Amani—Unaweza Kuipataje?
KWA kuwa tunaishi katika ulimwengu wenye misukosuko, lazima tujitahidi sana ili tuwe na amani. Ingawa hivyo, hata tunapokuwa na amani kwa kiasi fulani, sisi hupambana sana ili kuidumisha. Neno la Mungu linataja mambo gani yanayoweza kutusaidia kupata amani ya kweli na inayodumu? Na tunaweza kuwasaidiaje wengine waipate?
KINACHOHITAJIWA ILI TUWE NA AMANI YA KWELI
Ili tuwe na amani ya kweli, ni lazima tujihisi tukiwa salama na wenye utulivu wa kihisia. Pia, tunahitaji kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na wengine. Na jambo muhimu hata zaidi, ili tupate amani ya kudumu ni lazima tusitawishe urafiki wa karibu pamoja na Mungu. Tunawezaje kufanya hivyo?
Mahangaiko ya maisha huwanyima watu wengi amani
Tunapotii amri na kanuni za Yehova za uadilifu, tunaonyesha kwamba tunamtumaini yeye na kwamba tunatamani kuwa na uhusiano wenye amani pamoja naye. (Yer. 17:7, 8; Yak. 2:22, 23) Kisha Yehova hutukaribia na kutubariki kwa kutupatia amani ya moyoni. Andiko la Isaya 32:17 linasema hivi: “Matokeo ya uadilifu wa kweli yatakuwa amani, na mazao ya uadilifu wa kweli yatakuwa utulivu wa kudumu na usalama wa kudumu.” Tunaweza kupata amani ya kweli kwa kumtii Yehova kutoka moyoni.—Isa. 48:18, 19.
Pia, zawadi nyingine ya pekee kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni inayotusaidia kusitawisha amani ya kudumu ni roho yake takatifu.—Mdo. 9:31.
ROHO YA MUNGU HUTUSAIDIA KUSITAWISHA AMANI
Mtume Paulo aliorodhesha sifa ya amani ikiwa ya tatu kati ya sifa za “tunda la roho.” (Gal. 5:22, 23) Kwa kuwa amani ya kweli hutokana na roho ya Mungu, ni lazima tukubali kuongozwa na roho takatifu ili tusitawishe amani ya kweli. Acheni tufikirie njia mbili ambazo Mungu kupitia roho yake anatusaidia kupata amani.
Kwanza, roho ya Mungu hutusaidia kusitawisha amani tunaposoma kwa ukawaida Neno la Mungu lililoongozwa na roho. (Zab. 1:2, 3) Tunapotafakari ujumbe wa Biblia, roho takatifu hutusaidia kuelewa njia ya Yehova ya kufikiri au maoni yake kuhusu mambo mbalimbali. Kwa mfano, kwenye Biblia tunaona jinsi ambavyo Yehova hudumu akiwa mwenye amani na kwa nini amani ni sifa muhimu sana kwake. Tunapotumia mambo hayo yaliyo katika Neno lake, tunakuwa na amani nyingi zaidi maishani.—Met. 3:1, 2.
Pili, tunapaswa kusali ili tupate roho takatifu ya Mungu. (Luka 11:13) Yehova anatuahidi kwamba tukiomba msaada wake, “amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote itailinda mioyo [yetu] na nguvu [zetu] za akili kupitia Kristo Yesu.” (Flp. 4:6, 7) Tunaposali kwa ukawaida ili tupate roho takatifu ya Yehova, Mungu wetu hutupatia amani ya moyoni ambayo ni wale tu walio na urafiki wa karibu pamoja naye hufurahia.—Rom. 15:13.
Baadhi ya ndugu wametumiaje shauri hilo la Kimaandiko na kufanya marekebisho yaliyowasaidia kufurahia amani inayodumu—pamoja na Yehova, wao wenyewe, na pamoja na wanadamu wenzao?
JINSI WALIVYOPATA AMANI YA KUDUMU
Kutaniko la Kikristo leo, lina watu ambao hapo awali walikuwa na mwelekeo wa ‘kukasirika upesi’ lakini ambao sasa wanawajali wengine, ni wenye fadhili, subira, na wanashughulika na wengine kwa amani.a (Met. 29:22) Mambo yaliyoonwa kuhusu wahubiri wawili wa Ufalme waliosaidiwa kudhibiti hasira na kusitawisha amani pamoja na wengine yanathibitisha ukweli huo.
Kutumia kanuni za Biblia na kusali ili tupate roho takatifu ya Mungu kutatusaidia kupata amani
David alikuwa na mtazamo mbaya ulioathiri mazungumzo yake. Kabla ya kujiweka wakfu kwa Mungu, alizoea kuwachambua wengine na kutumia maneno makali alipozungumza na watu wa familia yake. Baada ya muda, David aliona uhitaji wa kubadilika na kuwa mwenye amani. Alifanya nini ili awe mwenye amani? Anasema, “Nilianza kutumia kanuni za Biblia maishani, na kwa sababu hiyo heshima kati yangu na watu wangu wa familia ikaongezeka.”
