Uchunguzi Wenye Kuendelea wa Kazi Yenye Uharaka ya Kufanya Wanafunzi
1 Kabla ya kuondoka duniani, Yesu aliwaamuru wafuasi wake ‘wafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ Hilo lilitaka wafanye kampeni kali ya kuhubiri na kufundisha na kupanua utendaji wao katika dunia yote inayokaliwa na watu. (Mt. 28:19, 20; Mdo. 1:8) Je, waliona utume huo kuwa mzigo wenye kulemea ulio mgumu mno kutimiza? Sivyo kulingana na mtume Yohana. Baada ya kuwa mfanya-wanafunzi kwa miaka 65, yeye aliandika hivi: “Hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake; na bado amri zake si zenye kulemea.”—1 Yoh. 5:3.
2 Taarifa ya Kimaandiko ya utendaji wa Wakristo wa mapema yathibitisha kwamba walitimiza utume wao wa kufanya wanafunzi wa Yesu Kristo kwa bidii. (2 Tim. 4:1, 2) Walifanya hivyo, si kwa sababu tu ulikuwa wajibu, bali kwa sababu ya tamaa yao yenye upendo ya kumsifu Mungu na kuletea wengine tumaini la wokovu. (Mdo. 13:47-49) Kwa sababu wote waliokuja kuwa wanafunzi, baadaye wao wenyewe walikuwa wafanya-wanafunzi, kutaniko la Kikristo lilikua haraka katika karne ya kwanza.—Mdo. 5:14; 6:7; 16:5.
3 Kazi ya Kufanya Wanafunzi Yasonga Haraka: Kazi kubwa zaidi ya kufanya wanafunzi ambayo imepata kufanywa wakati wote inatimizwa katika karne hii ya 20! Kufikia sasa, mamilioni ya watu wamekubali habari njema na kutenda kulingana nayo. (Luka 8:15) Kwa kuwa wakati wa mfumo huu wa sasa wa mambo unapungua, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ametuandalia vyombo vinavyofanya iwezekane kwa watu wenye moyo wenye kufuata haki wajifunze kweli haraka.—Mt. 24:45.
4 Katika 1995 tulipokea kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, na katika 1996 kilifuatwa na broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Kuhusu kitabu Ujuzi, toleo la Mnara wa Mlinzi la Januari 15, 1996, ukurasa wa 14, lilisema: “Mafunzo ya kitabu hiki cha kurasa 192 yaweza kuchukua wakati mfupi kwa kulinganishwa, na wale ‘wenye mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele’ watazamiwa kuweza kujifunza vya kutosha kupitia funzo la kitabu hicho ili wajiweke wakfu kwa Yehova na kubatizwa.”—Mdo. 13:48.
5 Nyongeza ya Huduma ya Ufalme Yetu ya Juni 1996, “Jinsi ya Kufanya Wanafunzi kwa Kutumia Kitabu Ujuzi,” ilitupatia mradi huu: “Ikitegemea hali na uwezo wa mwanafunzi, huenda ikawezekana kwako kusoma sura nzima katika kipindi kimoja cha muda wa saa moja hivi, bila kuharakisha funzo. Wanafunzi watafanya maendeleo mazuri wakati mwalimu na mwanafunzi wanaposhikilia miadi yao ya funzo kila juma.” Makala hiyo iliendelea kusema: “Inatazamiwa kwamba kufikia wakati mtu anapomaliza funzo la kitabu Ujuzi, unyofu wake na kina cha upendezi wake katika kumtumikia Mungu lazima utakuwa wazi.” Sanduku la Swali katika Huduma ya Ufalme Yetu ya Oktoba 1996 lilieleza: “Yatarajiwa kwamba katika muda mfupi kwa kulinganishwa, mwalimu mwenye matokeo ataweza kumsaidia mwanafunzi wa kawaida mwenye moyo mweupe apate ujuzi wa kutosha ili kufanya uamuzi wenye akili wa kumtumikia Yehova.”
6 Kitabu Ujuzi Chawa na Matokeo: Katika pindi ambayo mwanamke fulani mchanga alibatizwa, asimulia jinsi alivyohisi kuhusu kujifunza kitabu Ujuzi. Kwa muda fulani alikuwa akijifunza kitabu Kuishi Milele. Kitabu Ujuzi kilipotolewa, dada mwenye kuongoza funzo naye aligeukia kitabu kipya. Upesi, mwanafunzi huyo aliweza kuona kwamba hilo lilimtaka afanye uamuzi, naye alichochewa kufanya maendeleo haraka kuanzia hapo na kuendelea. Mwanamke huyo mchanga, ambaye sasa ni dada yetu, asema hivi: “Kitabu Kuishi Milele kilinisaidia kumpenda Yehova, lakini kitabu Ujuzi kilinisaidia kufanya uamuzi wa kumtumikia.”
7 Ona vile mwanamke mwingine alivyojifunza kweli haraka. Baada ya kujifunza mara mbili, alihudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme wakati wa ziara ya mwangalizi wa mzunguko. Juma hilo, ikiwa mara yake ya tatu kujifunza, alimwambia kwamba alikuwa amejiweka wakfu kwa Yehova naye alitaka kuwa mhubiri asiyebatizwa. Alikutana na wazee, ambao walimpendekeza awe mhubiri, na juma lililofuata alianza kwenda katika utumishi wa shambani. Alijiingiza sana katika funzo lake la Biblia hivi kwamba akachukua likizo kutoka kazini ili ajifunze mara mbili au tatu kwa juma na kutumia wakati mwingi katika huduma. Nyakati nyingine, walijifunza sura mbili au tatu katika kipindi kimoja. Alianza kutumia yale aliyokuwa akijifunza katika sehemu zote za maisha yake, akamaliza kitabu Ujuzi kwa majuma manne, na kufanya maendeleo hadi ubatizo!
