Tutaungana Ulimwenguni Pote Kutangaza Kusanyiko la Wilaya la “Mfuateni Kristo!” Kwa Mara Nyingine
Tena Wahubiru Watasanbaza Nwaliko wa Pekee
1 Mwaka uliopita, kampeni iliyofanywa ulimwenguni pote kutangaza Kusanyiko la Wilaya la “Ukombozi Unakaribia!” iliwachochea sana watu wanaopendezwa. Wale waliokubali mwaliko huo wa pekee na kuhudhuria, walijionea kwa mara ya kwanza karamu kubwa ya kiroho ya Mashahidi wa Yehova. (Isa. 65:13) Walifurahia ushirika wa undugu wetu wa Kikristo wenye umoja na uchangamfu. (Zab. 133:1) Ili kuwasaidia wengi iwezekanavyo wahudhurie Kusanyiko la Wilaya la “Mfuateni Kristo!” kwa mara nyingine tena tutasambaza mwaliko wa pekee ulimwenguni pote.
2 Matokeo ya Mwaka Uliopita: Kulingana na ripoti tulizopokea kutoka sehemu zote za ulimwengu, matokeo mazuri yalipatikana kwa kutangaza Kusanyiko la Wilaya la “Ukombozi Unakaribia!” Katika sehemu nyingi, vyombo vya habari vilitangaza mambo mazuri kutuhusu. Kwa mfano, katika jiji moja, gazeti fulani lilichapisha makala yenye safu sita kuhusu kampeni hiyo, likisema: “Ili kuwafikia watu wote kwa wakati, Mashahidi wamefanya jitihada za pekee katika eneo hili, wakifanya kazi kwa saa nyingi zaidi, kutembea mbali zaidi, na kuongea haraka zaidi.” Kampeni hiyo ilivutia sana vyombo vya habari katika jiji lingine hivi kwamba habari kemkemu kuihusu zilisambazwa. Angalau magazeti matatu yaliripoti kuhusu utendaji wetu kabla ya kusanyiko. Mwandishi mmoja aliandika makala kadhaa ndefu ambazo zilichukua zaidi ya kurasa mbili katika toleo la Jumapili la gazeti fulani. Gazeti hilo lilieleza kwa mapana na marefu kuhusu imani yetu, undugu wetu, kampeni ya kusambaza mwaliko, na kusanyiko. Mhubiri mmoja alipotoa mwaliko huo katika nyumba moja, mwenye nyumba alimkatiza akisema: “Ndiyo. Nimetoka tu kusoma habari hiyo katika gazeti!” Mwenye nyumba mwingine alisema: “Nimetoka tu kusoma juu yenu, na tayari mmefika! Je, huo ni mwaliko wangu?” Kisha akaongezea, “Mashahidi wa Yehova wanafanya jambo zuri sana.”
3 Watu wengi waliopendezwa walifika katika vituo vya makusanyiko wakiwa na karatasi zao za mwaliko. Watu fulani waliopendezwa waliendesha magari kutoka majiji ya mbali ili wahudhurie vipindi vya makusanyiko. Jitihada zetu za kuwaalika wengine zilichangia ongezeko la hudhurio. Katika nchi moja, kulikuwa na ongezeko la asilimia 27 katika hudhurio ikilinganishwa na mwaka uliotangulia.
4 Kufanyia Kazi Eneo: Itafaa muanze kusambaza karatasi za mwaliko majuma matatu kabla ya kusanyiko lenu. Jitahidini juu chini kufanyia kazi eneo lote la kutaniko. Juma moja kabla ya kusanyiko, wahubiri wa makutaniko yaliyo na maeneo makubwa wanaweza kuingiza mwaliko chini ya mlango ikiwa hakuna mtu nyumbani katika juma linalotangulia kusanyiko. Makutaniko yanapaswa kujitahidi kusambaza mialiko yote iliyotumwa na kufanyia kazi eneo kubwa iwezekanavyo. Mialiko ya ziada inaweza kutumiwa na mapainia wa kutaniko.
5 Mambo ya Kusema: Mnaweza kusema: “Tunashiriki katika kampeni inayofanywa ulimwenguni pote ili kusambaza mwaliko huu unaohusu tukio muhimu litakalofanyika karibuni. Hii ni nakala yako. Habari zaidi ziko katika mwaliko wenyewe.” Ukiongea kwa ufupi, utawafikia wengi. Bila shaka, mwenye nyumba akiwa na maswali, mjibu. Akipendezwa, andika jina lake na umrudie haraka iwezekanavyo.
6 Ni muhimu kama nini tujitahidi kumfuata Kristo! (Yoh. 3:36) Kusanyiko la wilaya linalokuja litawasaidia wote watakaohudhuria kufanya hivyo. Bila shaka, tunaweza kutazamia kwamba ushahidi mkubwa utatolewa tena tunapoungana kutangaza Kusanyiko la Wilaya la “Mfuateni Kristo!” Hivyo basi, tia bidii kuwaalika wengi iwezekanavyo wahudhurie. Yehova na abariki jitihada zako unaposhiriki katika kampeni hii itakayofanywa ulimwenguni pote.