Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
AGOSTI 7-13
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | EZEKIELI 28-31
“Yehova Alithawabisha Taifa la Wapagani”
it-2 1136 ¶4
Tiro
Kuharibiwa kwa Jiji. Mazingiwa ya muda mrefu ya Nebukadneza dhidi ya Tiro yalifanya vichwa vya askari wa Nebukadneza viwe na “upara” kutokana na kuchubuliwa na kofia, na mabega yao ‘yalikwaruzwa’ kwa sababu ya kubeba vifaa ya ujenzi. Kwa kuwa Nebukadneza hakupata “malipo” yoyote kutokana na utumishi wake akiwa kama kifaa cha Mungu cha kuadhibu Tiro, Yehova aliahidi kumpa utajiri wa Misri kama malipo ya kazi aliyofanya. (Eze 29:17-20) Kulingana na maelezo ya mwanahistoria Myahudi Josephus, mazingiwa hayo yalidumu kwa miaka 13 (Against Apion, I, 156 [21]), na Wababiloni walitumia gharama kubwa. Historia ya ulimwengu haionyeshi Nebukadneza alifanya kazi kubwa kadiri gani au jitihada zake zilikuwa na matokeo gani. Lakini lazima watu wengi wa Tiro wawe walikufa na mali nyingi sana iliharibiwa.—Eze 26:7-12.
it-1 698 ¶5
Misri, Mmisri
Maandishi fulani ya Wababiloni, yanayofikiriwa kuwa ya mwaka wa 37 wa utawala wa Nebukadneza (588 K.W.K.), yamepatikana na yanaeleza kuhusu kampeni ya Babiloni dhidi ya Misri. Haijulikani ikiwa maandishi hayo yalihusu uvamizi wa kwanza au matukio mengine ya kijeshi. Vyovyote vile, Nebukadneza alipokea mali za Misri kama malipo ya utumishi wake wa kijeshi alipotekeleza hukumu ya Yehova dhidi ya Tiro, jiji lililowapinga watu wa Mungu.—Eze 29:18-20; 30:10-12.
g87 7/8 27 ¶4-5
Je! Ni Lazima Kodi Zote Zilipwe?
Ili kujibu swali hilo, tunaweza kutoa ulinganifu kwa habari ya mwenendo wa Muumba mwenyewe katika kulipa deni kwa serikali kwa utumishi uliotolewa. Hasira yenye haki ilimsukuma Yehova kuagiza uharibifu wa mji wa kale wa Tiro. Katika utimizo wa kitendo hiki, Mungu alitumia jeshi kubwa la Babuloni chini ya mfalme wao Nebukadreza. Ijapokuwa Babuloni ilishinda kazi hiyo iligharimu sana. Hivyo Yehova akahisi kwamba lazima walipwe kwa utumishi waliotoa. Maneno yake yanapatikana katika Ezekieli 29:18, 19: “Mwanadamu, Nebukadreza, mfalme wa Babeli, alilihudumisha jeshi lake huduma kuu juu ya Tiro. . . . lakini alikuwa hana mshahara uliotoka Tiro, wala yeye wala jeshi lake, kwa huduma ile aliyohudumu juu yake. Basi, Bwana [Yehova] asema hivi; Tazama, nitampa Nebukadreza, mfalme wa Babeli, hiyo nchi ya Misri; naye atawachukua watu wake jamii yote pia, na kutwaa mateka yake, na kutwaa mawindo yake, nayo yatakuwa ndio mshahara wa jeshi lake.”
Wanafunzi wa Biblia wanajua kwamba Nebukadreza alikuwa mwenye kiburi, mwenye kujifikiria, mfalme mpagani. Babuloni na majeshi yake ilijulikana kwa kuwatenda vikali wafungwa. Yehova hakukubali mwenendo huo, hata hivyo, kwake deni lilikuwa deni, naye alilipa lote.
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-2 604 ¶4-5
Ukamilifu
Mtenda-dhambi wa kwanza na mfalme wa Tiro. Dhambi na kutokamilika kwa wanadamu kulitanguliwa na dhambi na kutokamilika katika makao ya kiroho, kama Yesu alivyosema kwenye Yohana 8:44 na simulizi la mwanzo sura ya tatu linavyofunua. Ingawa wimbo wa huzuni uliorekodiwa kwenye Ezekieli 28:12-19 umeelekezwa moja kwa moja kwa “mfalme wa Tiro,” unapatana na matendo ya mwana wa kiroho wa Mungu ambaye alifanya dhambi. Kiburi cha “mfalme wa Tiro,” kujifanya kwake kuwa ‘mungu,’ kuitwa kwake “kerubi,” na kurejezewa kwa “Edeni, bustani ya Mungu,” kunalingana na maelezo ya Biblia kumhusu Shetani Ibilisi, ambaye alijitutumua kwa kiburi, anahusianishwa na nyoka wa Edeni, na anaitwa “mungu wa mfumo huu wa mambo.”—1 Ti 3:6; Mwa 3:1-5, 14, 15; Ufu 12:9; 2 Ko4:4.
