‘Uone Mema kwa Sababu ya Kazi Yako’
“Tazama, mimi niliyoyaona kuwa ndiyo mema na ya kufaa, ni mtu kula na kunywa, na kujiburudisha kwa mema katika kazi yake yote.”—Mhu. 5:18.
1. Kama inavyoonyeshwa katika 1 Timotheo 1:11, Yehova ni Mungu wa aina gani, na kwa hiyo tuna haki ya kukata maneno kwamba anataka viumbe vyake vyenye akili vifanye nini? (Kum. 12:18; 26:11; Zab. 32:11)
MUNGU Aliye Juu Zaidi, Yehova, ni mwenye furaha isiyo na kifani, naye anapendezwa na ukamilifu wake na kazi zake. (1 Tim. 1:11) Zaidi ya hilo, yeye anataka viumbe vyake vyenye akili viwe na furaha iyo hiyo, hasa watumishi wake waaminifu.
2. Mambo tunayohisi kwa akili zetu yanaonyeshaje kwamba Yehova ‘ametupa vitu vyote kwa wingi ili tuvitumie kwa furaha’?
2 Naam, akili tulizo nazo zimekusudiwa kuhisi (kufahamu) maono, sauti, harufu, ladha na maumbo mengi ajabu. Weee! jinsi inavyoweza kuwa furaha kuona jua likishuka kwa njia adhimu, kuona mbingu zilizotapakaa mapambo ya nyota, mito yenye kupinda-pinda, maziwa ya maji yaliyotulia vizuri, maporomoko ya maji yenye kupomoka-pomoka kwa utaratibu, pwani zenye michikichi, makonde yenye majani mabichi-mabichi na milima iliyofunikwa na theluji! Loo! ni ladha nzuri namna gani inayoweza kupatikana katika matunda yaliyotundwa karibuni, katika vyakula vyenye kuongeza afya na tamutamu za kufungia kinywa! Tunafurahi tunapojisikia tukipigwa na upepo mzuri katika siku yenye joto, na hasa tunapoguswa au kukumbatiwa na wapendwa wetu. Na je! si jambo la kupendeza kusikiliza vijito vikibubujika, mawimbi yakiipiga pwani kwa mshindo, majani ya mimea yakiimbishwa na upepo, ndege wakitoa vikelele na kuimba, na watoto wenye furaha wakicheka? Weee! jinsi tunavyoweza kufurahia kutembea katika mwitu au bustani nzuri, huku tukinusa harufu ya maua yenye kunukia vizuri! Hakika lazima tukubaliane na mtume Paulo aliyeongozwa na Mungu kusema kwamba Mungu ‘anatupa vitu vyote kwa wingi ili tuvitumie kwa furaha.’—1 Tim. 6:17.
3. Biblia inasema Mungu ana maoni gani juu yetu tunapofurahia vyakula na vinywaji?
3 Kwa wazi Mungu anakusudia tufurahie vitu ambavyo amekirimia sana wanadamu. (Matendo 14:16,17) Ndivyo Mfalme Sulemani mwenye hekima alivyokata maneno baada ya kuchunguza sana mambo ya kidunia. Alisema: “Tazama, mimi niliyoyaona kuwa ndiyo mema na ya kufaa, ni mtu kula na kunywa, na kujiburudisha kwa mema katika kazi yake yote.”—Mhu. 5:18.
