Stahi Mahali pa Ibada pa Yehova
1 Tunapokuwa wageni nyumbani kwa mtu fulani, twastahi mali ya mtu huyo, bila kufanya chochote kuiharibu, na hatuvurugi kawaida yenye utaratibu ya hiyo nyumba. Lapaswa kuwa hivyo hata zaidi kama nini tunapokuwa wageni-waalikwa wa Yehova! Twapaswa kujua jinsi ya kujiendesha wenyewe katika nyumba yake. (Zab. 15:1; 1 Tim. 3:15) Iwe mkutano wetu wa Kikristo wafanyiwa katika Jumba la Ufalme, makao ya kibinafsi, au jengo la watu wote, walio wengi kati yetu hustahi sikuzote mahali pa ibada kana kwamba ni nyumba ya Yehova, ambaye “adhama yake i juu ya nchi na mbingu.”—Zab. 148:13.
2 Ndugu wengine huonyesha ukosefu wa staha kwenye mikutano kwa kuwa wenye kelele au kutenda kana kwamba habari inayotolewa haina umaana. Watu wazima wachache huendelea na maongezi yasiyohitajika ukumbini, sebuleni, vyooni, au nje ya Jumba la Ufalme mikutano inapoendelea. Mtoto mwenye umri mkubwa zaidi ya mwingine aachwapo kumsimamia yule mchanga zaidi, nyakati nyingine wote wawili huanza kucheza na hukosa manufaa nyingi kutokana na programu. Vijana fulani wamekuwa wakionekana nje ya Jumba la Ufalme baada ya mikutano, wakicheza, wakipiga kelele kupita kiasi, hata wakifanya kana kwamba wanapigana karate. Katika visa fulani wamesumbua majirani au kuzuia mwendo wa magari kwenye maegesho au barabarani.
3 Jinsi ya Kuepuka Kuwa Wasio na Staha: Tukifahamu adhama na utakatifu wa ibada yetu, bila shaka hatutataka kukengeusha wengine kwa kunong’ona, kula, kutafuna chingamu, kupepesua makaratasi, kwenda msalani isivyo lazima, au kuwa na mazoea ya kuchelewa kufika mikutanoni. Wazazi wenye staha na uthamini hawaruhusu watoto wao wachafue zulia, matakia, au kuta za Jumba la Ufalme au makao ambamo funzo la kitabu hufanyiwa. Na bila shaka sisi sote twakubali hakika kwamba haifai kuwa na mwenendo wowote wa aibu, maongezi ya kipumbavu, au mzaha wenye aibu kwenye mikutano yetu.—Efe. 5:4.
4 Sikuzote tukikumbuka kusudi la mikutano yetu ya Kikristo, tutahakikisha kwamba sisi na watoto wetu twastahi istahilivyo mahali pa ibada pa Yehova ambapo “tumechagua kusimama.”—Zab. 84:10, NW.