Kuonyesha Hali ya Kutopendelea Katika Huduma Yetu
1 “Mungu hana upendeleo,” akasema Petro, bali “mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.” (Mdo. 10:34, 35) Huduma yetu leo huendeshwa kwa kutambua kikamili kweli hiyo iliyosemwa waziwazi. Hivyo, ni jambo la maana tutie kila jitihada kushinda kizuizi chochote kinachoweza kutuzuia tusifikie kila mtu na habari njema.
2 Tunapohubiri nyumba kwa nyumba katika sehemu fulani, ni jambo la kawaida kuwapata watu ambao hawasemi au kuelewa lugha inayotumiwa katika kutaniko letu. Kizuizi cha lugha huzuia watu fulani wasinufaike kikamili na ujumbe wa Ufalme tuhubirio. Miongoni mwao ni viziwi, wanaowasiliana kwa lugha ya ishara. Ni nini laweza kufanywa ili kusaidia kushinda kizuizi cha lugha kinachotuzuia tusiwafikie watu hao na habari njema kwa matokeo?
3 Unapopata mtu katika eneo ambaye ni kiziwi au mtu ambaye haelewi lugha inayotumiwa na kutaniko, wapaswa uandike hilo na upate kujua kama kuna mtu katika kutaniko lenu au katika kutaniko jingine anayeelewa lugha inayosemwa na mtu huyo. Ukimpata mtu kama huyo unaweza kumkabidhi ziara hiyo. Huenda ikanufaisha kuandamana naye katika ziara mara ya kwanza.
4 Huenda hilo lisihitajike katika visa fulani. Kwa kielelezo, yaelekea wahubiri wengi katika Afrika Mashariki wajua ni makutaniko gani, ikiwa yapatikana, wanayoweza kuwaelekeza watu wanaosema lugha fulani. Katika visa fulani huenda marekebisho ya mipaka ya eneo yakahitajiwa ili kutaniko linalotumia lugha hiyo lishughulikie eneo hilo.
5 Ikiwa hakuna kutaniko au kikundi katika eneo la ujumla kinachoweza kutoa ushahidi katika lugha inayohitajiwa, huenda kukawa na mhubiri katika mojawapo makutaniko ya kwenu anayejua lugha hiyo na anayeweza kushughulikia ziara hiyo. Ikiwa hata baada ya kuwasiliana na mwangalizi wa jiji hakuna mtu anayepatikana anayesema lugha hiyo, ndugu wenyeji wapaswa wafanye kila wawezalo ili kuhakikisha kwamba ushahidi umetolewa. Broshua Furahia Milele Maisha Duniani! imethibitika kuwa yenye kusaidia sana katika hali hizo.
6 Kila mhubiri apaswa awe macho kutumia vikaratasi vya kufuatia kupendezwa kadiri inavyohitajiwa. Kwa kutia bidii-nyendelevu ili kuwafikia watu wote na habari njema bila kujali lugha yao, tutakuwa tukionyesha upendo wa Mungu wetu, Yehova, “ambaye hutaka watu wote waokolewe, na kupata kujua yaliyo kweli.”—1 Tim. 2:4.