Toa Kitabu Vijana Huuliza
1 Ingawa kitabu Upeo wa Ufunuo kinatolewa mwezi huu, huenda ukaamua kutoa kitabu Vijana Huuliza ikiwa wazungumza na mzazi au kijana ambaye anahangaikia matatizo ambayo hutatiza vijana.
2 Huenda ukaona yafaa kusema hivi:
◼ “Kukua katika nyakati hizi zenye taabu si rahisi. Vijana hukabili hali mpya ambazo huwataka wafanye maamuzi mazito. ‘Je! ninywe kileo? Nitumie dawa za kulevya? Ni mwenendo gani unaofaa nikiwa na mtu wa jinsia tofauti?’ Vijana waulizapo juu ya masuala hayo ya msingi, mara nyingi wao hujawa na majibu yenye kupingana. Wewe wafikiri wengi wao hugeukia wapi ili kupata shauri? [Ruhusu maelezo.] Kitabu hiki, Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, chaandaa habari yenye kusaidia. [Elekeza fikira kwenye orodha ya yaliyomo, ukionyesha zile habari tofauti-tofauti zinazozungumzwa.] Vijana wanahitaji majibu ya moja kwa moja na ya kweli. Majibu yaliyomo katika kitabu hiki yanaungwa mkono na yale ambayo Biblia husema.”
3 Huu ni utoaji mwingine uwezao kutumia:
◼ “Vijana wanapatwa na mibano mingi sana leo. Wanahitaji msaada ili wakabiliane nayo kwa mafanikio. Tunapojaribu kadiri tuwezavyo tuwasaidie, je, hatutafuti kitu fulani kiandaacho mwongozo wenye kutumika? [Ruhusu elezo.] Baadhi ya mibano mikali zaidi hutoka kwa vijana wengine, marika wao. Angalia picha zilizomo kwenye kurasa 76 na 77 katika kitabu hiki. [Elekeza fikira kwenye maelezo mafupi ya picha hizi na kwenye mafungu yenye herufi za italiki kwenye ukurasa 77.] Kurasa zinazofuata katika sura hii zatoa majibu yenye haki, yafanyayo kazi.”
4 Hizi kwa kweli ni “nyakati zenye hatari,” hasa kwa vijana. (2 Tim. 3:1) Kitabu Vijana Huuliza kwa kweli chaweza kusaidia kijana akabiliane na magumu ya leo kwa mafanikio. Sura hizo 39 zina vielezi vingi, na makala ni halisi na zenye kutumika. Kwa hiyo pindi ikijitokeza wakati wowote, uwe chonjo kutumia kichapo hiki kizuri.