Kufanya Maendeleo Katika Huduma
1 Kuna mithali ya kale ambayo husema: “Anza ulipo. Lakini usikae ulipo.” Mithali hiyo inatumika kama nini kwa habari za kufanya maendeleo katika Huduma! Ulipoanza katika huduma, huenda ukawa uliweza kufanya utoaji mfupi tu wa ujumbe wa Ufalme. Lakini ikiwa miaka michache imepita nawe hujasonga mbele kupita hatua hiyo, ukiwa umekuwa ukikaa ulipokuwa, waweza kufanya nini?
2 Hatua ya kwanza ni kumwomba Yehova akupe hekima unayohitaji ili kufundisha kwa ustadi. (Mit. 15:14; Yak. 1:5) Hatua ya pili ni kufanya kazi kupatana na sala yako. Tenga wakati fulani usome utoaji mbalimbali katika kitabu Kutoa Sababu. Tafuta mmoja ambao unahisi kwamba waweza kutumia kwa mafanikio, kisha uusome tena na tena utoaji huo mpaka ukae waziwazi akilini. Hatua ya tatu ni kuandamana na akina ndugu shambani ili uweze kutumia utoaji uliotayarisha.
MARAFIKI WA KUKUSAIDIA
3 Huenda ukawa unasema, ‘Ni rahisi kusema hilo kuliko kulifanya.’ Ni kweli, lakini ndiyo sababu una marafiki wa kukusaidia. Ukiwa kijana, ongea na wazazi wako au wahubiri wenye ujuzi ambao ni wahudumu wenye kutoa mazao. Waulize madokezo juu ya jinsi ya kuzungumza na watu milangoni. Huenda wakadokeza mwe na vipindi vya mazoezi ambapo waweza kujaribu utoaji wako. Wanaweza kuwa wenye nyumba, wakizusha vipingamizi vilivyo vya kawaida tunavyokutana navyo milangoni. Kwa kufanya mazoezi waweza kujifunza kuzungumza na watu kwa ustadi.
4 Una marafiki wengine ambao waweza kukusaidia. Kuna mapainia ambao wamejifunza mbinu za kuhubiri kupitia mambo waliyojionea na kwa kuhudhuria Shule ya Utumishi wa Painia. Kiongozi wa funzo la kitabu lenu au mwangalizi wa utumishi huenda pia wakawa katika hali ya kufanya kazi pamoja nawe nyumba kwa nyumba na kukuonyesha zaidi jinsi ya kuongea na kutoa sababu kwa watu.
KUFUATIA KUPENDEZWA KULIKOONYESHWA
5 Tunapendezwa kuwapa watu wanaokubali fasihi zetu usaidizi zaidi wa kiroho. Hilo lamaanisha ni lazima turudi kuchochea kupendezwa zaidi. Kabla ya kufanya ziara ya kurudia, pitia yale uliyokuwa umesema katika ziara ya kwanza ili uweze kusitawisha kwa mafanikio zaidi habari ambayo ilinasa kupendezwa kwao. Pia, kumbuka kwamba ingawa sisi tunapanda na kumwagilia maji, Yehova ndiye huifanya ikue. Omba mwongozo wake kabla ya kufanya ziara hiyo. ( 1 Kor. 3:6; 2 Kor. 9:10) Tusaidiapo wengine wajifunze, sisi wenyewe twafanya maendeleo ya kibinafsi.
6 Hatua ya maana inayofuata ni kuanza na kuongoza funzo la Biblia. Ikiwa bado wewe hujafikia hatua hiyo katika kufanya maendeleo kwako katika huduma, endelea kumwendea Yehova kwa sala na kumwomba akusaidie upate na kulisha mtu mwenye mfano wa kondoo. Huenda ukalipata kuwa jambo lenye kusaidia kuangalia jinsi mwalimu mwenye mafanikio huongoza funzo la Biblia na kisha uige njia zake za kufundisha. Pia rudia habari kama ile inayopatikana katika Mnara wa Mlinzi wa Januari 1, 1985, kurasa 11-16. Kwa kujitayarisha hivyo, utakuwa tayari kuongoza funzo wakati sala zako zinapojibiwa.
WEKA NA KUFIKIA MIRADI
7 Kufikia miradi ya kufundisha, kufanya ziara za kurudia, na kuongoza mafunzo yenye mafanikio zaidi huchukua wakati. Je! wewe ungeweza kujiwekea mradi mwingine, ule wa kuwa painia msaidizi au wa kawaida? Uendeleapo kufanya maendeleo katika huduma, waweza kuwa chanzo cha kitia-moyo kwa wengine. Baraka nyingi kutoka kwa Yehova zaweza kuwa zako ikiwa hutakaa pale ulipo bali unazidi kufanya maendeleo.