‘Jina la Mungu na Litakaswe’
1. Programu ya kusanyiko la mzunguko la mwaka wa utumishi wa 2012 ina kichwa gani, na msingi wake ni nini?
1 Tuna pendeleo kama nini kujulikana kwa jina la Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote, Yehova! Mungu mwenyewe ndiye aliyetupatia jina hilo, na hasa tangu mwaka wa 1931, tukiwa Mashahidi wa Yehova, tumejulikana kwa jina hilo la pekee la Yehova. (Isa. 43:10) Yesu, Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu, alilithamini sana jina hilo, hivi kwamba akalitanguliza katika ile sala aliyowafundisha wafuasi wake. (Mt. 6:9) Maneno ya Yesu ndiyo msingi wa kichwa cha programu ya kusanyiko letu la mzunguko la mwaka wa utumishi wa 2012. Kichwa hicho ni “Jina la Mungu na Litakaswe.”
2. Tunatazamia habari zipi?
2 Mambo Tutakayojifunza: Siku ya Jumamosi, hotuba yenye kichwa “Tangazeni Jina la Mungu Mkiwa Watumishi wa Wakati Wote” itazungumzia ni kwa nini utumishi wa wakati wote ni njia yenye kuridhisha ya maisha. Pia, tutasikiliza mfululizo wenye kichwa, “Jihadhari Usililetee Suto Jina la Yehova,” ambao utatusaidia kuepuka tusinaswe na mambo manne yanayoweza kuwa mitego. Hotuba yenye kichwa “Kwa Nini Jina la Mungu Linapaswa Kutakaswa?” itajibu maswali haya, Ni nini kitakachotusaidia kuhubiri kwa bidii watu wanapoonekana kuwa hawapendezwi sana? na, Ni nini kitakachotusaidia kuwa wenye matokeo katika huduma? Siku ya Jumapili, tutafurahia mfululizo wenye sehemu nne unaozungumzia jinsi tunavyoweza kulitakasa jina la Mungu kupitia mawazo, usemi, maamuzi, na mwenendo wetu. Wapya hasa watafurahia hotuba ya watu wote yenye kichwa, “Yehova Atatakasa Jina Lake Kuu Kwenye Har–Magedoni.”
3. Tuna pendeleo gani, na programu hiyo itatusaidiaje?
3 Hivi karibuni, Yehova atachukua hatua ya kulitakasa jina lake. (Eze. 36:23) Kwa sasa, tuna pendeleo kubwa sana la kulitetea jina la Yehova na mambo yote ambayo linawakilisha. Tuna hakika kwamba programu ya kusanyiko hilo la mzunguko itasaidia kila mmoja wetu kutimiza daraka letu zito la kuitwa kwa jina la Mungu.