Funzo la Kibinafsi—Jambo la Kuhangaikiwa
1 Ni mambo gani hutupa sababu ya kuhangaika kwa uzito? Twapaswa kuhangaikia sana kujenga na kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Funzo la kibinafsi hutimiza fungu kubwa katika kusitawisha ukaribu wa aina hiyo. Leo, wachache kati yetu wana hali zinazoruhusu kutumia vipindi virefu vya wakati katika kutafakari na funzo la kibinafsi. Lakini, tusiposoma Neno la Mungu kwa ukawaida, twaweza kudhoofika kufikia hatua ya kukosa nguvu ya kukinza roho ya ulimwengu na tamaa zake za kimwili.
2 Kuza Tamaa ya Lile Neno: Tulipojifunza juu ya makusudi ya Mungu kwa mara ya kwanza, yamkini tulitamani kutwaa ujuzi zaidi. Hata hivyo, kwa kipindi fulani cha wakati, huenda njaa yetu ya lishe ya kiroho ilififia. Huenda kukawa na uhitaji wa ‘kutamani’ chakula cha kiroho. (1 Pet. 2:2) Twaweza kusitawishaje tamaa hiyo?
3 Harufu ya chakula kipendwacho itachochea umivu kali la njaa kwa sababu ya kumbukumbu zenye kupendeza. Vipindi vifupi vya funzo la kibinafsi vyaweza kutuathiri katika njia hiyohiyo kiroho. Kufurahia mimego michache ya kiroho kwaweza kuzidisha hamu yetu ya kweli zenye kina zaidi. Utoshelezo utokanao na kujifunza waweza kututia moyo tuchimbe kwa kina zaidi katika Neno la Yehova.
4 Sitawisha Kawaida Yenye Matokeo Zaidi Kwako: Watu fulani huweka kando jioni yote ili wafanye funzo la kibinafsi, ilhali wengine hupendelea vipindi vifupi zaidi na vingi zaidi vya funzo. Ikiwa unaona kwamba unaweza kukazia fikira vizuri zaidi saa za asubuhi, unaweza kuamua kujifunza kadiri fulani kabla ya kiamsha-kinywa. Ikiwa unakuwa chonjo zaidi wakati wa jioni, unaweza kuchagua kujifunza usiku kabla ya kwenda kulala. Kwa vyovyote vile, jambo la maana ni kuwa wa kawaida na kushikilia kawaida inayofaa zaidi mahitaji yako.
5 Tunapotiwa moyo tufanye funzo la kibinafsi zaidi, huenda tukawa wepesi kuonyesha kwamba tayari tuna ratiba yenye shughuli nyingi. Hata hivyo, sisi sote twahitaji kuwa wafuatiaji wa haki katika kuchanganua jinsi tunavyotumia wakati wetu. Je, saa nyingi zatumika kila siku kwa kutazama vipindi vya televisheni? Je, tuko tayari kudhabihu baadhi ya mapendezi ya kibinafsi? Uchunguzi wa kweli wa jinsi tunavyotumia wakati wetu yamkini utaonyesha vipindi vya kila siku ambavyo vyaweza kutumiwa kwa faida zaidi katika funzo la kibinafsi.—Efe. 5:15, 16.
6 Funzo la Neno la Mungu lastahili uangalifu wetu usiogawanyika. Kujaribu kufanya jambo jinginelo wakati uleule hupunguza manufaa hizo. Ikiwa twaelekea kujifunza huku tukila, tukisikiliza redio, au tukitazama televisheni, yamkini hatutajiingiza kabisa katika yale tunayojaribu kujifunza. (1 Tim. 4:15) Kwa hiyo kuna uhitaji wa kuondoa vikengeusha-fikira.—Ona kitabu Kiongozi cha Shule, kurasa 33-34.
7 Funzo la kila siku na kutumia shauri la Biblia ni muhimu kwa sababu hiyo ndiyo njia tunayopokea mwongozo kutoka kwa Yehova. Fanya uwe mradi wako kutoa kweli kutoka katika ukurasa uliochapwa uiingize moyoni mwako. Tumia kwa manufaa kila fursa, hata iwe fupi jinsi gani, ili usome, upitie, au utafakari mambo ya kiroho.—Kum. 6:6-8; Kol. 1:9, 10.