Kuishi kwa Utimamu wa Akili na Uadilifu
1 Tunaishi katika ulimwengu ulio na uvutano wenye nguvu kuelekea hali ya kutomwogopa Mungu. Viwango vya mfumo huu vyazidi kushuka sana. (2 Tim. 3:3) Tukiwa Wakristo, tunapaswa kuchukua msimamo kwa yaliyo sawa na kuelewa ni kwa nini tunapaswa kuendelea kufanya hivyo. Lakini ni mwelekezo na mwongozo gani unaopatikana? Tunapaswa kufuata viwango vipi? “Kuishi kwa Utimamu wa Akili na Uadilifu” ndicho kichwa chenye kutia moyo kilichochaguliwa cha programu yetu ya siku ya kusanyiko la pekee la mwaka wa utumishi wa 1993.—Tit. 2:12.
2 Kupitia hotuba, maonyesho, na mambo yaliyoonwa, tutajifunza jinsi tunavyoweza kujijenga ili kukinza hali ya kutomwogopa Mungu na kukataa katakata tamaa za kilimwengu. Tutaona pia jinsi inavyowezekana kuishi na utimamu wa akili na uadilifu katika mfumo huu mwovu. Maandalizi ya kutusaidia kulinda nguvu zetu za akili yataonyeshwa. (1 Pet. 4:7) Wazazi na vijana watataka hasa kutoa uangalifu kwa hotuba na mahoji katika programu ya alasiri. Hizo zitakazia uhitaji wa kupata hekima na ujuzi wa kimungu na kufanya kazi pamoja ili kujenga wakati ujao wa kitheokrasi wenye furaha.
3 Ingawa tumezungukwa na ulimwengu usiomwogopa Mungu, Neno la Mungu hutufunza juu ya mwendo ulio bora zaidi kufuata. Manufaa za kutii shauri la Biblia zitakaziwa katika hotuba “Zionee Shauku Baraka Zako Katika Ulimwengu Usio na Shangwe.” Tunapojitayarisha kuhudhuria, tunataka kukumbuka kwamba kusikiliza programu kwa makini na kutumia shauri kutatusaidia tuwe wenye matokeo zaidi katika utumishi wetu kwa Yehova.—Flp. 3:15, 16.