Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • wp18 Na. 1 kur. 12-13
  • 3 Hutusaidia Kuvumilia Matatizo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • 3 Hutusaidia Kuvumilia Matatizo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2018
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UGONJWA WA KUDUMU
  • HUZUNI
  • Kutoka Mshuko wa Moyo Hadi Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Sala Zinaweza Kukusaidiaje?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2021
  • Kutatua Matatizo ya Vijana
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Sala​—Ina Umuhimu Gani Kwako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2018
wp18 Na. 1 kur. 12-13

3 Hutusaidia Kuvumilia Matatizo

Kuna matatizo ambayo kwa sasa haiwezekani kuyaepuka au kuyatatua. Kwa mfano, ikiwa umefiwa na mpendwa wako au una ugonjwa wa kudumu, huenda usiwe na chochote cha kufanya zaidi ya kuvumilia hali unayokabili. Je, Biblia inaweza kukusaidia katika hali ngumu kama hizo?

UGONJWA WA KUDUMU

Rose anasema: “Nina ugonjwa wa kurithi ambao hunisababishia maumivu makali yasiyokoma. Hali yangu ya maisha imezorota.” Jambo moja lililomhangaisha zaidi ni kwamba nyakati fulani alishindwa kukazia fikira alipokuwa akijifunza Biblia au kufanya mambo mengine yanayohusiana na ibada. Lakini alitiwa moyo sana na maneno ya Yesu kwenye Mathayo 19:26: “Kwa Mungu mambo yote yanawezekana.” Rose aligundua kwamba kuna njia mbalimbali za kujifunza. Kwa sababu maumivu yake yalifanya nyakati nyingine ashindwe kabisa kusoma, alianza kusikiliza rekodi za usomaji wa Biblia na machapisho mengine yanayotegemea Biblia.a Anasema hivi: “Bila msaada huo sidhani kama ningeweza kudumisha hali nzuri ya kiroho.”

Rose anaposhindwa kufanya mambo ambayo alifaulu kuyafanya zamani, yeye hufarijiwa na maneno ya andiko la 2 Wakorintho 8:12: “Ikiwa utayari upo kwanza, hukubalika zaidi kulingana na kile ambacho mtu anacho, si kulingana na kile ambacho mtu hana.” Andiko hilo humkumbusha Rose kwamba Mungu anapendezwa na kile anachotimiza, kwa sababu anafanya yote awezayo kulingana na hali yake.

HUZUNI

Delphine, aliyetajwa awali, anasimulia hivi: “Binti yangu mwenye umri wa miaka 18 alipokufa, huzuni niliyokuwa nayo ilikuwa kubwa sana hivi kwamba nilihisi siwezi kuendelea kuishi. Hali isingeweza kurudi kama ilivyokuwa.” Hata hivyo alifarijiwa sana na maneno ya andiko la Zaburi 94:19, ambapo mtunga zaburi alimwambia hivi Mungu: “Mahangaiko yaliponilemea, ulinifariji na kunibembeleza.” Delphine anasema: “Nilisali Yehova anisaidie nipate mambo ya kufanya ili nitulize maumivu niliyohisi.”

Aliamua kutumia muda mwingi kufanya kazi ya maana sana ya kujitolea. Baada ya muda alijiona kama kalamu za watoto za kuchorea—hata zilizovunjika bado zinaweza kutumiwa kuchora. Vivyo hivyo, ingawa alihisi amevunjika, aligundua kwamba bado anaweza kuwasaidia wengine. Alisema: “Nilitambua kwamba nilipotumia kanuni za Biblia na njia ya kufikiri inayotajwa kwenye Maandiko kuwafariji wale niliojifunza nao Biblia, hiyo ilikuwa njia ya Yehova ya kunifariji na kunituliza.” Aliorodhesha majina ya watu wanaotajwa kwenye Biblia ambao walipitia vipindi vigumu vya huzuni. Aligundua kwamba, “watu wote hao walikuwa na zoea la kutoa sala.” Pia, alijifunza kwamba, “hauwezi kuvumilia ikiwa husomi Biblia.”

Jambo lingine ambalo Delphine amejifunza kupitia funzo lake la Biblia, ni kukazia fikira wakati ujao badala ya mambo yaliyopita. Tumaini linalotajwa kwenye Matendo 24:15 humfariji sana: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” Ana uhakika kiasi gani kwamba Yehova atamfufua binti yake? Delphine mwenyewe anajibu: “Ninamwona binti yangu akiwa hai wakati ujao. Tarehe yetu ya kukutana tena tayari imepangwa, na ipo kwenye kalenda ya Baba yetu wa mbinguni. Ninajiona nikiwa na binti yangu kwenye bustani yetu sawasawa kabisa na nilivyomwona na kumpenda siku aliyozaliwa.”

a Rekodi nyingi za aina hiyo zinapatikana kwenye tovuti ya jw.org.

Biblia inaweza kukusaidia upate faraja hata katika nyakati ngumu sana

MUNGU ANAWEZA KUTUSAIDIA JINSI GANI?

Biblia inatupatia jibu la wazi kabisa. Inasema hivi: “Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia, wote wanaomwitia yeye katika ukweli. Hutosheleza tamaa ya wale wanaomwogopa; husikia kilio chao cha kuomba msaada, naye huwaokoa.” (Zaburi 145:18, 19) Hiyo inatia moyo sana, sivyo? Hata hivyo, Mungu hujibu jinsi gani sala za watu ambao kwa unyoofu wanamwomba mwongozo?

KWA KUTUPATIA NGUVU:

Matatizo yanaweza kutuvunja moyo na kutufanya tuishiwe nguvu kimwili, kihisia, na kiroho. (Methali 24:10) Lakini Yehova “humpa nguvu mtu aliyechoka na kuwapa uwezo kamili wale wasio na nguvu.” (Isaya 40:29) Mtume Paulo ambaye alivumilia majaribu makali sana, alisema: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yule anayenipa nguvu.” (Wafilipi 4:13) Paulo alitiwa nguvu na roho takatifu ya Mungu. Wewe pia unaweza kumwomba Mungu akupe roho takatifu.—Luka 11:13.

KWA KUTUPATIA HEKIMA:

Namna gani ikiwa unahitaji msaada ili uelewe na kutumia ushauri wa Biblia? Mwanafunzi Yakobo aliandika: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu, naye atapewa.” (Yakobo 1:5) Unaweza kutenda kupatana na sala zako kwa kusoma Biblia na kutumia mafundisho yake. (Yakobo 1:23-25) Kadiri unavyofanya hivyo, utajionea jinsi ushauri wa Biblia ulivyo wa hekima.

KWA KUTUPATIA AMANI:

Hata unapolemewa na mahangaiko, Yehova anaweza kukusaidia upate utulivu. Neno lake linasema hivi: “Msihangaike kuhusiana na jambo lolote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani, mjulisheni Mungu maombi yenu; na amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kupitia Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Kwa nini usimwombe Yehova akupe amani?

Hata hivyo, namna gani ikiwa muda mrefu unapita bila matatizo yako kutatuliwa? Usifikiri kwamba Mungu amekuacha. Hata ikiwa matatizo yako hayaishi, Mungu anaweza kukupatia ujasiri na nguvu za kuvumilia. (1 Wakorintho 10:13) Biblia pia inaahidi kwamba wakati ujao matatizo yetu yataondolewa kabisa!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki