Inuko na Anguko la Ushetani
Desturi za kishetani zifanywazo na makuhani wenye kanzu nyeusi katika vijumba vyenye giza, wakisemasema sala juu ya wahanga waliofungwa juu ya madhabahu, huku mishumaa yenye kusinzia ikirusha vivuli vya kuogopesha juu ya kuta wakati ibada ya mungu wao, Shetani, iendeleapo. Wakiwa wamekusanywa na ujuzi wa siri wa fumbo fulani la kishirika lihusianalo na mambo ya kipepo, wale washiriki vijana katika safari hii ya kuingilia mafumbo ya kipepo wafurahia ule mteremesho ujaao mahali hapo. Wakaribiana wakihisi kwamba wao pekee ndio wajuao mambo ya ulimwengu wa roho. Je, ni mtindo wa muda tu, usio na madhara? Au ni ovu la roho waovu linaloienea jamii ya watu leo?
MENGI sana yameandikwa katika magazeti, na vitabu juu ya matendo ya kuogofya ya vidhehebu vya kishetani. Maelezo marefu ya utendaji ulioenea sana wa vikundi vya kishetani vyenye jeuri yametangazwa katika televisheni na redio za kitaifa. Hilo limekuwa tatizo kubwa kwa polisi katika majiji madogo na makubwa pia katika Marekani, Kanada, na Ulaya.
Ushetani una uvutio maalumu kwa vijana wa leo. Mwanzishi wa Kanisa la Shetani aeleza ni kwa nini, kama ilivyoripotiwa katika gazeti ’Teen la Juni 1993: “Badala ya kuamuru washiriki wazuie michocheo yao ya kiasili, sisi hufundisha kwamba waifuate. Hii yatia ndani uchu wa kimwili, tamaa ya kulipa kisasi, msukumo wa kutaka mali za kimwili.”
Lazima iwe Shetani hufurahishwa sana na wazo hili lenye upulizio wa kiibilisi, kwa kuwa ni kinyume cha kanuni za Kikristo zilizopuliziwa na Mungu!
Ushetani unaongezeka. Ni usumbufu unaozidi, lakini kutokomea kwao kwakaribia sana. Mungu wao yuko chini ya hukumu ya kifo. Ndivyo na ulimwengu wa Shetani na wafuasi wao, maana “ulimwengu wote unakaa katika nguvu ya yule mwovu.” (1 Yohana 5:19, New World Translation; Warumi 6:16) Yehova awaambia hivi waabudu wa Shetani na wengine wote ambao kwa kujua au kwa kutojua wanatumikia makusudi ya Shetani: “Yule Mungu apaye amani atamponda-ponda Shetani chini ya miguu yenu upesi.”—Warumi 16:20, NW.
Halafu utakuja wakati ujao gani kwa wanadamu watesekaji kutoka kwa “yule Mungu apaye amani”? Makala tatu zifuatazo zitaonyesha inuko na anguko la Ushetani na hali za duniani zitakazokuwako badala ya huo.