Usumbufu Hatari Unaoongezeka
Ushetani, au ibada ya Ibilisi, unaongezeka, ukihusisha dhabihu ya wanyama na wanadamu, masumbuo ya kingono, na vitendo vingine vya uhalifu. Wanashetani huamini nini? Na kwa nini dini yao ina uvutio huo? “Amkeni!” yajibu maswali hayo na pia kumfichua mtu aliye nyuma ya dini hiyo ya kuogopesha.
JE! WEWE huingiwa na ogofyo jingi kwa kufikiria wanadamu walio watu wazima wakinyemelea wanadamu wengine halafu wanaua windo lao kama simba wenye njaa, kisha wanakunywa damu yao, wanakula moyo wao na sehemu nyingine za mwili—yote hayo yakifanywa kwa jina la dini?
Je! wewe hutetemeka kwa kufikiria akina mama na akina baba wakitoa watoto wao wenyewe wakasumbuliwe kingono na wengine, hatimaye wakichinjwa juu ya madhabahu mbele ya watazamaji wote ili kutosheleza tamaa ya kidini?
Je! wewe huduwaa ufikiripo juu ya wanaume wenye kufanya mahusiano ya kingono pamoja na maiti katika majumba ya maziko ili wapendeze kiumbe-roho fulani ambaye wao hufikiri ni wa kimungu?
Je! hisia-moyo zako hufa ganzi usomapo juu ya watoto wachanga wakiua wazazi wao halafu wanakata-kata miili hiyo bila masikitiko wala majuto yoyote—yote hayo kwa kumfurahisha Ibilisi?
Je! wewe hutikisa kichwa chako kwa kutoamini kabisa kuhusu wale ambao huchimba makaburi, wanaiba vichwa na kukata-kata vifundo vya vidole ili vikavaliwe katika sherehe za kidini?
Wewe wafikiri nini juu ya dini ambayo hutetea kwamba washiriki wao wa kike walio na umri wa kuanzia miaka 13 hadi 25 watumiwe kwa makusudi ya kuzalisha sana ili vitoto vyao viweze kutolewa katika dhabihu za kumwaga damu?
‘Wafanyiza-sinema watafikiria nini wakati ule mwingine?’ huenda ikawa wafikiri hivyo usomapo habari hii. ‘Ingawaje, haya ni mambo ya kudhania tu,’ huenda wewe ukasema. Lakini, je! ni ya kudhania tu?
Hayo ambayo umesoma sasa hivi ni halisi! Huo si uwazio wa mwandishi wa sinema. Huenda ikawa matukio hayo yalitendeka katika mji wako mwenyewe. Ikiwa bado, kuna hofu zenye kuongezeka kwamba yatatendeka.
Dini ambayo huhusisha kusumbua-sumbua watoto, kuwaingilia kinguvu mabikira wenye kubalehe, ngono za ovyo-ovyo, na utendaji mwingine kama huo, huku mambo hayo yakiwa sehemu ya sherehe zayo za kudhabihu wanyama na wanadamu pia, huitwa Ushetani, au ibada ya Ibilisi. Mazoea ya Ushetani ni ya kiajabu sana, yanayotofautiana sana na kawaida zifaazo, hivi kwamba maofisa na hata raia wengi hukataa kuamini kwamba watu hufanya mambo haya yakiwa sehemu ya ibada yao.
Kiibada hicho cha Ushetani, ambacho miaka michache tu iliyopita kilikuwa na wafuasi wachache kwa kulinganishwa, kimekuwa usumbufu hatari unaoongezeka. “Ushetani ndicho kiibada cha miaka ya ’80,” akaripoti ofisa mmoja wa polisi wa San Francisco. “Ushetani ni sehemu ya uhalifu wa Australia uliopangwa kitengenezo,” akasema mmoja wa wastadi mashuhuri wenye kuchunguza uhalifu katika nchi hiyo. “Mimi naukadiria kuwa kitovu cha wafuasi 20,000 kotekote katika Australia, wenye kuhusika kwa utendaji katika ibada ya Shetani, sherehe mbaya za kufanya ngono, kudhabihu wanyama na labda hata wanadamu. Naamini kwamba harakati hii ndiyo pia husababisha kupotea kwa watoto na yahusika sana katika dawa za kulevya na utumizi najisi wa makaburi.”
Kwa kawaida vikundi vya kiibada cha Shetani huwa vimepangwa kitengenezo kuwa koveni (kikundi cha wachawi), kila moja ikiwa na washiriki kuanzia 9 hadi 13—labda hata zaidi, ikitegemea hali. Wenye mamlaka hukadiria kwamba katika United States, kulikuwako koveni kama 10,000 katika 1946; 48,000 kufikia 1976; na 135,000 kufikia 1985. Haijulikani ni ngapi za koveni hizo huwa hazina jeuri na hujaribu kujitenga mbali na zile zenye jeuri. Kulingana na National Catholic Reporter ya Machi 7, 1986, “kuna koveni 150 zenye utendaji” katika jiji la El Paso, Texas, “kukiwa na wanashetani 2,000 wa umri wote.” Na Bulletin ya Polisi wa Mkoa wa Pennsylvania yaripoti hivi: “Ushetani waongezeka katika Amerika. Ni vigumu siku kupita bila ripoti za vitendo vya jeuri vyenye kuendeshwa na Wanashetani.”
