Elekeza Ngumi Zako kwa Hekima
1. Andiko la 1 Wakorintho 9:26 linaweza kutumikaje kuhusiana na huduma?
1 Mtume Paulo aliandika: “Jinsi ninavyokimbia si bila uhakika; jinsi ninavyoelekeza ngumi zangu ni ili nisiwe nikipiga hewa.” (1 Kor. 9:26) Paulo alikuwa akirejelea jinsi alivyofuatia miradi yake ya kiroho bila kukengeushwa na chochote. Hata hivyo, maneno hayo yanaweza kutumiwa kuhusiana na huduma yetu. Tunataka kuelekeza “ngumi” zetu, au bidii yetu, kwa hekima ili tuweze kuwa na matokeo bora zaidi. Jinsi gani?
2. Tunawezaje kumwiga Paulo na waeneza-injili wengine wa karne ya kwanza katika kuchagua wakati na mahali pa kuhubiri?
2 Nenda Mahali Watu Wanapopatikana: Paulo na waeneza-injili wengine wa karne ya kwanza walienda kuhubiri mahali ambapo walitazamia kupata watu. (Mdo. 5:42; 16:13; 17:17) Kwa hiyo, ikiwa watu wengi katika eneo lenu wanapatikana nyumbani jioni, huenda huo ndio wakati mzuri zaidi wa kuhubiri nyumba kwa nyumba. Je, kituo cha basi au cha gari-moshi katika eneo lenu kina shughuli nyingi asubuhi na jioni, wakati ambapo watu wanaenda au kutoka kazini? Ni wakati gani ambapo maeneo ya maduka huwa na watu wengi? Huenda huo ndio wakati unaofaa zaidi wa kutoa ushahidi barabarani.
3. Tunawezaje kuelekeza ngumi zetu kwa hekima kupitia jinsi tunavyohubiri eneo letu?
3 Hubiri Eneo kwa Hekima: Tunapaswa kuwa waangalifu ili tuelekeze ngumi zetu kwa hekima tunapohubiri katika eneo. Kwa mfano, badala ya kupeleka kikundi kikubwa cha wahubiri katika eneo moja na kutumia wakati na jitihada nyingi kuwapanga na kuwaelekeza, ni afadhali kugawanya kikundi hicho katika vikundi vidogo-vidogo. Vilevile, tunapohubiri katika maeneo ya mashambani, tunaweza kuhubiri eneo kwa haraka zaidi na kupata nafasi ya kuzungumza na watu wengi zaidi ikiwa wahubiri watagawanywa katika vikundi vidogo, na kila kikundi kipewe eneo lake. Je, tunaweza kuomba eneo la kibinafsi karibu na mahali tunapoishi, hivyo kupunguza muda tunaotumia kusafiri?
4. Nini kitakachotusaidia kuwa “wavuvi wa watu” wenye mafanikio?
4 Yesu alilinganisha waeneza-injili na “wavuvi wa watu.” (Marko 1:17) Lengo la mvuvi si tu kutupa wavu ndani ya maji, bali ni kuvua samaki. Kwa hiyo, wavuvi wanaofanikiwa huenda kuvua wakati na mahali wanapotazamia kupata samaki, nao huanza kuvua bila kupoteza wakati. Ndiyo, wanaelekeza jitihada zao kwa hekima. Acheni sisi pia tuwe na bidii kama hiyo katika huduma.—Ebr. 6:11.