Nyimbo Mpya za Ibada!
1 Katika mkutano wa kila mwaka wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, uliofanywa Oktoba 4, 2014, tangazo lilitolewa kuhusu mipango ya kurekebisha kitabu chetu cha nyimbo. Hilo lilikuwa tangazo lenye kusisimua sana! Wote waliohudhuria walikumbushwa umuhimu wa nyimbo za Ufalme katika ibada yetu.—Zab. 96:2.
2 Huenda ukajiuliza, ‘Kwa nini kitabu cha nyimbo kifanyiwe marekebisho?’ Kuna sababu kadhaa. Kwanza kabisa, uelewaji wetu wa Maandiko unaendelea kuboreshwa, na hilo linaathiri maneno ya nyimbo zetu. (Met. 4:18) Sababu nyingine ni kwamba maneno mengi yanayotumiwa katika kitabu chetu cha sasa yanategemea toleo lililopita la Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kiingereza. Maneno hayo yanapaswa kurekebishwa ili yapatane na maneno yaliyo kwenye toleo lililofanyiwa marekebisho la Biblia ya Kiingereza. Kwa kuwa ni kazi kubwa kufanya marekebisho hayo, iliamuliwa kwamba nyimbo chache mpya ziongezwe.
3 Je, ni lazima tusubiri hadi kitabu kipya kichapishwe ili tuanze kutumia nyimbo mpya? Hapana. Tunafurahi kuwajulisha kwamba katika miezi inayokuja, nyimbo kadhaa mpya zitapatikana katika Tovuti yetu ya jw.org/sw. Baada ya wimbo mpya kutolewa, utapangwa mwishoni mwa ratiba ya Mkutano wa Utumishi ukiwa na maandishi “wimbo mpya.”
4 Jinsi ya Kujifunza Nyimbo Mpya: Inaweza kuwa vigumu kujifunza wimbo mpya. Hata hivyo, kama mtunga zaburi, tungependa kuimba kwa shauku katika mikutano yetu badala ya ‘kunyamaza.’ (Zab. 30:12) Ili kujifunza wimbo mpya, fuata hatua zifuatazo:
Sikiliza tena na tena muziki wa piano, ambao utawekwa kwenye Tovuti yetu. Kadiri unavyosikiliza muziki huo, ndivyo itakavyokuwa rahisi zaidi kuukumbuka.
Jifunze maneno ya wimbo, na ujaribu kuyakariri.
Imba ukifuatana na muziki. Fanya hivyo hadi uujue wimbo huo.
Fanyeni mazoezi ya kuimba nyimbo mpya mara kadhaa katika Ibada ya Familia mpaka mzijue vizuri.
5 Katika miezi ijayo, wimbo mpya ukipangwa kumalizia Mkutano wa Utumishi, kutaniko litasikiliza kwanza muziki wa piano mara moja kabla ya kuimba. Kisha waliohudhuria wataimba wimbo huo wakifuatana na muziki kama ilivyo kawaida.
6 Kwa kweli, kuimba katika mikutano yetu kunatupatia fursa ya kumsifu Yehova pamoja kwa shangwe. Kwa hiyo, hatupaswi kuwa na zoea la kuondoka kwenye viti vyetu isivyo lazima wakati wa wimbo.
7 Kuna njia nyingine ya kuonyesha uthamini wetu kuelekea nyimbo zetu za kumsifu Yehova. Katika makusanyiko, tunasikiliza muziki kabla ya kila kipindi kuanza. Ndugu na dada kutoka sehemu mbalimbali duniani husafiri kwa gharama zao wenyewe hadi Patterson, New York, mara mbili kwa mwaka, ili kuandaa muziki huo wenye kuvutia tunaotumia katika ibada yetu. Kwa hiyo, mwenyekiti anapotuomba tuketi na kusikiliza muziki, tunapaswa kufanya hivyo. Kufanya hivyo kutatusaidia kutayarisha mioyo yetu ili tunufaike na programu.—Ezra 7:10.
8 Leo, tutamalizia mkutano kwa kuimba wimbo mpya wenye kichwa “Ufalme Umeanza Kutawala—Na Uje!” Wimbo huo, ambao uliimbwa katika mkutano wa kila mwaka uliofanywa hivi karibuni, ulitungwa hasa kwa kusudi la kuadhimisha miaka 100 ya kuzaliwa kwa Ufalme wa Mungu.
9 Kwa kweli, nyimbo hizo mpya ni “mambo mema” kutoka kwa Yehova. (Mt. 12:35a) Na tuazimie kujifunza nyimbo hizo mpya na kuimba kutoka moyoni, tukimsifu na kumheshimu Mungu wetu!—Zab. 147:1.