Zaidi ya hilo, Ushetani hujisifia kuwa na ushiriki wa watu wenye kutoka kazi zenye kustahiwa za ulimwengu—madaktari, wanasheria, wafanya biashara, polisi, watawa wa kike, mapadri, wake wa kinyumbani, na wafanya kazi wa kijeshi. Hata hivyo, washiriki wapya wameingizwa kutoka shule za sekondari na nyanja za koleji kuzunguka ulimwengu, kukawa na matokeo ya kutazamisha. Kwa hiyo, katika mahali pengi leo, walio wengi wa washiriki wa koveni ni vikundi vya matineja.
New Zealand Herald la Agosti 26, 1988, liliripoti hivi: “Matineja walio wachanga kufikia miaka 14 walikuwa wakishawishwa waingie katika ulimwengu wa Ushetani.” Ofisa mmoja wa Kanada alisema hivi: “Watoto ambao . . . wanacheza-cheza katika Ushetani ni tisho kwa kadiri iliyo sawa na ile ya (Wanashetani) walio washupavu zaidi.”
Akiripoti juu ya vijana wengi wenye kutumikia kifungo katika kitovu cha uzuilio cha Kanada, mwajiriwa mmoja alisema hivi: “Mimi nastaajabia jinsi walivyo wengi watoto hawa ambao ni Wanashetani. Wao huchanja-chanja vifananisho vya Kishetani juu ya [miili yao] wenyewe, huendesha desturi za kiibada, huamini kikweli katika ibilisi.”
Mfungwa mwenye umri wa miaka 18 alikubali kwamba Ushetani hupendwa sana na marika wake. Kijana mmoja Mkanada alikiri kwamba yeye ni wa kiibada cha Kishetani chenye washiriki 400 kinachoendesha shughuli katika Alberta. “Waabudu-ibilisi walio matineja hawapasi kuachiliwa vyepesi-vyepesi,” akasema stadi Mkanada wa mambo ya uhalifu.
Washiriki wa kiibada hicho hujikabidhi wajibu imara wa kutumikia kikundi hicho muda wa maisha yote, na hiyo hutia ndani nadhiri kali ya kuweka siri. “Washiriki hawaruhusiwi kujitenga na ushirika wa kikundi hicho baada ya kujua wazi utendaji wacho wa mambo mbalimbali ya uhalifu,” laripoti The National Sheriff. “Mshiriki anayevunja orodha ya sheria za siri hutia uhai wake na uhai wa familia yake katika hatari kubwa,” likaongezea gazeti hilo. “[Wao] hupangiliwa mwongozo wa kutofunua siri,” akasema mwanamamlaka mmoja wa Chicago. “Wakifanya hivyo, hupangiliwa mwongozo wa kujiua wenyewe.”
Pia washiriki wa koveni hujaribu kubaki bila kutajwa majina na bila kujulikana na maofisa wenye kutekeleza sheria. Chanzo kimoja kilisema, “Wao huamini kwamba vile vitendo vyao viovu vya uhalifu havitathawabishwa na Shetani ikiwa wanatambulishwa na kushtakiwa na wenye mamlaka.” Hivyo, nasibu tu ndiyo hufanya kiibada cha kishetani kitambuliwe kwamba ndicho kilifanya uhalifu fulani. Katika miaka ya majuzi tu ndipo mashirika fulani ya kutekeleza sheria yamekuja kutambua kwamba ishara zilizoachwa kwenye tamasha ya vifo vilivyotokana na uhalifu vilihusiana na mafumbo ya kiroho yaliyo ya kustaajabisha sana—kwa kielelezo, kurasa za Biblia zikiwa juu-chini huku misalaba ikiwa imechorwa katika mavumbi yaliyo karibu au namba 666 ikiwa imechorwa kwa damu ya yule mhanga.
Ingawa hivyo, kwa nini jeuri itumiwe kwa jina la dini yao? Fikiria sababu fulani za kushtua katika makala inayofuata.
[Sanduku katika ukurasa wa 11]
Ni Vigumu Kuamini—Lakini Ni Kweli
“Bulletin,” kichapo cha sehemu yenye kutafuta watu waliopotea ya Polisi wa Mkoa wa Pennsylvania, huripoti hivi: “Huenda wachunguzi wakaona ni vigumu kuamini zile hadithi za kigeni na za kiajabu juu ya vitendo vya uhalifu vinavyotendwa na watu wanaovaa majoho ya kipadri na kupambwa vifananisho vya ibilisi.”
Hata hivyo, kulingana na “Bulletin:” “Ni vigumu siku kupita bila ripoti za vitendo vya jeuri vyenye kuendeshwa na wanashetani. Katika nchi yote mashirika ya kutekeleza sheria yanapokea ripoti juu ya visa vya kuua wanadamu, kukata-kata viungo vya watu, kushambulia, kujiua, kutumia watoto vibaya na visa vya kukata-kata viungo vya wanyama ambavyo vyahusiana na kiibada cha ushetani.”