Kuendeleza Huduma Yetu Bila Kuacha
1 Tamasha ya ulimwengu huu inapita kasi tunaposonga mbele ndani zaidi katika wakati wa mwisho. (1 Kor. 7:31) Katika kutimiza unabii wa Biblia, matukio yenye kuutikisha ulimwengu yanatukia. Tunapofikiria yale yanayotendeka katika ulimwengu unaotuzunguka na ndani ya tengenezo la kitheokrasi, tunaweza kuthamini jinsi lilivyo jambo la uharaka kwamba sisi tuhubiri “habari njema” za Ufalme.—Marko 13:10, NW.
2 Kiongozi na Kielelezo wetu, Yesu Kristo, ndiye aliyetoa amri ya kufanya wanafunzi. Kwa kufanya hivyo, alitoa uhakikisho wa kufanikiwa kwa kazi hiyo kwa ahadi yake, “Mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:19, 20, NW) Wanafunzi wa Yesu walichukua kwa uzito maneno yake, na hata walipokuwa wanakabili upinzani mkali, “hawakuacha kufundisha na kuhubiri habari njema za Yesu kwamba ni Kristo.” (Matendo 5:42) Jinsi walivyotuwekea kielelezo kizuri!
3 Tunaposoma Kitabu-Mwaka 1990, tunaona kwamba Yehova amebariki huduma yetu kwa kutokeza maongezeko mazuri ya wanafunzi wapya. Katika mabara fulani maongezeko yaliyoripotiwa ni ya kustaajabisha kikweli. Ongezeko la ujumla ulimwenguni pote linazidi sana yote ambayo yeyote wetu angeweza kuwazia miaka michache tu iliyopita. (Isa. 60:22) Lakini vipi juu ya eneo la mahali petu? Na vipi juu ya huduma yetu mmoja mmoja? Je! sisi tunaonea shangwe sehemu yetu katika huduma na pia huduma ya pamoja ya wafanya kazi wenzetu kila mahali? Je! sisi tunaendeleza jitihada yetu mmoja mmoja katika huduma bila kuacha?
SEHEMU YETU MMOJA MMOJA
4 Ni wazi kabisa, si maeneo yote yenye mazao jinsi ile ile. (Linganisha Mathayo 13:23.) Pia ni kweli kwamba maeneo fulani, kama vile Ailandi na Kwibeki, yamekuwa yenye kuzaa baada tu ya miaka mingi ya kazi ya bidii kwa upande wa wahudumu wenye juhudi. Kuna wapinzani wengi katika maeneo fulani, na katika mengine watu kwa ujumla ni wenye ubaridi na wasioitikia ujumbe wa Ufalme. Na bado katika sehemu nyingine, kuna wafanya kazi wengi sana shambani kwamba kuna eneo dogo tu la kueneza. Lakini hata tuwe tunafanyia kazi eneo la aina gani, bidii yetu haipasi kupungua kamwe. Mtume Paulo aliandika, “Tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho.” (Gal. 6:9) Maneno yake ya kushauri yanahusu Wakristo wote. Tutawezaje kufanya hilo? Ni nini kitakachotusaidia tuendelee na huduma yetu bila kuacha?
5 Tunaweza kuendelea kuwa watendaji na kufanya huduma yetu ifanikiwe tukiitibari Yehova na kutegemea nguvu zake zitutegemeze. Sikuzote kumbuka kwamba Yehova ndiye anayefanya shamba lizae. (1 Kor. 3:6) Katika kujibu sala zetu za msaada, Yehova huandaa shauri, maagizo yanayotumika, na wingi wa ugavi wa fasihi za Biblia kwa ajili ya matumizi yetu ya kibinafsi na kwa ajili ya kusaidia wengine wapate kumjua. Je! sisi tunatumia kwa manufaa kamili maandalizi hayo?
DUMISHA MTAZAMO UNAOFAA
6 Ikiwa tuna mtazamo hasi, hilo laweza kuwa kipingamizi kikubwa kwa huduma yenye mazao. Ikiwa tumesitawisha maoni yasiyofaa juu ya watu katika eneo letu kwa msingi wa kutoitikia kwa wakati uliopita, mtazamo huo utaonyeshwa na namna yetu ya sauti, ishara ya sura, na kukosa kujitayarisha kwa juhudi kwa ajili ya utumishi wa shambani. Tumepokea utume wa kuhubiri na kufundisha, na sisi hatujaambiwa kwamba kazi imekwisha. Tamaa yetu ya kuwa watiifu na wenye kujitiisha kwa mwelekezo wa kimungu yapasa kutuchochea tuendelee na huduma yetu bila kuacha.
7 Kusudi la Yehova kuhusu kuonya waovu na kukusanya wanafunzi litatimizwa kabla ya mwisho kuja. Tunaweza kushiriki katika shangwe ya huduma sasa na kutazamia baraka za milele kati ya watu wa Mungu tukidhihirisha imani yetu na upendo kwa kuendelea na huduma yetu bila kuacha.