Je! Wewe Hustahi Mahali Pako pa Ibada?
“Tangu mwanzo kabisa wa gospeli, Wakristo sikuzote walikuwa na mahali pao imara na thabiti pa ibada ya kimungu.” —“Primitive Christianity,” cha William Cave.
WATU wa Mungu wamefurahia sikuzote kukusanyika pamoja kwa ajili ya ibada. Hilo lilikuwa kweli katika karne ya kwanza jinsi lilivyo kweli sasa. Watungaji vitabu na wanatheolojia wa mapema, kama vile Lucian, Clement, Justin Martyr, na Tertullian, wote wanakubaliana kwamba Wakristo walikuwa na mahali hususa walipokusanyika ili kuabudu pamoja kwa ukawaida.
Biblia huthibitisha jambo lilo hilo, ikifanya marejezo mengi kwenye mikutano ya kawaida iliyofanywa na vikundi vya Wakristo. Vikundi hivyo viliitwa makundi. Hilo lilifaa kwa sababu neno “kundi” katika lugha za awali za Biblia humaanisha kikundi cha watu waliokusanyika pamoja kwa kusudi au utendaji mahususi.
Mahali-Mahali pa Mapema pa Ibada ya Kikristo
Wakristo wa karne ya kwanza walifanya nini walipokusanyika pamoja? Biblia yasimulia idadi fulani ya mikutano ya jinsi hiyo na yaonyesha kwamba kufundisha kulikuwa ndilo jambo kuu. (Matendo 2:42; 11:26; 1 Wakorintho 14:19, 26) Programu za kielimu zilipangwa, pamoja na hotuba, masimulizi ya maono yenye kutia moyo, na uchunguzi wenye uangalifu wa barua zilizopokewa kutoka kwa baraza lililoongoza katika Yerusalemu au kutoka kwa mtume fulani.
Kwenye Matendo 15:22-35, twasoma kwamba baada ya barua moja ya jinsi hiyo kusomwa kwa kikundi kimoja cha Wakristo katika Antiokia, Yuda na Sila “wakawausia ndugu kwa maneno mengi, wakawathibitisha.” Usimulizi mwingine wasema kwamba Paulo na Barnaba walipowasili Antiokia “wakalikutanisha kanisa [kundi, NW], wakawaeleza mambo yote aliyoyafanya Mungu pamoja nao.” Kusali kwa Yehova kulikuwa pia jambo la maana katika mikutano ya Kikristo.—Matendo 14:27.
Mahali ambapo makundi ya karne ya kwanza walikusanyika kwa ajili ya ibada hapakuwa majengo yenye madoido kama vile makanisa mengi ya Jumuiya ya Wakristo leo. Mara nyingi, Wakristo wa mapema walikutana katika nyumba za faragha. (Warumi 16:5; 1 Wakorintho 16:19; Wakolosai 4:15; Filemoni 2) Mara nyingi kichumba cha paa au chumba cha orofa ya juu zaidi ya nyumba ya faragha ndicho kilitumiwa. Mlo wa Jioni wa Bwana ulifanywa katika chumba cha orofa ya juu zaidi. Wale wanafunzi 120 walipakwa kwa roho takatifu katika Pentekoste wakiwa katika chumba cha orofa ya juu zaidi pia.—Luka 22:11, 12, 19, 20; Matendo 1:13, 14; 2:1-4; 20:7, 9.
Leo Mashahidi wa Yehova hufuata kigezo kilichowekwa na mitume. Wao hutumia mahali pa kukutania panapoitwa Majumba ya Ufalme. Hapo wao huzoezwa kuwa wahubiri wa habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Kwenye Jumba la Ufalme, wao hujifunza pia Maandiko, husali, na kutiana moyo. Hilo lapatana na himizo hili la Biblia kwenye Waebrania 10:24, 25: “Tukaangaliane sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri; wala tusiache kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya wengine; bali tuonyane; na kuzidi kufanya hivyo, kwa kadiri mwonavyo siku ile kuwa inakaribia.”
Kutumia Mahali Petu pa Ibada Ifaavyo
Je! unakumbuka maneno haya ya mtume Paulo: “Mungu si Mungu wa machafuko, bali wa amani” na, “Mambo yote na yatendeke kwa uzuri na kwa utaratibu”? Ukichunguza muktadha wa maneno hayo, utagundua kwamba Paulo alikuwa akizungumzia njia ambayo mikutano ya Kikristo ilipasa kuongozwa. Kama vile katika enzi ya kimtume, Wakristo leo huhakikisha kwamba mikutano yao ni yenye utaratibu na yenye kupangwa vizuri.—1 Wakorintho 14:26-40.