4. Mfano wa Yesu Kristo unaonyeshaje kwamba inafaa Wakristo wafurahie vitu?
4 Hakika watumishi wa Yehova wanapaswa kufurahi. Yesu Kristo, kichwa cha kundi la Kikristo, aliweka mfano ulio bora juu ya kufurahia vitu. Yeye hakuwa kamwe mtu wa kujinyima hata vitu vilivyo vizuri akitaka kujionyesha utawa wake. Alipokaribishwa vyakulani na karamuni alikubali. (Luka 5:29; 7:36; 14:1; 19:5, 6) Mwujiza wa kwanza aliofanya, yaani, kugeuza maji yakawa divai bora, uliongeza furaha katika karamu ya arusi. (Yohana 2:1-11) Wengine waliona kwamba Yesu alikosa kuwa na kiasi kwa kufanya hivyo, kwa hiyo wakamshtakia uongo wakisema: “Mlafi huyu, na mlevi”! (Mt. 11:19) Walishindwa kujua kwamba Yesu Kristo alikuwa anatumia vizuri mipango tele ya Baba yake, huku akitanguliza mambo ya kiroho nyakati zote.—Mt. 6:24-34.
UWE NA MAONI YA KIASI JUU YA ANASA
5. Kulingana na unabii wa Biblia, wenye kupenda anasa wangepatikana kati ya nani “siku za mwisho,” na kwa sababu gani jambo hilo linaletea watumishi waaminifu wa Yehova hatari?
5 Kwa hiyo, ingawa watumishi wa Mungu wana haki ya kufurahia vyakula na vinywaji, na vilevile tafrija za namna mbalimbali, inawapasa waepuke mitego fulani. Kulingana na Biblia, kati ya wenye kujiita Wakristo ndipo wangepatikana “wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu” katika “siku za mwisho.” (2 Tim. 3:4) Watu hao wangeanza kuishi kwa ajili ya anasa, kutanguliza mambo yenye kuwafurahisha maishani mwao. Kwa kuwa watumishi waaminifu wa Yehova wanakabiliwa leo na maongozi yenye nguvu ya watafutaji wa anasa, lazima wajihadhari yasije yakaanza kuharibu mawazo yao.
6, 7. (a) Mfalme Sulemani alikataje maneno kwa njia nzuri kuhusu shangwe na kicheko? (b) Inatupasa tuyaeleweje hasa maneno ya Sulemani?
6 Tunaweza kusaidiwa sana na maoni ya kiasi juu ya anasa yaliyotolewa na Mfalme Sulemani. Anaeleza aliyoona baada ya kufanya uchunguzi: “Nikauambia moyo wangu, Haya, nitakujaribu kwa njia ya furaha; basi ujifurahishe kwa anasa. Na tazama, hayo nayo yakawa ubatili. Nikasema juu ya kicheko, Ni wazimu; na juu ya furaha, Yafaa nini?”—Mhu. 2:1, 2.
7 Sulemani anatuonyesha nini hasa? Maneno yake yanaonyesha wazi kwamba mtu hawezi kupata furaha ya kweli na yenye kudumu kwa kutafuta vitu vya kumfurahisha akiwa na pupa. Aliona kwamba kufurahi au kufanya macheko bila kusudi ni “ubatili,” kazi bure. Hiyo ni kwa sababu ‘kufurahi’ bila kusudi hakuwezi kuleta jambo lenye faida. Ni kweli kwamba mambo yenye kufurahisha na kicheko yanaweza kusaidia mtu asahau matatizo yake kwa muda. Lakini matatizo hayo hayatakwisha baada ya kipindi hicho chenye shangwe, bali mtu atalazimika kuyakabili. Tena, wakati mtu anapojiondolea matatizo mazito sana kwa kucheka kipumbavu, huyo hatumii akili na huenda akachukiza watu. Ndiyo sababu kicheko chake kinaweza kuitwa “wazimu.” “Kufurahi” au macheko ya mtu mwenye kucheza-cheza nyakati zote ni kazi bure. Ni kama Sulemani alivyouliza, “Yafaa nini?” Naam, macheko hayo yanaleta faida gani?
