Pata Kuwajua Ndugu Zako
1 Biblia hufafanua rafiki wa kweli kuwa mtu aambatanaye kwa ukaribu kuliko ndugu, ambaye daima hupenda na huwa mwaminifu-mshikamanifu, na ambaye humsaidia mwandamani wake wakati wa taabu. (Mit. 17:17; 18:24) Hatutapungukiwa na marafiki wa aina hiyo katika kutaniko tukijitahidi kujuana na kupendana.—Yn. 13:35.
2 Fursa za kupata kujuana na ndugu zetu zapatikana kabla na baada ya mikutano. Kwa nini usifike mapema na ukawie baadaye ili uweze kufurahia uchangamfu na shauku ya ushirika? Tafuta ndugu mbalimbali wa kuzungumza nao, kutia ndani wazee-wazee, walio na uzoefu na wachanga au wenye haya.
3 Anzisha Mazungumzo: Endelea zaidi ya kusalimu kijuu-juu tu ndugu zako. Waweza kuanzisha mazungumzo kwa kushiriki jambo lililoonwa katika huduma ya shambani, jambo lenye kupendeza katika magazeti ya karibuni, au elezo linalohusu mkutano ambao umetoka kwisha. Waweza kujifunza mengi kuhusu ndugu zako kwa kuwa msikilizaji mzuri, kuwatia moyo waongee juu ya mambo waliyojionea na mambo wanayojifunza. Kuuliza tu jinsi mtu alivyopata kumjua Yehova kwaweza kufunua mengi. Wengine wamepatwa na mambo yenye kuimarisha imani maishani mwao, ilhali wengine wanavumilia hali ambazo kwa sasa huenda zikaonekana kuwa ngumu kwa wengi kuziwazia. Kutambua hilo kutatusaidia, tukiwa rafiki wa kweli, kuwa wenye hisia nyepesi na kuitikia mahitaji ya wengine.
4 Fanyeni Urafiki: Baada ya kifo cha mtoto wake, dada mmoja aliona ugumu kuimba nyimbo za Ufalme zilizotaja ufufuo. Yeye akumbuka hivi: “Wakati mmoja, dada aliyekuwa amekaa upande ule mwingine wa njia baina ya viti aliniona nikilia. Alikuja, akaniwekelea mikono yake, na kuimba wimbo wote pamoja nami. Nilihisi nimejawa na upendo kwa ndugu na dada na mwenye furaha sana kwamba tulikuwa tumeenda kwenye mikutano, tukitambua kwamba hapo ndipo palipo na msaada wetu, hapo katika Jumba la Ufalme.” Twapaswa kufanya urafiki na ndugu zetu kwa kuwapa faraja inapohitajiwa na kitia-moyo nyakati zote.—Ebr. 10:24, 25.
5 Ulimwengu huu uwapo wenye kuonea zaidi, acheni tuazimie kuwajua ndugu zetu vizuri. Badilishano hili la kweli la kitia-moyo litathibitika kuwa baraka kwa wote.—Rom. 1:11, 12.