Toleo la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 1969, (katika Kiingereza) lilisema hivi: “Hali ya kiroho kwenye Jumba la Ufalme ni ya kweli, ikitokana na kupendezwa kihalisi na ibada ya kweli na maagizo ya Kibiblia. Na yale mazingira myepesi, na ya asili katika jumba huwatia moyo wale waliopo wawe wenye kujitokeza na wenye urafiki, si wenye kuzuiwa na hali ya uchaji iliyowekwa kimafumbo.” Bila shaka, uangalifu huonyeshwa ili matumizi ya Jumba la Ufalme yaonyeshe sikuzote staha na fahari.
Jumuiya ya Wakristo imedhihirisha ukosefu mbaya sana wa staha katika jambo hilo. Baadhi ya matengenezo ya kidini hutumia mahali payo pa ibada kama vitovu vya kijumuiya kwa ajili ya vitumbuizo. Wanakuwa na maonyesho ya muziki wa roki wa kidini, mashindano ya kuinua uzani, michezo ya kuvingirisha mipira kwenye meza kwa mti, shule za watoto wachanga, na sinema. Kanisa moja lilikuwa na shindano la mwereka likiwa sehemu ya programu yalo. Hilo halipatani hata kidogo na kile kigezo kilichowekwa na mitume.
Ikiwa kundi lolote la karne ya kwanza lilitenda isivyofaa, usahihisho ulifaa. Kwa kielelezo, wengine katika kundi la Kikristo katika Korintho walikuwa wakitumia mwadhimisho wa Mlo wa Jioni wa Bwana ukiwa pindi ya kula na kunywa. Walikuwa wanaleta chakula chao cha jioni ili wale kabla au wakati wa mkutano, wengine hata wakila na kunywa kupita kiasi. Hilo halikufaa hata kidogo. Mtume Paulo aliwaandikia hivi: “Je! hamna nyumba za kulia na kunywea?”—1 Wakorintho 11:20-29.
Kwa kupatana na shauri la Paulo, Mashahidi wa Yehova hujitahidi kushughulikia mambo ya kibinafsi nyumbani au kwingineko kuliko kwenye Jumba la Ufalme. Ni kweli, mikutano yetu ya kawaida huandaa fursa ifaayo ya kuona marafiki kadhaa kwa wakati mmoja. Hata hivyo, Jumba la Ufalme limewekwa wakfu kwa Yehova, kwa hiyo linapasa kutumiwa hasa kwa ajili ya ibada yake. Sisi hatutumii kwa faida yetu hudhurio letu huko ili kufuatia biashara ya kilimwengu au kushughulikia shughuli za kifedha za kibinafsi.
Zaidi ya hayo, Majumba ya Ufalme hayatumiwi na kundi kwa ajili ya programu za kitafrija, utendaji wa kukusanya fedha, wala utumishi wa kijamii, kama vile utunzaji wa watoto. Kuna mahali penginepo ambapo mtu aweza kushughulikia mambo hayo ya kibinafsi na ya kibiashara.
Wazee katika Jumba la Ufalme moja waliona kwamba washiriki wa kundi walikuwa wakianza kuzoea kuazima au kurudisha vitu vilivyoazimwa kwenye mikutano. Pia, walikuwa kwa kawaida wakibadilishana sinema za vidio-kaseti kwenye Jumba la Ufalme. Ingawa utendaji huo haukuwa wa kibiashara, wazee waliwasaidia waone hekima ya kushughulikia mambo hayo nyumbani ilipowezekana.
Ili kuepuka hali ambazo zingeweza kutoa maoni yasiyofaa na kuhakikisha kwamba Jumba la Ufalme linatumiwa ifaavyo, kila mtu apaswa kujiuliza hivi: ‘Je! kuna mambo yoyote ya kibinafsi ambayo nimekuwa nikishughulikia kwenye Jumba la Ufalme ambayo yaweza kushughulikiwa nyumbani?’ Kwa kielelezo, unapopanga matembezi au vikusanyiko vingine vya kijamii, je, isingefaa zaidi kuzungumzia mipango hiyo nyumbani? Je! tungeweza kutumia simu au kutembelea nyumba za wale tunaotaka kuwasiliana nao? Kwa kuazima maneno ya Paulo, tungeweza kusema hivi: ‘Je! hatuna nyumba za kushughulikia mambo kama hayo?’
Wakati na Mahali Palipowekwa Ili Kumwabudu Yehova
Biblia yasema hivi kwenye Mhubiri 3:1: “Kwa kila jambo kuna majira yake [wakati uliowekwa, NW], na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu.” Tunapohudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme, twaweza kujihusisha kikamili katika utendaji mbalimbali unaohusiana na huduma ya Kikristo. Ni wakati uliowekwa wa kumwabudu Yehova.
