Usiamue kwa Kutazama Sura
■ Biblia hutushauri tusihukumu moyo wa mtu kwa kutazama sura yake. Hata akija kwenye mkutano wa Wakristo wa kweli amevaa matambara, apaswa kuonyeshwa upendo na kufkiriwa.—Yak. 2:1-4.
Matokeo mema yanayoweza kuja juu ya mtu huyo kwa sababu ya kumtendea kwa upendo yaonekana kutokana na yaliyompata kijana mmoja Mali, Afrika. Mmoja wa Mashahidi wa Yehova alikuwa akijifunza Biblia na kijana huyu na alimkaribisha mara nyingi ahudhurie mikutano katika Jumba la Ufalme. Ingawa aliahidi kufanya hivyo, kijana huyo hakufika. Ili aepuke kukaribishwa tena, mwishowe alifika.
Mavazi yake yalikuwa machafu, yalikuwa mafupi mno tena yalikuwa matambara. Isitoshe, alivaa kofia ya kusokotwa ambayo kanda zake zilifika magotini, nazo ziliunganishwa mwishoni zikawa kama mpira wa sufu. Alivaa hivyo akikusudia Mashahidi wa Yehova wakatae asiingie katika Jumba la Ufalme lao. Lakini jinsi alivyoshangaa kukaribishwa kwa uchangamfu!
Kijana huyo aeleza matokeo: “Sijaona aibu niliyoona wakati huo maishani mwangu. Nilikwenda kwenye Jumba la Ufalme ili nikafukuzwe, lakini lo! nikakaribishwa kama mmoja wa Mashahidi! Nakuambia, ingalikuwa vizuri kama ningalivaa mavazi ya adabu; kila mtu alikuwa amevalia vizuri.” Kilichoongeza aibu yake ni kwamba mmoja wa rafiki zake alikuwa amehudhuria pia. Mara baada ya mkutano rafiki yake alimjia akamwambia: “Wewe huna haya kuja kwenye Jumba la Ufalme na mavazi machafu hivyo? Sikutazamia utende hivyo.” Tangu wakati huo, kijana huyo alianza kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano bila mchezo. Sasa anashiriki kwa bidii nyingi kueleza wengine kweli ya Biblia.