Chochea Wengine Wamtazame Yesu Kwa Mkazo
1 Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi ni kitabu chenye kutokeza. Sura zacho 133 zaweza kuwachochea wasomaji wamtazame Yesu kwa mkazo na kuwasukuma waige kielelezo chake. Imesemwa vizuri kwamba wafalme wote waliopata kutawala, wakijumlishwa pamoja, hawakuwa na uvutano juu ya maisha ya mwanadamu katika dunia hii kwa nguvu nyingi kama vile Yesu amekuwa nao. Wale wanaomtazama Yesu kwa mkazo kwa hakika watanufaishwa.
2 Yesu aliwafundisha wanafunzi wake juu ya Baba yake na alitoa kielelezo cha sifa za Mungu zenye thamani kubwa. Mioyo yetu inasukumwa tunapochunguza uwezo mzuri sana wa Yesu akiwa mwalimu, uongozi wake usio na hofu, na huruma yake nyororo. Tunapokumbuka mateso yake alipotoa uhai wake ili atufidi sisi, tunasukumwa na uthamini! Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi chaweza kuwasaidia watu wamwone Yesu katika njia hiyo.
3 Tayarisha Kikamili: Jitayarishe vizuri ili kuanzisha mazungumzo ya Biblia yatakayowachochea wengine wamtazame Yesu kwa mkazo. Vikundi vya familia na wengine wanaweza kujizoeza pamoja. Jitahidi kuamsha kupendezwa na kuwasukuma watu wasome kitabu Mtu Mkuu Zaidi. Ikiwa hakuna kupendezwa kwingi mwanzoni, twaweza kuacha trakti au labda broshua au gazeti.
4 Tunaweza kuamuaje kama mtu anapendezwa kikweli? Ikiwa mtu anasikiliza kwa uangalifu, anauliza maswali, au anakaza fikira hasa juu ya yale tunayosoma katika Biblia, hilo laweza kuwa wonyesho wa kupendezwa kwa moyo mweupe. Nyakati nyingine mwenye nyumba anaonyesha uthamini kwa ziara zetu au anasema amefurahia kusoma fasihi yetu. Ikiwa tunaonyesha kitabu hicho naye anakichunguza kwa utayari au auliza jinsi angeweza kujipatia kimoja, hilo laonyesha kupendezwa kikweli.
5 Kama ilivyokaziwa katika Huduma ya Ufalme Yetu mwezi uliopita, sisi huithamini fasihi yetu na kwa kuwa hatuwezi kuzungumza mambo yote milangoni ni vizuri kuwa na kichapo cha kumwachia mwenye nyumba. Kwa hiyo, hatungeamua kimapema uwezo wa mwenye nyumba wa kukubali kitabu Mtu Mkuu Zaidi.
6 Mazungumzo yetu kutoka nyumba kwa nyumba wakati wa Desemba yatakazia Yesu na kuwatia watu moyo wapate kumjua vema zaidi. Kwa kutokeza mambo yanayoonyeshwa katika kitabu Mtu Mkuu Zaidi, tunaweza kuwasaidia watu wamwone Yesu, si akiwa mtu wa kihistoria tu, bali akiwa Mwana wa Mungu na Mfalme anayetawala wa serikali itakayosuluhisha matatizo yote ya ainabinadamu.
7 Mtu mmoja ambaye mara nyingi hafurahii kusoma alionyesha uthamini kwa kitabu Mtu Mkuu Zaidi, akisema kwamba kilifanya kusoma kuwe jambo la kufurahisha mwishoni mwa siku yake. Acheni tuwasaidie wengine wahisi vivyo hivyo, tukijitahidi kadiri tuwezavyo kuwachochea wamtazame Yesu kwa mkazo kwa kusoma kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi kwa kupendezwa kikweli.