Familia Zawezaje Kuwa na Nguvu Kiroho?
1 Familia za Kikristo zapongezwa kwa “kuzoea ujitoaji-kimungu kwa watu wa nyumbani mwao.” (1 Tim. 5:4) Hata hivyo, kwa kuwa tumezungukwa na uvutano mwingi mbaya unaoweza kudhoofisha imani yetu, ni jambo la maana kwa familia kufanya bidii ili zidumu zikiwa na nguvu kiroho. Hilo laweza kufanywaje?
2 Jizoeze Ukichwa Kama wa Kristo: Vichwa vya familia wanahitaji kumwiga Yesu Kristo kwa njia ambayo wanatimiza daraka lao la kuimarisha nyumba zao. Mbali na kuonyesha upendo wake kwa kutoa uhai wake uwe dhabihu mara moja, Yesu bado anaendelea ‘kulisha na kutunza sana’ kutaniko. (Efe. 5:25-29) Wazazi wenye upendo hufuata kielelezo hicho cha utunzaji mwororo kwa kuhakikisha kwamba mahitaji ya kiroho ya familia yao yanatunzwa kila siku. Hiyo yatia ndani kuwa na funzo la Biblia la familia kila juma, kuwa na mazungumzo yenye kujenga kiroho inapowezekana, na kushughulikia matatizo yanapotokea.—Kum. 6:6, 7.
3 Katika Huduma ya Shambani: Washiriki wote wa familia wanapaswa kufahamu kwamba kuhubiria wengine juu ya Yehova na makusudi yake ni sehemu muhimu ya ibada yao. (Isa. 43:10-12) Ikiwa nyinyi wazazi mwataka watoto wenu wawe Mashahidi wa Yehova waaminifu, lazima mwanze mapema sana kutayarisha mioyo yao kwa ajili ya huduma. Zungumzieni sababu zinazofanya kuwe na uhitaji wa kujitolea katika utumishi na kuhubiri kila juma. (Mt. 22:37-39) Kisha fanyeni mipango ili mshiriki nao kwa ukawaida katika huduma ya shambani.
4 Wasaidie kuthamini zaidi kazi ya kuhubiri kwa kuweka kando wakati katika funzo la familia la kila juma ili mtayarishe na kujizoeza utoaji wenye matokeo. Wape watoto wako mazoezi katika huduma wakiwa mmoja-mmoja, ukiwasaidia wafanye maendeleo kulingana na umri na uwezo wao. Baada ya kuhubiri pamoja kwa muda fulani, zungumzia jinsi walivyojionea wema wa Yehova. Simulia mambo yaliyoonwa yenye kujenga imani. Kadiri familia ‘zinavyoonja kwamba Bwana ni mwenye fadhili,’ ndivyo zitakavyokuwa na uhusiano wa karibu zaidi na Yehova, zikiimarishwa kukataa “ubaya wote.”—1 Pet. 2:1-3.
5 Kwenye Mikutano: Inapendeza kama nini washiriki wa familia wakisaidiana kuhudhuria mikutano, hasa kama mmoja wao amechoka, amevunjika moyo, au amelemewa! “Babangu anapofika nyumbani kutoka kazini, huwa amechoka,” akasema dada mmoja mchanga. “Lakini mimi humwambia jambo fulani lenye kupendeza litakalozungumziwa kwenye mkutano jioni hiyo, na hiyo humtia moyo kwenda. Kisha mimi ninapochoka yeye hunitia moyo kwenda.”—Ebr. 10:24, 25.
6 Kufanya Mambo Pamoja: Familia zapaswa kufanya mambo pamoja kama vile kusaidiana kazi za nyumbani. Pia wanapaswa kuweka kando wakati kwa ajili ya tafrija ambazo zimechaguliwa ifaavyo. Kwenda mandari, kutembea safari ndefu, kucheza, na kutembelea watu wa ukoo au marafiki kwaweza kuleta furaha na kumbukumbu nzuri za baadaye.—Mhu. 3:4.
7 Familia za Kikristo zenye nguvu hushinda magumu ya kila siku yanayokabili hali yao ya kiroho. Kwa kuendelea kuwa na uhusiano wa karibu zaidi na Yehova, wanaona nguvu anazowapatia.—Efe. 6:10.