Ezekieli
35 Neno la Yehova likanijia tena likisema: 2 “Mwana wa binadamu, uelekeze uso wako kwenye eneo lenye milima la Seiri,+ na utabiri dhidi yake.+ 3 Uliambie, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Niko dhidi yako, ewe eneo lenye milima la Seiri, nami nitaunyoosha mkono wangu dhidi yako na kukufanya uwe mahame na ukiwa.+ 4 Nitayafanya majiji yako kuwa magofu, nawe utakuwa mahame na ukiwa;+ nawe utalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova. 5 Kwa maana ulikuwa na chuki isiyo na mwisho,+ nawe uliwatia Waisraeli mikononi mwa upanga wakati wa msiba wao, wakati wa adhabu yao ya mwisho.”’+
6 “‘Kwa hiyo, kwa hakika kama ninavyoishi,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘nitakutayarisha kwa ajili ya umwagaji wa damu, na umwagaji wa damu utakufuatia.+ Kwa maana uliichukia damu, umwagaji wa damu utakufuatia.+ 7 Nitalifanya eneo lenye milima la Seiri kuwa mahame na ukiwa,+ nami nitamwangamiza mtu yeyote anayepitia humo na yeyote anayerudi. 8 Nitaijaza milima yake watu waliouawa; na wale waliouawa kwa upanga wataanguka kwenye vilima vyako, katika mabonde yako, na katika vijito vyako vyote. 9 Nitakufanya uwe ukiwa wa kudumu, na majiji yako hayatakaliwa;+ nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.’
10 “Kwa sababu ulisema, ‘Mataifa haya mawili na nchi hizi mbili zitakuwa zangu, nasi tutazimiliki zote mbili,’+ hata ingawa Yehova mwenyewe alikuwa humo, 11 ‘kwa hiyo kwa hakika kama ninavyoishi,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘nitakutendea kulingana na hasira ileile na wivu uleule ulioonyesha ulipowachukia;+ nami nitajijulisha miongoni mwao nitakapokuhukumu. 12 Kisha utalazimika kujua kwamba mimi mwenyewe, Yehova, nimesikia mambo yote ya dharau uliyosema kuhusu milima ya Israeli, uliposema, “Imefanywa ukiwa nasi tumepewa ili tuinyafue.”* 13 Nanyi mlizungumza kwa kiburi dhidi yangu, na kuzidisha maneno yenu dhidi yangu.+ Niliyasikia yote.’
14 “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Dunia yote itashangilia nitakapokufanya uwe mahame na ukiwa. 15 Kama ulivyoshangilia urithi wa watu wa nyumba ya Israeli ulipofanywa ukiwa, hivyo ndivyo nitakavyokutendea.+ Utakuwa magofu yaliyo ukiwa, ewe eneo lenye milima la Seiri, naam, Edomu yote;+ nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.’”