8 Mume wa dada mmoja ajisimulia yeye binafsi kuwa “mfano hasa wa mwenzi asiyeamini.” Siku moja, ndugu alimtolea funzo la Biblia katika kitabu Ujuzi ikiwa tu kwamba mwanamume huyo angeweza kuacha baada ya kujifunza mara ya kwanza au wakati wowote baada ya hapo. Mume huyo alikubali kujaribu, ajapokuwa mtu ambaye hakujifunza vizuri alipokuwa mchanga, na ambaye hakusoma fasihi za kidini za aina yoyote kwa miaka zaidi ya 20. Itikio lake la kujifunza kitabu Ujuzi lilikuwaje? Yeye alisema hivi: “Ilipendeza sana kujua kwamba msaada huo wa kujifunza Biblia uliandikwa kwa usahili hivyo. Habari hiyo ilitolewa waziwazi na kupatana na akili hivi kwamba punde, nilikuwa nikitazamia funzo letu lililokuwa likifuata kwa hamu nyingi sana. Mwalimu wangu alifuata kwa ustadi njia za kufanya wanafunzi ambazo zimeonyeshwa na Sosaiti, na kwa msaada wa roho takatifu ya Yehova, nilibatizwa miezi minne baadaye. Naweza kusema kikweli kwamba tukisitawisha upendo wa kufanya wanafunzi, tukiendelea kutafuta walio na moyo ufaao katika huduma ya shambani, tukitumia kitabu Ujuzi na misaada mingine ya Biblia inayoandaliwa na Sosaiti na zaidi ya yote, kusali ili kupata mwelekezo wa Yehova, twaweza kuwa na pendeleo la pekee zaidi la kusaidia kufanya wanafunzi.” Yaliyo juu ni mambo yaliyoonwa ya kipekee. Wengi kati ya wanafunzi wetu hawaji katika kweli haraka hivyo.
9 Wanafunzi Hufanya Maendeleo kwa Mwendo Tofauti-Tofauti: Yapaswa kutambuliwa kwamba uwezo wa walimu na wanafunzi wa Neno la Mungu waweza kutofautiana kwa kiasi kikubwa kadiri. Ukuzi wa kiroho waweza kuwa wa polepole au haraka-haraka. Wanafunzi fulani hufanya maendeleo kwa miezi michache ambapo wengine huchukua muda mrefu. Kiwango cha ukuzi wa mtu wa kiroho huathiriwa na malezi yake ya kielimu, na kiwango cha uthamini wake kwa mambo ya kiroho, na kina cha ujitoaji wake kwa Yehova. Si kila mtu tunayejifunza naye aliye na “akili iliyo kubwa zaidi sana” ya kujifunza Maandiko kila siku, kama walivyokuwa Waberoya ambao walikuja kuwa waamini.—Mdo. 17:11, 12.
10 Hiyo ndiyo sababu nyongeza ya Huduma ya Ufalme Yetu ya Aprili 1998, yenye kichwa “Mafunzo Zaidi ya Biblia Yanatakwa,” yatoa mwelekezo huu ulio halisi: “Bila shaka, wanafunzi wote wa Biblia hawafanyi maendeleo kwa kiwango kilekile. Baadhi yao si wenye mwelekeo wa kiroho kama wengine wala hawaelewi mambo haraka wanapofundishwa. Wengine huwa na maisha yenye shughuli nyingi sana nao huenda wasiweze kutoa wakati unaohitajiwa ili kumaliza sura nzima kila juma. Hivyo, katika visa fulani huenda ikawa lazima kuchukua zaidi ya kipindi kimoja cha funzo [kumaliza] sura kadhaa na miezi ya ziada kumaliza kitabu.”
11 Wafanyao Wanafunzi Huwa na Maoni Yaliyosawazika: Ni muhimu kukadiria mwendo wa funzo kulingana na hali na kipaji cha mwanafunzi. Kwa kuwa twatiwa moyo kuanzisha mafunzo katika broshua Anataka, huenda ikachukua miezi miwili au mitatu kumaliza kabla ya kuanza kitabu Ujuzi. Tukitumia madokezo yote yaliyo kwenye nyongeza ya Huduma ya Ufalme Yetu ya Juni 1996, inaweza kuchukua miezi sita hadi tisa tu kumaliza kitabu Ujuzi. Wengine ambao walianza funzo tu kwa kutumia kitabu Ujuzi waligeukia broshua Anataka kusaidia mwanafunzi ajifunze kweli za msingi za Biblia haraka. Kisha wakarudia kujifunza tena kitabu Ujuzi. Funzo likianzwa kwa kutumia kitabu Ujuzi na liendelee vizuri, huenda ikafaa kujifunza broshua Anataka baada ya kumaliza kitabu hicho, hivyo, kupitia haraka kweli za msingi za Neno la Mungu. Vyovyote vile, hatutaki kumzuia mwanafunzi kupata uelewevu ulio wazi kwa sababu tu ya kumaliza kitabu haraka. Kila mwanafunzi huhitaji msingi imara wa imani yake mpya katika Neno la Mungu.
12 Tukijua nyakati tunamoishi, kusaidia wengine wajifunze kweli ni jambo la uharaka zaidi sasa kuliko wakati mwingine wowote. Mbali na kuendelea kusali ili kuanzisha mafunzo mapya ya Biblia, na tusali kwa ajili ya wale ambao tayari tunajifunza nao. Ndipo itakapokuwa shangwe yetu kuendelea kubatiza wanafunzi wengine zaidi “siku zote hadi umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mt. 28:20.