8. Tunaweza kusaidiaje tukiIitumia somo linaloweze Kupatikana katika uchunguzi wa Sulemani?
8 Tukijiacha tuongozwe na mambo aliyoona Sulemani baada ya uchunguzi wake, hakika hatutaruhusu anasa zisonge utendaji wetu wa kiroho. Basi inatupasa tuhudhurie karamu kwa kiasi na kutumia wakati kwa kiasi karamuni. Tukiwa na mazoea ya kukaa katika karamu mpaka usiku unapoingia sana, tunawezaje kuwa macho kesho yake ili kutimiza mambo ya kiroho, kama kuhudhuria mikutano ya kundi au kutolea watu ushuhuda? Mtu akichoka sana asiweze kutimiza utendaji wa kiroho kwa sababu ya kufanya tafrija mpaka usiku unapoingia sana, je! mambo ya kufurahisha hayawi yameanza kuruka mpaka? Ingawa tuna haki ya kufurahia karamu na tafrija za namna nyingine, zisiwe ndiyo mambo ya maana zaidi maishani mwetu. Inatupasa tuendelee kutosheka hasa na maisha yanayotegemea kumtumikia Yehova Mungu kwa uaminifu.
9. Huenda ikawapasa Wakristo ambao kwa kawaida hawachezi wajiangalie wasifanye nini?
9 Kwa upande mwingine, kwa kuwa inafaa wakati fulani watumishi wa Mungu wafurahi na kucheka, Wakristo ambao kwa kawaida si watu wa kucheza na hawapendezwi sana na tafrija za namna fulani wasiwadharau wala kulaumu waamini wenzao wanaofurahia michezo, dansi au mambo mengine kwa njia nzuri. (Rum. 14:10-12) Biblia inatushauri hivi: “Usiwe na haki kupita kiasi.” (Mhu. 7:16) Kwa hiyo, inampasa mtu ajiangalie asije akahangaikia mambo kupita kiasi na kutokeza matata makubwa juu ya mambo yasiyomhusu. Kuwa mwenye haki kupita kiasi kwa njia hiyo kunaweza kumfanya awe na juhudi ya kujipeleka mbele mno na hata kuonyesha ukatili na ukosefu wa upendo kiasi cha kupoteza upendeleo na baraka za Mungu.
LAZIMA ANASA ZIANGALIWE
10. Ni matatizo gani yaliyotokea katika ‘karamu za upendo’ zilizofanywa na Wakristo wa kwanza?
10 Ni wazi kwamba lazima anasa ziangaliwe yasije yakatokea matatizo makubwa. Wakristo wa karne ya kwanza walipaswa kuangalia sana jambo hilo katika ‘karamu zao za upendo,’ ambako inaonekana hata Wakristo maskini wangeweza kufurahia chakula na ushirika wenye kuwajenga. Lakini linalosikitisha ni kwamba, watu wasio na maoni ya kiroho walitumia nyakati hizo kutosheleza tamaa zao za kichoyo. Ndiyo sababu mwanafunzi Mkristo Yuda alitaja watu fulani kuwa “miamba iliyofichwa chini ya maji katika karamu zenu za upendo.” (Yuda 12, NW) Mtu angeweza kuvunjiwa imani yake kwa kushirikiana na watu hao wenye makusudi mabaya. Vivyo hivyo, mtume Petro aliandika hivi: “Wanafikiri maisha ya anasa wakati wa mchana ni raha. Wao ni madoa na mawaa, wakijitia katika mafundisho yao ya uongo kwa furaha isiyozuiwa na huku wakifanya karamu pamoja nanyi.” (2 Pet. 2:13, NW) Kusudi la pekee la watu hao lilikuwa kutosheleza nyege na tamaa zao mchana na usiku. Walijisingizia kuwa Wakristo, wakaendesha mazoea mabaya ya ulimwengu uliotenganishwa na Mungu bila kuona aibu. Walikuwa kama madoa na mawaa, wakaharibu sifa nzuri ya Wakristo waaminifu, wakaletea jina takatifu la Mungu malawama mengi. Kwa kutamka “mafundisho yao ya uongo,” maoni yao mapotovu, inaonekana walifaulu kuharibu vikusanyiko vizuri vya Kikristo vikawa vyenye makelele na mchafuko wa anasa.
