasaidia. (Zek. 4:6, 7) Je, mfano huo unaweza kutusaidia kuepuka kukata kauli isiyofaa kuhusu siku ya Yehova?—1 Kor. 10:11.
Kuacha Mawazo Yasiyo ya Kweli na Kuanza Kufikiri kwa Utimamu
Katika barua yake ya pili, mtume Petro alizungumza kuhusu programu au ratiba ya Yehova ya kuleta “mbingu mpya na dunia mpya.” (2 Pet. 3:13) Alisema kwamba wadhihaki fulani walikuwa na mashaka ikiwa Mungu angeingilia mambo ya wanadamu. Walisema kwa makosa kwamba hakuna jambo ambalo lingetokea, na kwamba “mambo yote [yalikuwa yakiendelea] sawasawa kama tangu mwanzo wa uumbaji.” (2 Pet. 3:4) Petro alitaka kupinga mawazo hayo yenye makosa. Aliandika hivi: “Ninaamsha uwezo wenu mzuri wa kufikiri kwa njia ya kikumbusho.” Aliwakumbusha Wakristo wenzake kwamba wadhihaki hao walikosea. Hapo zamani Mungu alikuwa ameingilia mambo ya wanadamu, akaleta gharika yenye msiba duniani pote.—2 Pet. 3:1, 5-7.
Katika mwaka wa 520 K.W.K., Hagai pia aliwapa himizo kama hilo Wayahudi waliovunjika moyo na wasiotenda. Aliwashauri hivi: “Wekeni moyo wenu juu ya njia zenu.” (Hag. 1:5) Ili kuamsha uwezo wao wa kufikiri, aliwakumbusha waabudu wenzake makusudi na ahadi za Mungu kuhusu watu Wake. (Hag. 1:8; 2:4, 5) Muda mfupi baada ya Wayahudi hao kutiwa moyo hivyo, kazi ya ujenzi ilianza tena, hata ingawa wenye mamlaka walikuwa wameipiga marufuku. Kwa mara nyingine tena, maadui walijaribu kusimamisha mradi huo wa ujenzi, lakini hawakufanikiwa. Amri ya marufuku iliondolewa, na ujenzi wa hekalu ukamalizika katika muda wa miaka mitano—Ezra 6:14, 15; Hag. 1:14, 15.
Kuweka Mioyo Yetu Juu ya Njia Zetu
Je, unafikiri kwamba matatizo yanapotokea tunaweza kuvunjika moyo kama Wayahudi katika siku za Hagai? Hali hiyo ikitokea, inaweza kuwa vigumu kwetu kudumisha bidii yetu ya kuhubiri habari njema. Lakini ni nini kinachoweza kutufanya tuvunjike moyo? Kwa kweli, tunaweza kuteseka kwa sababu ya ukosefu wa haki wa mfumo huu wa mambo. Mfikirie Habakuki aliyeuliza hivi: “Ninapaswa kulilia msaada kwa muda gani ili usikie, na ili utuokoe kutokana na jeuri?” (Hab. 1:2, Today’s English Version) Kwa kuwa huenda wengine wakafikiri kwamba Mungu anachelewa, Mkristo anaweza kupoteza hisi yake ya uharaka na badala yake kutanguliza maisha ya starehe. Je, unafikiri inaweza kuwa hivyo kwako? Tukiwaza kwa njia hiyo, tutakuwa tukijidanganya wenyewe. Ni jambo la maana kama nini kwetu kutii shauri la Kimaandiko la ‘kuweka mioyo yetu juu ya njia zetu’ na ‘kuamsha uwezo wetu mzuri wa kufikiri’! Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, ninapaswa kushangaa kwamba mfumo huu mwovu wa mambo umedumu kwa muda mrefu kuliko nilivyotazamia?’
