Ubadilishanaji wa Kitia-Moyo kwa Wote
1 Mtume Paulo aliliandikia hivi kutaniko huko Roma: “Ninatamani kuwaona ninyi, ili niwape sehemu ya zawadi ya kiroho kusudi mfanywe imara; au, badala ya hivyo, kwamba kuwe na ubadilishanaji wa kitia-moyo kati yenu, kila mmoja kupitia imani ya mwingine, yenu na yangu pia.” (Rom. 1:11, 12) Ziara za nyakati za kisasa za waangalizi wanaosafiri zinaandaa nafasi kama hiyo ya ubadilishanaji wa kitia-moyo.
2 Kutaniko: Kwa kawaida tangazo kuhusu ziara ya mwangalizi wa mzunguko hutolewa miezi mitatu hivi mapema. Hilo hutupa nafasi ya kubadili ratiba zetu ili tunufaike kikamili. (Efe. 5:15, 16) Ikiwa umeajiriwa, huenda ukaomba likizo ili ushiriki katika utumishi wa shambani juma la ziara. Wengine wanafanya mipango ili wawe mapainia wasaidizi katika mwezi wa ziara. Iwapo ulikuwa umepanga kusafiri juma la ziara, je, unaweza kubadili mipango yako ili uwepo juma hilo?
3 Kusudi la msingi la ziara ya mwangalizi wa mzunguko ni kuwatia moyo na kuwazoeza watu mmoja-mmoja katika huduma ya shambani. Je, unaweza kuomba uhubiri naye au na mke wake ikiwa ameoa? Mwangalizi wa mzunguko anafurahia kuhubiri na wahubiri mbalimbali, kutia ndani wale wasio na uzoefu mwingi au wale ambao wangependa kuwa na ustadi zaidi katika huduma. Wote wanaweza kujifunza kutokana na njia yake ya kuhubiri na kutumia mapendekezo yoyote anayotoa kwa fadhili. (1 Kor. 4:16, 17) Kumkaribisha ale chakula pamoja nawe kutatokeza nafasi zaidi ya kushirikiana naye. (Ebr. 13:2) Sikiliza hotuba zake kwa makini kwa kuwa zimetayarishwa kulingana na hali za kutaniko.
4 Mwangalizi wa Mzunguko: Mtume Paulo hakuwa tofauti na ndugu aliowatumikia. Kwa kuwa yeye pia alikabili matatizo na alifadhaika, alihitaji kitia-moyo na alishukuru alipotiwa moyo. (2 Kor. 11:26-28) Kutaniko huko Roma liliposikia kwamba Paulo, ambaye sasa alikuwa mfungwa, hatimaye alikuwa njiani kuja Roma, baadhi walisafiri mpaka Soko la Apio na Mikahawa Mitatu ili kumlaki—umbali wa kilomita 74 hivi! “Alipowaona, Paulo akamshukuru Mungu na kujipa moyo.” (Mdo. 28:15) Hali kadhalika, wewe pia unaweza kumtia moyo mwangalizi wa mzunguko. Mpe “heshima mara mbili” kwa kuitegemeza ziara yake kwa bidii. (1 Tim. 5:17) Kwa maneno na matendo, onyesha kwamba unathamini jitihada zake kwa ajili yako. Yeye pamoja na mke wake watashangilia wanapoona imani, upendo, na uvumilivu wako.—2 The. 1:3, 4.
5 Katika hizi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” ni nani kati yetu asiyehitaji kutiwa moyo? (2 Tim. 3:1) Amua sasa kuwapo na kushiriki kikamili katika juma la pekee la ziara ya mwangalizi wa mzunguko. Sisi sote—waangalizi wanaosafiri na pia wahubiri makutanikoni—tunaweza kubadilishana kitia-moyo kwa shangwe. Kwa kufanya hivyo, ‘tutaendelea pia kufarijiana na kujengana.’—1 The. 5:11.
[Maswali ya Funzo]
1. Ziara za waangalizi wanaosafiri huandaa nafasi gani za pekee?
2. Kwa nini tangazo kuhusu ziara ya mwangalizi hutolewa mapema?
3. Sisi binafsi tunaweza kufanya nini ili tutiwe moyo wakati wa ziara?
4. Tunaweza kumtiaje moyo mwangalizi wetu wa mzunguko?
5. Kwa nini kila mmoja wetu anahitaji kitia-moyo leo?