11. Ni mambo gani ambayo lazima yaondolewe mbali katika vikusanyiko vya kujifurahisha vinavyofanywa na watu wa Mungu?
11 Jambo hilo linawapa watumishi wa Mungu leo somo la maana sana. Ni vizuri Wakristo wakiweza kukutana na kufurahia ushirika, vyakula na vinywaji kwa kiasi. Lakini uulimwengu lazima uondolewe mbali katika vikusanyiko hivyo ili viwe vyenye kujenga watu kiroho. Kikusanyiko kinakuwa kikusanyiko gani ikiwa watu wanajijaza vileo bila kujizuia, ikiwa muziki unadunda-dunda mpaka kunakaribia kupambazuka na ikiwa watu wanacheza dansi zisizo za adabu? Hata watu fulani wakijaribu kutetea sana kikusanyiko cha namna hiyo, bado hiyo ni karamu ya kilimwengu, karamu ya ulevi.
12. Inawapasa Wakristo wawe na maoni gani juu ya shangwe zisizo na kiasi?
12 Wakristo wa kweli walikwisha shiba shangwe zisizo na kiasi wakati walipokuwa hawajui mapenzi wala kusudi la Mungu. Wao hawataki kuwa katika kipindi ambacho watu wanakunywa kupindukia, kisicho na utaratibu na chenye nyege, wala hawataki kuwa katika kikusanyiko ambamo lo lote la mambo hayo linapatikana au watu wanakaribia kulifanya. Kwa kuwa sasa wameelimishwa, wanathamini shauri hili la Maandiko: “Kama ilivyohusika na mchana na tuenende kwa adabu; si kwa ulafi na ulevi, si kwa ufisadi na uasherati, si kwa ugomvi na wivu.” (Rum. 13:13) “Maana wakati wa maisha yetu uliopita watosha kwa kutenda mapenzi ya Mataifa; kuenenda katika ufisadi, na tamaa, na ulevi, na karamu za ulafi, na vileo, na ibada ya sanamu isiyo halali.”—1 Pet. 4:3.
13, 14. Kama inavyoonekana katika Wagalatia 5:21 na Isaya 5:11, 12, kwa sababu gani watafutaji wa anasa wamo katika hatari kubwa?
13 Hilo si jambo la mchezo hata kidogo. Watu wanaohusika katika karamu za ulevi wanatajwa katika Maandiko kuwa kati ya wale ambao “hawataurithi ufalme wa Mungu.” (Gal. 5:21) Kwa hiyo, watu wanaoanza kuishi kwa ajili ya anasa tu wamo katika hatari kubwa. Jambo hilo linakaziwa sana kwa habari ya Waisraeli fulani walioishi wakati wa Isaya. Walijijaza sana divai katika karamu zao. Usiku ulipoendelea kuingia, walevi hao walikuwa wakizidisha makelele. Karamu yao yenye makelele ilikuwa na muziki uliokusudiwa kuamsha nyege zao. Kwa hiyo, Yehova alimtumia nabii wake Isaya kuwaambia maneno haya: “Ole wao waamkao asubuhi na mapema, wapate kufuata kileo; wakishinda sana hata usiku wa manane mpaka mvinyo imewaka kama moto ndani yao! Na kinubi, na zeze, na matari, na filimbi, na mvinyo, zote ziko katika karamu zao; lakini hawaiangalii kazi ya [Yehova] wala kuyafikiri matendo ya mikono yake.”—Isa. 5:11, 12.
