Mikutano ya Maana ya Utumishi wa Shambani
1 Kwenye Luka 10:1-11, tuna rekodi ya mkutano ambao Yesu alifanya akiwa na wale wanafunzi wapya 70 waliokuwa wamepewa mgawo wa kuwasaidia wajitayarishe kwa ajili ya utumishi wa shambani. Alitoa maelekezo hususa ya kuwasaidia wawe na mgango, watayarishe watakayosema, na washughulikie hali ngumu. Twaweza kujifunza kwa kuchunguza habari hii.
2 Ni wazi kwamba wanafunzi wote 70 walikuwapo kwenye mkutano huo pamoja na Yesu. Wakati mwingi hupotezwa kwenye mikutano ya utumishi wa shambani watu fulani wakizoea kuja wamechelewa. Kufika kwao kwa kuchelewa hufanya ilazimu kupanga tena vikundi na pia migawo ya eneo. Jambo hili mara nyingi hufanya kikundi chote kichelewe. Sisi sote twaweza kufanya sehemu yetu kwa kufika kwa wakati na kuwa tayari kwenda kwenye eneo upesi.
3 Yesu alikipa kikundi kichwa mahususi cha mazungumzo ya kutumia, yaani, “ufalme wa Mungu.” (Lk. 10:9) Tumepewa mgawo wa kuhubiri ujumbe uo huo, nasi huthamini kwa kawaida madokezo yenye msaada ya yale tunayopaswa kusema. Kiongozi anaweza kurejezea kitabu Kutoa Sababu, ambacho hutoa matangulizi tofauti-tofauti zaidi ya 40 na Maandiko yanayoyahusu ambayo yanaweza kutumiwa katika hali nyingi mbalimbali. Pitio fupi la utoaji mmoja au mawili laweza kutusaidia tuwe na jambo la kusema akilini, likituwezesha tuseme kwa ujasiri milangoni.
4 Yesu hakuambia wanafunzi wake jambo la kusema tu bali pia na jinsi ya kulisema. (Lk. 10:5, 6) Maonyesho katika programu ya Mkutano wa Utumishi kila juma hutuonyesha jinsi tunavyoweza kujieleza wenyewe kwa matokeo. Kiongozi anaweza kupitia yaliyoonyeshwa katika mkutano uliopita na atoe madokezo ya jinsi yanavyoweza kutumiwa katika utumishi siku hiyo. Onyesho fupi lililotayarishwa la utoaji mfupi wa Kimaandiko waweza kutusaidia tukazie mawazo yetu na kuyaweka kwa maneno.
5 Yesu aliwafunza wanafunzi wake juu ya mwenendo wao pia. (Lk. 10:7, 8) Kiongozi vilevile anaweza kutupa mwelekezo wa kutusaidia tuepuke chochote kitakachotukengeusha kutoka kazi yetu. Anaweza kutuonya juu ya kujikusanya katika pembe za barabara au kupoteza wakati tukibishana na wapinzani. Anaweza kutukumbusha juu ya uhitaji wa kuweka rekodi za nyumba kwa nyumba zilizo sahihi au umuhimu wa kuwa na vichapo mbalimbali vya lugha tofauti-tofauti. Wazazi huenda wakahitaji kikumbusha cha kuwa waangalifu kusimamia watoto wao.
6 Wanafunzi 70 walishirikiana na maagizo ya Yesu nao baadaye “wakarejea wakiwa na shangwe.” (Lk. 10:17) Tukitumia mwelekezo tunaopata kwenye mikutano ya utumishi wa shambani, sisi pia twaweza kutazamia shangwe nyingi katika kuhubiri ujumbe wa Ufalme.—Mdo. 13:48, 49, 52.