Kuboresha Ustadi Wetu Katika Huduma—Kuandika Habari Zote Kuhusu Mtu Anayependezwa
“Jiangalie daima wewe mwenyewe na kufundisha kwako.” (1 Tim. 4:16) Shauri hilo la mtume Paulo lililoongozwa na roho kwa Timotheo linaonyesha kwamba iwe sisi ni wahubiri wapya au walio na uzoefu tunapaswa kujitahidi kufanya maendeleo tukiwa waeneza injili. Ili kutusaidia kutimiza jambo hilo, mfululizo mpya wenye kichwa “Kuboresha Ustadi Wetu Katika Huduma” utapatikana katika Huduma Yetu ya Ufalme. Kila makala itazungumzia jambo muhimu na kutoa mapendekezo fulani ya jinsi ya kulitumia. Katika mwezi huo, wote wanatiwa moyo kukazia fikira jambo hilo. Mwishoni mwa mwezi huo, kutakuwa na sehemu katika mkutano wa Utumishi ambayo itatupa fursa ya kuelezea jinsi tulivyofaidika kwa kufanyia kazi jambo hilo. Mwezi huu tunatiwa moyo kuandika habari zote kuhusu wanaopendezwa.
Kwa Nini Ni Muhimu: Ili kutimiza huduma yetu, tunapaswa kufanya mengi zaidi ya kuhubiri tu. Tunapaswa kuwarudia waliopendezwa na kuwafundisha, na hivyo kutilia maji mbegu za ukweli tulizopanda. (Mt. 28:19, 20; 1 Kor. 3:6-9) Hilo linahusisha kumtafuta tena mtu huyo, kuzungumzia mambo yanayomhangaisha, na kuendeleza mazungumzo tuliyokuwa nayo. Kwa hiyo, tunapopata mtu anayependezwa, ni muhimu kuandika habari kumhusu.
Jinsi ya Kufanya Hivyo:
• Hakikisha kwamba katika mkoba wako wa mahubiri una vifaa vya kuandika habari za wanaopendezwa. Panga vizuri habari hizo, ziwe nadhifu na za karibuni zaidi. Andika habari hizo mara tu unapomaliza kuongea na mtu huyo.
• Andika habari kumhusu mwenye nyumba huyo. Jina lake na anwani yake, kama vile mahali anapoishi, namba ya simu, au barua pepe. Ni mambo gani uliyoona kumhusu yeye na familia yake ambayo yanaweza kuwa muhimu?
• Andika mambo mliyozungumzia. Mlisoma maandiko gani? Alisema anaamini nini? Ulimwachia chapisho gani? Andika wakati, siku na tarehe ya ziara hiyo.
• Andika jambo utakalofanya katika ziara inayofuata. Uliahidi kuzungumzia jambo gani? Ulisema utarudi siku gani?
• Kila mara unaporudi andika mambo mapya ya ziara hiyo. Si vibaya kuandika habari nyingi zaidi ya unazohitaji.
Jaribu Dokezo Hili kwa Mwezi Mzima:
• Unapoandika habari za wanaopendezwa, mwambie yule unayehubiri naye ni mambo gani unayoandika.