Shamba la Starehe Duniani Pote Jinsi Gani?
ILI WATOSHELEZE tamaa yao ya kiasili ya kuelewa na kuona shangwe juu ya uumbaji, mamilioni ya watu huzuru mashamba ya starehe kila mwaka. Kwa uhakika sisi tungependezwa sana kuishi mahali penye uzuri mwingi kama huu wenye kuonekana hapa. Labda wewe waiona tamasha hii kuwa kikumbusha cha Paradiso katika Edeni ambamo Muumba wetu aliweka wanadamu wawili wa kwanza.
Jambo la umaana mkubwa ni kwamba miwili ya mito minne ambayo vichwa vyayo vilianzia Edeni ingali yatiririka leo. Hiyo ni Hidekeli, ambayo kwa kawaida zaidi hujulikana kuwa Tigri, na Eufrate. (Mwanzo 2:10-14) Hans Bruns mtafsiri wa Biblia alieleza juu ya usimulizi huu wa Biblia, akisema: “Mito hiyo imekusudiwa kuonyesha kwamba hii si hadithi ya kuwazia tu, bali ni jambo lililotendeka kikweli hapa duniani.”
Sawa na vile mashamba mengi ya starehe leo yalivyokuwa na mianzo midogo lakini yakapanuka kuwa makubwa mara nyingi kuliko eneo lile la asili, Mungu alikuwa na kusudi kama hilo kuhusiana na shamba lile lililokuwa kama bustani ya starehe katika Edeni. Mipaka yalo ingepanuliwa na jamaa ya kibinadamu yenye kukua mpaka Paradiso ifunike dunia nzima na kuipamba kwa uzuri mwingi ajabu wa kiasili.
Kwa kweli, kutotii kwa wanadamu wawili wa kwanza kuliwapotezea pendeleo la kuendelea kuona shangwe juu ya Paradiso hiyo ya asili. Lakini kusudi la Muumba wetu kwamba wanadamu waone shangwe juu ya paradiso ya kidunia halikubadilika. (Isaya 46:11; 55:11) Hivyo, Biblia huelekeza mara nyingi kwenye kuumbwa upya kwa Paradiso duniani chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu. Kwa kielelezo, unabii mmoja watabiri hivi: “Maana kwa uhakika Yehova atafariji Sayuni. . . . Atafanya jangwa lake liwe kama Edeni na uwanda wayo wenye jangwa uwe kama bustani ya Yehova.” Baadaye, unabii huu wanena pia juu ya watu kujenga nyumba, kupanda mashamba ya mizabibu, na kuona shangwe juu ya mazao ya dunia.—Isaya 51:3; 65:21-23, NW.
Vivyo hivyo, katika Ufunuo, kitabu cha mwisho cha Biblia, kuna njozi ya “mbingu mpya na dunia mpya” ambazo zingali ni za wakati ujao. “Mbingu mpya,” au utawala mpya wenye kuendeshwa na Mungu, zaonekana zikielekeza uangalifu kwenye dunia. Tokeo likiwa nini? Sisi twaambiwa, “Tazama! Mungu amefanya makao yake kati ya watu [angalia kwamba Mungu anenwa kuwa pamoja na wanadamu, si wanadamu pamoja na Mungu mbinguni]. Atakaa kati yao, nao watakuwa watu wake, naye atakuwa Mungu wao. Yeye atayafuta machozi yao yote; maana hakutakuwako tena na kifo, wala uchungu, wala kilio, wala maumivu; maana ile hali ya kale imepita!”—Ufunuo 21:1, 3, 4, HNWW.
Ahadi hizi za Biblia kuhusu paradiso yenye kurudishwa si matabiri ya kusisimua tu. Ingawa wahifadhi mazingira na vitu vya kiasili wamekuwa wakiwazia kupunguza ukubwa wa mbuga zilizo kama jangwa, huku wakitegemea watunga-sheria wenye huruma, Mtegemezaji wa ahadi za Biblia ni Muumba wa ulimwengu wote mzima, Yehova Mungu, ambaye Neno lake haliwezi na halitaweza kupita bila kutimizwa.
Leo, hususa katika mashamba ya starehe milimani, watembeleaji huwa na wasiwasi kwa kadiri fulani. Lakini katika shamba la starehe litakalokuja lizunguke tufe lote, viumbe wanyama hawataumiza wanadamu wala hawatakuwa tisho lolote kwao, wala wanyama hawatakimbia na kutetemeka waonapo mwanadamu, kwa maana Biblia yaahidi hivi: “Mbwa-mwitu atakaa pamoja na mwana-kondoo, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; ndama na mwana-simba na kinono watakuwa pamoja, na mtoto mdogo atawaongoza. Ng’ombe na dubu watalisha pamoja; watoto wao watalala pamoja; na simba atakula majani kama ng’ombe.”—Isaya 11:6-9.
Wakati huo itasisimua kama nini kutembea mwituni halafu simba wa mlimani ajiunge kutembea kando yako kwa muda mfupi au labda hata dubu mkubwa sana mwenye urafiki! Kitu chochote kilicho hai hakitahofu chenzake tena kamwe.
Waanzishi wa mashamba ya starehe yaliyo mazuri leo walikuwa na makusudio mazuri sana, wakatenga maeneo fulani yawe ya kulinda majani-majani na wanyama wa pori. Lakini kusudi la Mungu lenye kuendelea kukunjuka likihusu mfumo mmoja wa shamba la starehe duniani pote chini ya serikali ya Ufalme ndilo tu laweza kuhakikisha uhifadhi wa daima wa hazina za dunia. Ufalme huu tu ukiwa mikononi mwa Mwana wake, Yesu Kristo, ndio uwezao kusimamisha imara paradiso ya daima duniani pote na amani ya kweli kati ya mwanadamu na mwanadamu na kati ya mwanadamu na hayawani.