Kipindi Kilichotabiriwa na Biblia
Hebu tua na ufikirie maneno ya Yesu kuhusu umalizio wa mfumo huu wa mambo. Simulizi la Marko la unabii wa Yesu kuhusu siku za mwisho linafunua kwamba Yesu alituhimiza tena na tena tuendelee kukesha. (Marko 13:33-37) Tunapata onyo kama hilo katikati ya maelezo ya kinabii kuhusu siku kuu ya Yehova ya Har-Magedoni. (Ufu. 16:14-16) Kwa nini maonyo hayo yanarudiwa-rudiwa? Vikumbusho hivyo vinahitajiwa kwa sababu baada ya watu kungoja kwa muda ambao unaonekana kuwa mrefu sana, wanaweza kupoteza hisi yao ya uharaka.
Yesu alitoa mfano ambao unaonyesha kwa nini tunahitaji kuendelea kukaa macho tunapongojea mwisho wa mfumo wa mambo. Alitoa mfano wa mwenye nyumba ambaye nyumba yake ilikuwa imevunjwa na kuporwa. Angefanya nini ili asiibiwe? Angeendelea kukaa macho usiku kucha. Yesu alimalizia mfano huo kwa kutushauri hivi: “Iweni tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja katika saa msiyofikiria.”—Mt. 24:43, 44.
Mfano huo unaonyesha uhitaji wa kuwa tayari kungoja, hata kwa muda mrefu. Hatupaswi kamwe kuhangaika sana kwamba huenda mfumo huu mwovu wa mambo umedumu kwa muda mrefu kuliko tulivyotazamia. Hatupaswi kujidanganya wenyewe kwa kuwaza kwa njia isiyo ya kweli kwamba ‘wakati wa Yehova haujaja.’ Kufikiri kwa njia hiyo kutapunguza tamaa yetu ya kuhubiri habari njema ya Ufalme.—Rom. 12:11.
Kung’oa Kabisa Mawazo Yasiyo ya Kweli
Kuhusu mawazo yasiyo ya kweli, kanuni ya Wagalatia 6:7 inatumika: “Msipotoshwe . . . Kwa maana lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.” Ikiwa shamba halilimwi, magugu yanasitawi kwa urahisi. Vivyo hivyo, tusipoamsha uwezo wetu mzuri wa kufikiri, mawazo yasiyo ya kweli yanaweza kutia mizizi katika akili zetu. Kwa mfano, huenda tukajiambia, ‘Bila shaka siku ya Yehova inakuja, lakini haiji wakati huu.’ Kubadili matarajio yetu kwa njia hiyo kunaweza kutufanya tupunguze bidii katika utendaji wetu wa kitheokrasi. Baada ya muda, tunaweza kuanza kupuuza mazoea yetu ya kiroho. Kisha, siku ya Yehova inaweza kuja juu yetu kwa ghafula.—2 Pet. 3:10.
Hata hivyo, mawazo yasiyo ya kweli hayatatia mizizi katika akili zetu ikiwa sikuzote tunajihakikishia wenyewe “mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Rom. 12:2) Moja kati ya njia bora zaidi za kutusaidia kufanya hivyo ni kusoma Neno la Mungu kwa ukawaida. Maandiko yanaweza kutia nguvu au kuimarisha usadikisho wetu kwamba sikuzote Yehova anatenda kwa wakati uliowekwa.—Hab. 2:3.
Kujifunza, kusali, kuhudhuria mikutano kwa uaminifu, na kuhubiri, pamoja na matendo yetu ya fadhili zenye upendo, yatatuwezesha “kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.” (2 Pet. 3:11, 12) Yehova atathamini bidii yetu inayoendelea. Mtume Paulo anatukumbusha hivi: “Na tusife moyo katika kufanya yaliyo mema, kwa maana katika majira yanayofaa tutavuna ikiwa hatuchoki kabisa.”—Gal. 6:9.
Bila shaka huu si wakati wa kuruhusu mawazo yasiyo ya kweli yatudanganye na kutufanya tufikiri kwamba siku ya Yehova imesukumwa mbele. Badala yake, huu ni wakati wa kutia nguvu mioyo yetu, kwa kuwa siku ya Yehova imekaribia.
[Picha katika ukurasa wa 4]
Hagai na Zekaria waliwahimiza Wayahudi wajenge hekalu
[Picha katika ukurasa wa 5]
Namna gani ikiwa mwenye nyumba angejua kwamba mwizi anakuja?