Sanduku La Swali
◼ Ni jambo gani ambalo lapaswa kukumbukwa kuhusu kusoma mafungu kwenye mikutano?
Wakati mwingi unaotolewa kwa ajili ya Funzo la Mnara wa Mlinzi na Funzo la Kitabu la Kutaniko hutumiwa kwa usomaji wa mafungu. Hili humaanisha kwamba ndugu aliyegawiwa kuwa msomaji huwa na daraka zito akiwa mwalimu. Lazima asome kwa njia ‘itiayo maana’ katika habari ili wasikilizaji wasiielewe tu bali pia iwachochee kutenda. (Neh. 8:8) Kwa sababu hiyo, msomaji ahitaji kutayarisha vizuri mgawo wake. (1 Tim. 4:13; ona somo la 6 la kitabu Kiongozi cha Shule.) Haya ni baadhi ya mambo ya lazima kwa usomaji wenye maana mbele ya watu wote.
Tumia Mkazo wa Maana Unaofaa: Chunguza mapema maneno au misemo inayohitaji kukaziwa ili kutoa uelewevu sahihi.
Tamka Maneno kwa Usahihi: Utamkaji unaofaa na unenaji ulio wazi ni wa lazima ikiwa wasikilizaji wataelewa misemo iliyo katika kichapo. Angalia katika kamusi maneno yasiyofahamika au yatumiwayo mara chache, au usikilize mirekodio ya kaseti za Sosaiti.
Sema kwa Sauti na Idili: Kusema kwa sauti ya juu kwa idili hutokeza upendezi, husisimua hisia-moyo, na kuchochea msikilizaji.
Uwe Mchangamfu na Mwenye Hali ya Kuongea: Uasilia hutokana na ufasaha. Kwa utayarishaji na mazoezi, msomaji aweza kustarehe, na tokeo litakuwa lenye kupendeza badala ya kuwa la namna moja tu na lenye kuchosha.—Hab. 2:2.
Soma Habari Kama Ilivyochapwa: Vielezi-chini pamoja na habari zilizo kwenye mabano-duara au braketi kwa kawaida husomwa kwa sauti ikiwa yanaelewesha habari iliyochapishwa. Isipokuwa tu marejezeo yanayotambulisha chanzo cha habari. Kielezi-chini chapaswa kusomwa wakati ambapo kimerejezewa katika fungu, kwa utangulizi wa kusema: “Kielezi-chini chasema . . .” Baada ya kukisoma, endelea tu kusoma sehemu inayobaki ya fungu.
Usomaji wa mbele ya watu wote unapofanywa vema, ni mojapo njia muhimu tuwezayo ‘kuwafundisha wengine kuyashika yote yaliyoamriwa’ na Mfundishaji Mkuu wetu.—Mt. 28:20.