Mfalme huyo wa Tiro asiyetajwa jina, anayeishi katika jiji linalodai kuwa ‘ukamilifu wa uzuri,’ alikuwa ‘amejaa hekima na mkamilifu [kivumishi kinachohusiana na cha Kiebrania ka·lalʹ] katika uzuri,’ na ‘hakuwa na kosa [Kiebrania, ta·mimʹ]’ katika njia zake tangu siku alipoumbwa na kuendelea mpaka ukosefu wa uadilifu ulipoonekana ndani yake. (Eze 27:3; 28:12, 15) Inawezekana kwamba wimbo wa huzuni wa Ezekieli ulikuwa kwa ajili ya ukoo wa watawala wa Tiro badala ya kwa mfalme mmoja tu. (Linganisha na unabii kuhusu “mfalme wa Babiloni” ambaye hajatajwa jina unaopatikana katika Isaya 14:4-20.) Katika kisa hicho, tunaweza kufikiria urafiki na ushirikiano uliokuwepo kati ya watawala wa Tiro katika kipindi cha utawala wa Mfalme Daudi na Sulemani. Wakati huo Tiro hata ilitoa mchango kwa ajili ya ujenzi wa hekalu la Yehova kwenye Mlima Moria. Kwa hiyo, mwanzoni, maofisa wa utawala wa Tiro hawakuwa na mtazamo usiofaa dhidi ya Israeli watu wa Yehova. (1Fa 5:1-18; 9:10, 11, 14; 2Nya 2:3-16) Hata hivyo, wafalme walioanza kutawala baadaye waliacha kuwa na mtazamo huo wa “kutokuwa na kosa,” na Tiro likaja kushutumiwa na manabii wa Mungu Yoeli na Amosi, na pia Ezekieli. (Yoe 3:4-8; Amo 1:9, 10) Mbali na ufanani wa wazi kati ya matendo ya “mfalme wa Tiro” na yale ya Mpinzani mkuu wa Mungu, unabii unaonyesha tena jinsi “ukamilifu” na “kutokuwa na kosa” kunavyoweza kutumiwa kwa njia ndogo.
AGOSTI 14-20
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | EZEKIELI 32-34
“Mlinzi Ana Daraka Zito”
it-2 1172 ¶2
Mlinzi
Maana ya Mfano. Yehova aliwainua manabii ambao walitumikia wakiwa walinzi wa taifa la Israeli kwa njia ya mfano (Yer 6:17), nao pia, nyakati nyingine walizungumza kuhusu walinzi kwa njia ya mfano. (Isa 21:6, 8; 52:8; 62:6; Ho 9:8.) Manabii hao waliofananishwa na walinzi walikuwa na wajibu wa kuwaonya watu kuhusu uharibifu uliokuwa ukikaribia, na ikiwa hawangetoa onyo, wangekuwa na hatia. Bila shaka, ikiwa watu hawangeitikia na wakose kutii onyo lililotolewa, damu ya watu hao ingekuwa juu yao wenyewe. (Eze 3:17-21; 33:1-9) Nabii asiye mwaminifu hakuwa na thamani kama tu mlinzi kipofu au mbwa asiyeweza kubweka.—Isa 56:10.
Endelea Kuhubiri Ule Ufalme
Kuepuka Hatia ya Damu
13 Lile daraka la Mashahidi walio wakfu wa Yehova kuonya watu juu ya hukumu ya Mungu inayokuja linaweza kulinganishwa na lile la Ezekieli katika wakati wake. Yeye alichaguliwa akatajwa wazi kuwa mlinzi kwa ile nyumba ya Israeli. Mgawo wake ulikuwa kuonya Waisraeli kwamba wangeuawa ikiwa wao hawangegeukia mbali kutoka njia zao mbaya. Ikiwa yeye akiwa mlinzi angekosa kusikizisha onyo hilo, bado watu waovu wale wangeuawa, lakini damu yao ingekuwa juu ya kichwa cha yule mlinzi mwenye kupuuza wajibu. Katika jambo hilo Yehova anaonyesha mwelekeo wake kuhusu ufikilizaji hukumu: “Sikufurahii kufa kwake mtu mwovu; bali aghairi mtu mwovu, na kuiacha njia yake mbaya, akaishi. Ghairini, ghairini, mkaache njia zenu mbaya; mbona mnataka kufa, Enyi nyumba ya Israeli?”—Ezekieli 33:1-11.
AGOSTI 21-27
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | EZEKIELI 35-38
Kutafuta Hazina za Kiroho
“Watalazimika Kujua Kwamba Mimi ni Yehova”
11 Baada ya mabaki kurudi Yuda, bara hilo lililofanywa ukiwa liligeuzwa likawa ‘bustani ya Edeni’ yenye kuzaa matunda. (Soma Ezekieli 36:33-36.) Vivyo hivyo, tangu 1919 Yehova amegeuza makao yaliyokuwa ukiwa ya mabaki waliopakwa mafuta yakawa paradiso ya kiroho yenye kujaa matunda, ambayo sasa inashirikiwa na “mkutano mkubwa.” Kwa kuwa hiyo paradiso ya kiroho imejazwa watu watakatifu, acheni kila Mkristo aliyejiweka wakfu ajitahidi kuiweka ikiwa safi.—Ezekieli 36:37, 38.
AGOSTI 28–SEPTEMBA 3
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | EZEKIELI 39-41
Kuifungua Njia ya Kurudi Kwenye Paradiso
20 Lakini namna gani vyombo vyote vya vita ambavyo mataifa yataviacha nyuma? Vyombo hivyo vitakuwa vingi ajabu, ikiangaliwa kulingana na ufananisho wa muda ambao itachukua kuondolea mbali sehemu zavyo zinazoweza kuteketea. (Ezekieli 39:8-10) Huenda waokokaji wa Har–Magedoni wakaweza kubadili vyombo vyovyote vya masalio ya mataifa ya kivita viwe na makusudi yenye mafaa.—Isaya 2:2-4.