Mpango wa Funzo la Kitabu la Kundi
Sehemu ya 2: Uhitaji wa Kutayarisha na Kushiriki
1 Neno la Yehova humtangaza mtu ambaye hupata hekima na kujipatia utambuzi kuwa mwenye furaha, kwa kuwa thawabu ni kubwa. (Mit. 3:13, 14, 16-18) Hekima ya kiroho ni yenye thamani kubwa na ni yenye kuokoa uhai. Inamwezesha Mkristo kutumia kwa faida katika ibada yenye utendaji maarifa apatayo kutoka kwa Neno la Mungu, katika kutatua matatizo ya siku kwa siku, na katika kufanya maamuzi kuhusiana na miradi yake maishani.
2 Funzo la Kitabu la Kundi limekusudiwa kutusaidia tujifunze na kutumia Neno la Mungu na kwa njia hiyo tunakua katika hekima na ufahamu wa kiroho. Kwa hiyo kuhudhuria kwa kawaida Funzo la Kitabu la Kundi, kwapaswa kuwe sehemu muhimu katika programu yetu ya kibinafsi ya kupata hekima.—Mit. 4:7-9.
TAYARISHA KIKAMILI
3 Baadhi ya wale walioshirikiana na kundi la karne ya kwanza hawakujitahidi kwa bidii kujifunza kweli na kwenda sambamba na nuru yenye kusonga mbele. Walibaki wakiwa vitoto katika Kristo na hivyo hawakufahamiana na neno la uadilifu. (Ebr. 5:11-13) Mtume Paulo alilihimiza kundi ‘likaze mwendo ili kufikia utimilifu [ukomavu, NW].’ (Ebr. 6:1) Kwa wazi, hilo lataka zaidi ya kusikiliza kijuujuu wengine wakizungumza kweli. Fikira na utafiti vyatakwa ili kuamusha “nia zetu safi,” na ni lazima sisi tujitahidi kwa bidii.—2 Pet. 3:1, 2; Luka 13:24.
4 Kutayarisha kikamili kwa ajili ya Funzo la Kitabu la Kundi huzidisha uelewevu wetu na hujenga uthamini kwa habari. Hata hivyo, utayarishaji wenye mafanikio, hutaka zaidi ya kusoma mafungu na kupiga mistari kwa haraka chini ya yale majibu ya msingi ya maswali. Twahitaji wakati wa kuonja ladha ya habari kwa kutafakari juu ya maana na thamani yake kwetu sisi binafsi. Angalia katika Biblia maandiko yaliyotajwa na kufikiria jinsi yanavyohusiana na mambo katika mafungu. Angalia katika kamusi maneno ambayo hayakufahamika kikamili.
5 Kwa baadhi yetu, funzo la binafsi huenda likawa kazi ngumu, nalo linatumia wakati; lakini, lo, ni lenye kunufaisha kama nini! Paulo alielekeza kwenye matokeo ya funzo kama hilo, akisema hivi: “Lakini chakula kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.” (Ebr. 5:14) Funzo la binafsi kama hilo hutusaidia kukua kufikia ukomavu, ili tuweze kupambanua mwendo ufaao tunapoelekewa na maamuzi ya kufanya.
SHIRIKI
6 Yatupasa tujitahidi kushiriki katika kila mkutano. Kwa nini? Si kwamba tu maelezo yetu yaliyotayarishwa vizuri ni wonyesho wa imani yetu bali pia huwatia moyo na kujenga ndugu zetu. (Rum. 10:10; Ebr. 10:23-25) Ushiriki wenye kutenda katika Funzo la Kitabu la Kundi hutimiza pia sehemu yenye maana katika ukuzi wetu wa kiroho. Wenye ujuzi, watoto, na watu wapya wenye kupendezwa wote wakitoa maelezo sana, kikundi kinafurahia maelezo mengi ya namna mbalimbali. Hiyo ni yenye kuelimisha na kuburudisha kwa wote.—kmSW 4/86 uku. 3.
7 Tukijitayarishia kwa bidii Funzo la Kitabu la Kundi, tuhudhurie kwa kawaida, na kushiriki sana, utafutaji wetu wa hekima utafanikiwa nasi ‘tutapata kumjua Mungu.’—Mit. 2:4, 5.