Fanyeni Yote kwa Utukufu wa Mungu
1 Inaburudisha kama nini kushirikiana na ndugu na dada zetu wapendwa! (1 Kor. 16:17, 18) Twafanya hivyo kwenye mikutano, kwenye makusanyiko, kwenye mikusanyiko, na katika huduma ya shambani. Twashirikiana pia katika pindi nyinginezo, kama vile tunapoalika wageni watutembelee nyumbani kwetu. Tukifanya hivyo, twaonyesha ukaribishaji-wageni na twatiana moyo. (Rum. 12:13; 1 Pet. 4:9) Mnapopanga karamu za arusi, kumbukeni lile shauri zuri katika Mnara wa Mlinzi la Septemba 15, 1984.
2 Vikusanyiko vya Kijamii Vilivyopangwa Vizuri: ‘Tulapo, au tunywapo, au tutendapo neno lolote,’ twapaswa ‘kufanya yote kwa utukufu wa Mungu.’ (1 Kor. 10:31-33) Shauri hili halifuatwi na wengine, na matatizo yaendelea kutokea kwa sababu ya vikusanyiko vya kijamii vilivyo vikubwa mno kuweza kusimamiwa ifaavyo. Katika pindi nyingine, mamia ya watu wanaalikwa kwenye sherehe zenye madoido ambazo katika hizo vitumbuizo vya kilimwengu vinaonyeshwa. Nyakati nyingine wale wanaohudhuria wanaombwa kulipa fedha ili kuingia au kwa sababu nyinginezo. Vikusanyiko vya jinsi hiyo vyafanana sana na vile vya kilimwengu, ambao roho yao haipatani na adabu nzuri na kanuni za Biblia.—Rum. 13:13, 14; Efe. 5:15-20.
3 Imeripotiwa kwamba idadi kubwa za Mashahidi wamekusanyika kwenye majengo yaliyokodiwa ambako vitumbuizo si vyenye kujenga na ni vya kilimwengu na ambako usimamizi ufaao unakosekana. Utendaji kama huo ambao umetangazwa kuwa mwisho-juma wa “Mashahidi wa Yehova” umefanywa kwenye hoteli au mahali mbalimbali pa tafrija. Kwa sababu ya ugumu katika kusimamia vikundi hivyo vikubwa, matatizo yametokea. Kufanya makelele, kunywa vinywaji vya alkoholi kupita kiasi, na hata ukosefu wa adili umekuwa tokeo nyakati nyingine. (Efe. 5:3, 4) Vikusanyiko vya kijamii vilivyo na mwenendo wa jinsi hiyo havimheshimu Yehova. Badala ya hivyo, vinaleta suto juu ya jina zuri la kutaniko na kuwakwaza wengine.—1 Kor. 10:23, 24, 29.
4 Wakristo wanatiwa moyo kuonyesha ukaribishaji-wageni, lakini jambo linalopaswa kukaziwa ni lile badilishano la kiroho. (Rum. 1:11, 12) Kwa kawaida vikusanyiko vidogo ni bora zaidi. Kitabu Huduma Yetu chasema hivi kwenye kurasa 135-136: “Huenda nyakati fulani jamaa fulani zikakaribishwa kwenye nyumba ili kufurahia ushirika wa Kikristo. . . . Kwa busara, wale ambao ndio wenye kukaribisha wageni katika visa hivyo wamepaswa waone wenyewe binafsi kuwa wana daraka la mambo yanayotendeka. Kwa kukumbuka hayo, Wakristo wenye busara wameona hekima ya kupunguza ukubwa wa vikundi hivyo na muda ambao vikusanyiko hivyo vinaendelea.” Yesu alionyesha kwamba jambo lolote lenye madoido halihitajiwi wakati mradi wetu unapokuwa kuwatia moyo marafiki wetu kiroho.—Luka 10:40-42.
5 Ni jambo zuri kuonyesha ukaribishaji-wageni kwa Wakristo wenzetu. Hata hivyo, kuna tofauti kubwa kati ya kikusanyiko chenye kiasi katika nyumba yetu na kikusanyiko chenye madoido kinachoonyesha roho ya kilimwengu katika jengo lililokodiwa. Unapoalika wengine kuwa wageni wako, wewe wapaswa kuhakikisha kwamba waweza kuchukua daraka kamili kwa yale yanayotendeka.—Ona Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 1992, kurasa 17-20.
6 Kwa kweli, Yehova ametubariki kwa kutupa sisi udugu ambao kutoka kwao twaweza kupata kitia-moyo chenye kuburudisha kinachotuchochea tuendelee katika kazi nzuri. (Mt. 5:16; 1 Pet. 2:12) Kwa kuonyesha kiasi na busara katika utendaji mbalimbali wa kijamii, sikuzote sisi tutamletea Mungu wetu utukufu na kuwa wenye kujenga wengine.—Rum. 15:2.