14 Ni vizuri kwamba watafutaji hao wa anasa wangepatwa na ole au mabaya. Wao hawakufikiria kumpendeza Muumba. Lengo lao la pekee lilikuwa kutosheleza tamaa zao za kimwili tangu asubuhi. Hakuna tofauti leo. Watu wanaofanya ulevi bila kujizuia hawayafikirii matendo ya Yehova.’ Mtu anawezaje kuyafikiria matendo makuu ya Yehova kukiwa na muziki wenye kuamsha tamaa zake huku yeye akila na kunywa kupindukia? Kama anavyoeleza Isaya, wakati watafutaji wa anasa wanapoendelea na anasa zao, wanatenda mambo kama kwamba hakuna ushuhuda wa kuonyesha kwamba kuna Aliye Juu Zaidi na kwamba amekuwa na utendaji wake. Kwa hiyo, kama ilivyokuwa wakati wa nabii, leo wanaofanya karamu za ulevi bila kutubu wanakataliwa na Yehova Mungu.
15. Yesu alitoaje onyo juu ya hatari ya kuanza kuishi maisha ya anasa?
15 Tunastahili kuangalia kwamba Yesu Kristo alionya wanafunzi wake juu ya hatari kubwa ya kuwa watafutaji anasa, akawaamuru hivi: “Jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi.” (Luka 21:34) Kula na kunywa kupindukia kunaweza kulemea moyo ujisikie ukiwa na hatia na kuumalizia tamaa yo yote ya mambo ya kiroho. Ikitukia hivyo, huenda mtu akasinzia kiroho, akaacha kuona wajibu unaompasa kutimiza anapokuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo. Akiendelea kuwa katika hali hiyo, Mwana wa Mungu atakuja kuleta kisasi cha kimungu na kumnasa kama “mtego” unasavyo. Yesu alionya kwamba: “Ndivyo itakavyowajilia watu wote wakaao juu ya uso wa dunia nzima. Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika hayo yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu.” (Luka 21:35, 36) Hakika “siku za mwisho” sio wakati wa mtu ye yote kuyapuza maneno haya na kuingia katika mazoea ya kilimwengu katika karamu.
JINSI YA KUZUIA MATATIZO
16. Je! washiriki wote wa kundi la Kikristo ni washirika wazuri kwa sababu tu wanashirikiana na kundi?
16 Mtu anawezaje kuzuia karamu zisiwe za kilimwengu, zisije zikaharibu hali ya kiroho na kukataliwa na Mungu? Lazima afikiri ahakikishe kwamba waliokaribishwa hawataleta maongozi yasiyofaa. Katika barua aliyomwandikia Timotheo, mtume Paulo alionyesha kwamba, ingawa watu wanashirikiana na kundi la Kikristo, hiyo tu haionyeshi kwamba wote ni washiriki wazuri. Aliandika akasema: “Basi katika nyumba kubwa havimo vyombo vya dhahabu na fedha tu, bali na vya mti, na vya udongo; vingine vina heshima, vingine havina. Basi ikiwa mtu amejitakasa kwa kujitenga na hao, atakuwa chombo cha kupata heshima, kilichosafishwa, kimfaacho Bwana, kimetengenezwa kwa kila kazi iliyo njema. Lakini zikimbie tamaa za ujanani; ukafuate haki, na imani, na upendo, na amani, pamoja na wale wamwitao Bwana kwa moyo safi.”—2 Tim. 2:20-22.
17. Inawapasa Wakristo wasishirikiane na watu gani wa kundi katika mambo ya kujifurahisha, na kwa sababu gani? (2 The. 3:6-15)
17 Kwa hiyo, Wakristo wana wajibu wa kujiepusha na wale walio na mwenendo unaotiliwa sana mashaka. Si lazima wakaribishe katika karamu zao watu wenye sifa ya kutozuia usemi wao au wanaofanya mambo ya kupita kiasi. Kwa kweli, kukaribisha watu wa namna hiyo si kuwasaidia. Badala ya kuwatia moyo wabadilike, huenda wakakata maneno kwamba kundi la Kikristo linakubali maneno na matendo yao yasiyofaa.
18. (a) Ni nini kinachopasa kiongoze watumishi wa Mungu katika utendaji wao wote? (b) Ni mambo gani ambayo kwa kawaida yanasaidia kikusanyiko cha Wakristo kiwe chenye kuwajenga?