Rachel aliathiriwa na malezi yake. Anakiri hivi, “Hata sasa ningali napambana na hasira kwa sababu nililelewa katika familia ambapo watu walizoea kulipuka kwa hasira.” Ni nini ambacho kimemsaidia awe mwenye amani? Anasema hivi: “Mimi husali kwa ukawaida na kumwomba Yehova anisaidie.”
David na Rachel ni mifano miwili tu ya jinsi ambavyo kutumia kanuni za Kimaandiko zilizoongozwa na roho ya Mungu na kutegemea roho takatifu hutusaidia kusitawisha amani. Ingawa tunaishi katika ulimwengu wenye hatari, ni wazi kwamba tunaweza kuwa na amani ya moyoni inayochangia umoja ndani ya familia zetu na pamoja na Wakristo wenzetu. Hata hivyo, Yehova anatuhimiza “[tufanye] amani na watu wote.” (Rom. 12:18) Je, kweli hilo linawezekana, na tunanufaikaje tunapojitahidi kufanya amani?
FUATIA AMANI PAMOJA NA WENGINE
Kupitia huduma yetu ya shambani, tunawaalika watu wanufaike na ujumbe wetu wenye amani kuhusu Ufalme wa Mungu. (Isa. 9:6, 7; Mt. 24:14) Inafurahisha kwamba watu wengi wameukubali. Kwa sababu hiyo, hawalemewi tena na hisia za kukata tamaa au kukasirika kwa sababu ya mambo wanayoona yakitendeka. Badala yake, wamepata tumaini halisi la wakati ujao na wanachochewa ‘kutafuta amani na kuifuatia.’—Zab. 34:14.
Hata hivyo, si wote wanaokubali ujumbe wetu mwanzoni. (Yoh. 3:19) Licha ya hilo, roho ya Mungu hutuwezesha kuwahubiria habari njema kwa njia ya amani na heshima. Kwa njia hiyo, tunatii maagizo haya ambayo Yesu alitoa kuhusu huduma kwenye Mathayo 10:11-13: “Mnapoingia katika nyumba, wasalimuni watu wa nyumba hiyo. Ikiwa nyumba hiyo inastahili, amani mnayoitakia na iwe juu yake; lakini kama haistahili, amani yenu na iwarudie ninyi.” Tunapotii ushauri huo wa Yesu, tutabaki na amani yetu na kuna uwezekano kwamba mtu huyo huenda akasikiliza ujumbe wetu wakati ujao.
Tunachangia hali ya amani tunapowafikia maofisa wa serikali kwa njia ya heshima, kutia ndani wale wanaopinga kazi yetu. Kwa mfano, serikali ya nchi moja barani Afrika ilikataa kutoa kibali cha kujenga Majumba ya Ufalme kwa sababu ya ubaguzi waliokuwa nao. Ili kutafuta suluhisho kwa njia ya amani, ndugu mmoja ambaye hapo awali alikuwa mmishonari katika nchi hiyo alitumwa kwenda kuzungumza na Balozi wa nchi hiyo jijini London, Uingereza. Alipaswa kumwambia Balozi huyo kuhusu kazi ya amani inayofanywa na Mashahidi wa Yehova katika nchi yake. Ikawaje?
Anasimulia hivi: “Nilipofika kwenye mapokezi, nilitambua kwamba mwanamke aliyefanya kazi kwenye mapokezi alikuwa amevalia mavazi ya watu wanaozungumza lugha ambayo nilikuwa nimejifunza. Hivyo nilimsalimu kwa lugha yake. Kwa mshangao aliniuliza, ‘Ungependa tukusaidiaje?’ Nilimwambia kwa upole kwamba ningependa kuzungumza na Balozi. Alimpigia simu, naye akaja na kunisalimu katika lugha yake. Baada ya hapo alinisikiliza kwa makini nilipokuwa nikieleza kuhusu kazi ya amani inayofanywa na Mashahidi wa Yehova.”
Maelezo yenye heshima ambayo ndugu huyo alitoa yalimfanya Balozi huyo aelewe vizuri kazi yetu na kuondoa ubaguzi aliokuwa nao. Baadaye, serikali ya nchi hiyo iliondoa vizuizi vya ujenzi ilivyokuwa imeweka. Unaweza kuwazia jinsi akina ndugu walivyofurahia matokeo hayo ya amani! Kwa kweli, kuwatendea wengine kwa heshima huleta manufaa tele, kutia ndani amani.
FURAHIA AMANI MILELE
Leo, watu wa Yehova hufurahia paradiso ya kiroho iliyojaa amani. Utachangia amani ya paradiso hiyo unapoendelea kusitawisha sifa hiyo ya tunda la roho maishani mwako. Jambo muhimu hata zaidi, utapata kibali cha Yehova na kufurahia amani tele na inayodumu katika ulimwengu mpya wa Mungu.—2 Pet. 3:13, 14.
a Sifa ya fadhili itazungumziwa katika makala ya wakati ujao katika mfululizo huu wa sifa za tunda la roho takatifu ya Mungu.