Je, Unaweza Kusaidia?
1 Sikuzote Yehova hutafuta njia za kuwasaidia watumishi wake washikamanifu. (2 Nya. 16:9; Isa. 41:10, 13) Akimlinganisha Yehova na mchungaji mwenye kujali, Isaya aliandika: “Atawakusanya pamoja wana-kondoo kwa mkono wake; naye atawabeba katika kifua chake. Wale wanaonyonya atawaongoza kwa uangalifu.” (Isa. 40:11) Fikiria baadhi ya njia tunazoweza kuiga jinsi Yehova anavyowahangaikia watu wake kwa upendo.
2 Wasaidie Wapya: Tunaweza kuwasaidia wapya kwa kuwaalika wafurahie ushirika wenye kujenga pamoja nasi. (Met. 13:20) Akikumbuka jinsi wengine walivyomsaidia wakati alipoanza kushirikiana na kutaniko, ndugu mmoja alisema hivi: “Familia fulani ilinialika kwenye funzo lao la familia mara kadhaa. Nilipofanya maendeleo, wenzi wa ndoa ambao ni mapainia walinialika nijiunge nao wakati walipohubiri siku nzima. Sikuzote tulizungumzia mambo yenye kujenga kiroho.” Aliongeza kusema: “Kabla ya kuwa Mkristo, nilikuwa nikienda kujistarehesha Ijumaa na Jumamosi usiku. Lakini nilipoanza kushirikiana na akina ndugu, sikuhitaji kufanya hivyo tena.” Upendezi ambao akina ndugu kutanikoni walimwonyesha ndugu huyo, ulimsaidia kuwa na imani yenye nguvu, na sasa yeye ni Mwanabetheli.—Kol. 2:6, 7.
3 Jenganeni: Ndugu zetu wanapokabili hali ngumu, tunaweza kutumia fursa hiyo kuwasaidia. Je, unaweza kupanga kuhubiri kwa njia ya simu pamoja na mhubiri mgonjwa au kumwalika kwenye funzo la Biblia, labda hata kumpeleka mwanafunzi nyumbani kwa mhubiri huyo? Je, unaweza kumsaidia mzazi mwenye watoto wadogo kwenye huduma ya shambani? Je, kuna wahubiri wenye haya ambao wangefurahia msaada wako wanapofanya ziara za kurudia au wanaposhiriki katika aina nyingine ya huduma? Kupendezwa na ndugu zetu kutatuchochea kutafuta njia za kuwajenga kiroho.—Rom. 14:19.
4 Tunapoiga jinsi Yehova anavyowajali watumishi wake, tunajengana, kuimarishana, kusaidia kutaniko liwe na upendo na umoja, na kumtukuza Baba yetu wa mbinguni.—Efe. 4:16.