18 Wakati wo wote watumishi wa Mungu wanapofurahia kushirikiana, inawapasa wakumbuke onyo la upole la Biblia linalosema: “Mlapo, au mnywapo, au mtendapo neno lo lote, fanyeni yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Kor. 10:31) Tunaweza kujiuliza ulizo hili, Je! kipindi hiki kweli kinamletea Yehova Mungu sifa? Kwa kawaida watu wote wanaweza kufurahia ushirika wenye kuwajenga wakati karamu zinapokuwa na watu wachache kiasi, wakati wenye kukaribishwa wanapochaguliwa kwa uangalifu na wakati mkaribishaji Mkristo anapokubali kuwa na wajibu wa jambo lo lote litakalotokea. Kwa mfano, kundi zima likifurahia mandari (pikniki) pamoja, ingewapasa wazee watumie maongozi yao kwa njia yenye faida. Bila shaka, watu wo wote tu wasio wa kundi hilo wakiletwa karamuni, ni vigumu na labda hata haiwezekani wazee waangalie vizuri watu waliokusanyika. Kwa hiyo watu wo wote wanaopanga karamu wakumbuke jambo hilo na kuepuka hali zinazoweza kufanya watu wasisimamiwe vizuri.
19. Tunaweza kutumia kanuni gani katika Luka 14:13, 14 na Mathayo 6:3 kwa habari ya vikusanyiko vya kujifurahisha (karamu)?
19 Inampasa pia Mkristo akumbuke ubora wa kutokaribisha nyakati zote watu wale wale wachache waje kufurahia naye matunda ya kazi yake. Huenda wakawako waamini wenzake ambao wangefurahi sana na kufaidika kutokana na ushirika mzuri—kwa mfano, wazee wa umri na wajane. Yesu Kristo alipendekeza hivi: “Ufanyapo karamu, waite maskini, vilema, viwete, vipofu, nawe utakuwa heri, kwa kuwa hao hawana cha kukulipa.” (Luka 14:13, 14) Mtu asingekuwa akifuata pendekezo hilo akipanga karamu zenye utapanyaji mwingi kiasi cha kutaka waliokaribishwa walipe pesa za kusaidia gharama, labda hata ajipatie faida. Tena, karamu kubwa mno inaweza kufanya watu wamfikirie kupita kiasi mwenye kuipanga, na hicho kingekuwa kinyume cha roho aliyoshauri Yesu aliposema ‘mkono wetu wa kushoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume.’—Mt. 6:3.
20. Kunaweza kuwa na faida gani kwa kutumia kanuni za Biblia katika vikusanyiko vya kujifurahisha (karamu)? (2 Pet. 3:11-14)
20 Kwa kweli, mashauri ya Maandiko yafuatwapo, watumishi wa Yehova Mungu wanaweza kufurahia matunda ya kazi yao na kukaribisha wenzao wafurahi pamoja nao. Wakifuata mashauri hayo wataendelea kukesha kiroho, kuepuka uulimwengu wote. Hapo ndipo karamu zao zinapoweza kumletea utukufu Mungu mwenye furaha, Yehova, na kufanya watazamaji wanyofu waseme: “Mungu yu kati yenu bila shaka.” (1 Kor. 14:25) Zaidi ya hilo, wataendelea kuwa na ukubali wa Mungu na Kristo, huku wakiutazamia sana wakati ambao “Bwana MUNGU atapangusa machozi toka nyuso zote” na ‘kufanyia mataifa yote karamu ya vitu vya kunona vilivojaa mafuta’—ili wawe na furaha ya kiasi pamoja na mipango mingine yote ya upendo iliyo katika uumbaji wa Mungu.—Isa. 25:6-8, ZSB.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Je! kujifurahisha bila kiasi kutajenga watu?
[Picha katika ukurasa wa 9]
Au, inafaa zaidi utafute kujifurahisha vizuri pamoja na jamaa?