Yakobo ndugu-nusu wa Yesu alitoa shauri dhidi ya kuonyesha upendeleo ndani ya kundi la Kikristo. (Yakobo 2:1-9) Tunaweza kutumiaje shauri hilo katika Majumba ya Ufalme yetu? Upendeleo ungeweza kuonekana wakati mialiko kwenye vikusanyiko vya kijamii inapopitishwa humo kwa wazi. Katika kundi moja desturi ilikuwa kuweka mialiko hiyo katika mikoba au Biblia za wale waliokuwapo. Ni kweli, hiyo ni njia iliyo rahisi zaidi kuliko kupeleka mialiko hiyo kwa posta au kuipeleka kwenye kila nyumba. Hata hivyo, wale ambao hawapokei mwaliko wanahisije baada ya kuona kwamba mialiko inapitishwa kwa wengine? Je! hilo lingeweza kuonyesha upendeleo?
Bila shaka, si lazima kuwe amri imara inayosema kwamba hakuna awezaye kumpa mwingine ujumbe au kifurushi cha kibinafsi kwenye Jumba la Ufalme; wala si jambo baya kuongea katika Jumba la Ufalme juu ya utendaji mbalimbali au matukio ya kila siku, kumwalika mtu fulani nyumbani mwako, au kumwomba mtu fulani aungane na wewe katika tafrija fulani. Lakini hilo lapasa liwe kwa tukio tu na kufanywa kwa njia yenye busara na isiyo ya wazi. Mipango ya kibinafsi haipasi kamwe kukengeusha fikira kutoka kwenye kusudi la kweli la kukusanyika kwetu kwenye Jumba la Ufalme, yaani, ili kuelimishwa kiroho.—Mathayo 6:33; Wafilipi 1:10.
Watu Wanaoweka Kielelezo
Wazee na watumishi wa huduma huweka kielelezo kwa bidii katika kuonyesha staha kwa Jumba la Ufalme. Kwa kawaida kuna mzee mmoja au wawili na watumishi wa huduma wanaopewa mgawo wa kuratibu mambo yanayohusu utunzaji wa Jumba la Ufalme. Mahali ambapo zaidi ya kundi moja linatumia jumba lilelile, halmashuri ya wazee husimamia mambo hayo.
Ingawa watu fulani wamepewa mgawo hususa wa kutunza wajibu huo mbalimbali, watumishi wa huduma na wazee wote wanapaswa kuonyesha kupendezwa kikweli na jumba. Wanatambua kwamba Jumba la Ufalme limewekwa wakfu kwa Yehova na hutumiwa kwa ajili ya ibada yake.
Wazee hawapaswi kukawia-kawia wakati marekebisho yanapohitaji kufanywa. (2 Mambo ya Nyakati 24:5, 13; 29:3; 34:8; Nehemia 10:39; 13:11) Katika baadhi ya makundi ukaguzi wa kawaida wa Jumba la Ufalme hufanywa ili kushughulika upesi na marekebisho yoyote yanayohitajiwa. Orodha zinawekwa ili kuhakikisha kwamba vifaa vinavyohitajiwa vyapatikana na vyafikika kwa urahisi. Ikiwa kuna mahali maalumu pa kuwekea vifaa, vyombo vya kufanyia kazi, na vyombo vya kusafishia, wazee na watumishi wa huduma wote wanapaswa kuonyesha kupendezwa na hali yavyo, wakihakikisha kwamba vyote vimewekwa kwa unadhifu. Wale wanaofanya kazi kwenye kaunta za fasihi na magazeti wanaweza kuonyesha kupendezwa kwao kwa kuhakikisha upesi kwamba makatoni matupu hayachafui jumba.
Kwa kuweka kielelezo kizuri, wazee na watumishi wa huduma wanaweza kuwasaidia wengine kundini wadhihirishe bidii kwa ajili ya Jumba la Ufalme. (Waebrania 13:7) Wote wanaweza kuonyesha staha kwa kushiriki sehemu fulani katika kusafisha jumba na kwa kuonyesha kupendezwa kikweli na sura yalo ya ujumla.
Yesu alisema hivi kwenye Mathayo 18:20: “Walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao.” Naam, Yesu anapendezwa na yale tunayofanya tunapokusanyika pamoja ili kumwabudu Yehova. Hilo latia ndani mikutano yoyote yanayofanywa kwenye nyumba za faragha na mikutano mikubwa kama vile mikusanyiko au makusanyiko.
Kwa mamilioni ya Mashahidi wa Yehova, hapana mahali palipo karibu zaidi na moyo wao kuliko mahali pao pa kawaida pa ibada, Jumba la Ufalme. Wanaonyesha staha ifaayo kwa mahali hapo. Wanadhihirisha roho ya bidii katika kupatunza, na wanajitahidi sikuzote kupatumia ifaavyo. Wewe pia na ufuate lile himizo ambalo Yehova mwenyewe atoa: “Jitunze mguu wako uendapo nyumbani kwa Mungu.”—Mhubiri 5:1.