Kwa Nini Ule “Wasiwasi Mwingi”?
PAPA JOHN PAUL 2 alionyesha “kukata tamaa” juu ya mtengano wa harakati ya Askofu Mkuu Lefebvre ya kutetea mapokeo ya Kikatoliki. Alisema, kanisa liliitikia kwa “msononeko mkubwa.”
Padri Mkatoliki Joaquín Ortega, naibu mwandishi wa mkutano wa maaskofu wa Roma Katoliki katika Hispania, alihuzunikia hali hiyo: “Sisi tumetumbukia katika ‘Ukatoliki ulio kama duka la kujichagulia bidhaa.’ Watu wanachukua na kuchagua miongoni mwa kile kinachowafaa kana kwamba mafundisho yetu ni mitungi yenye mboga.”
Askofu Mkuu Lefebvre anashikilia kwamba Baraza la Vatikani la Pili lilisaliti Kanisa Katoliki la kimapokeo, hiyo ikilifungulia kanisa mabadiliko. Hivyo, yeye anahisi, kanisa lilitikisa imani ya Wakatoliki kwamba wao ni wa lile kanisa moja la kweli.
Likitoa muhtasari wa hoja za Lefebvre na wafuasi wake, International Herald Tribune liliandika hivi: “Watetea mapokeo wanabisha kwamba ama kanisa lilikosea kabla ya lile baraza, ama linakosea sasa, lakini haliwezi kuwa sawa njia zote mbili. Ikiwa lilikosea kabla ya lile baraza, wao wanasema, basi huenda likawa lilikuwa na kosa juu ya mafundisho mengine. ‘Sisi tupo hapa kuonyesha wazi ufungamano wetu kwa lile kanisa la nyakati zote,’ akasema askofu mkuu huyo.”
Hata hivyo, Wakatoliki wengi wenye moyo mweupe wanashangaa kama mambo yaliyofundishwa na kuzoewa na kanisa kabla ya ile Vatikani 2 yalikuwa ukweli au yalikuwa kosa.
Wakatoliki Wenye Akili Zilizofunguka Wana Wasiwasi
Wakatoliki wengi wenye akili zilizofunguka wana wasiwasi kwamba zile wanazoziona kuwa hatua za maendeleo zilizochukuliwa kwenye Vatikani 2 zinaharibiwa kwa makusudi kwa sababu ya kisa cha Lefebvre. Wanaogopeshwa na taarifa rasmi za hivi majuzi za Vatikani, kama zile zilizofanywa na Kadinali Ratzinger, mkingaji wa maoni kamili ya Kikatoliki. Yeye ndiye kichwa cha shirika la Vatikani ambalo kwa karne nne lilijulikana kuwa Kundi kwa Ajili ya Baraza Takatifu la Kuhukumu Wazushi.
Kadinali Ratzinger, msimamizi wa Kundi Takatifu kwa Ajili ya Fundisho la ile Imani, katika Roma, alisema hivi: “Mitengano inatokea wakati tu watu wanapoacha kuzifuata maishani na kuacha kuzipenda kweli na thamani fulani za imani ya Kikristo.” Wakatoliki wenye maendeleo wanaogopa kwamba kadinali alikuwa akifikiria “kweli na thamani” zilizokuwa katika Kanisa Katoliki la Kiroma kabla ya ile Vatikani 2.
Ikitamka hofu za jinsi hiyo, makala yenye kichwa “Bei ya Mtengano,” iliyochapishwa katika gazeti la Kifaransa Le Monde, ilisema hivi: “Nani anayejua kama Vatikani—kwa kujua au kwa kutokukubali—haijaanza kuzoea ‘ufuataji mapokeo bila Lefebvre’? . . . Je! sasa [Vatikani] haijaribu kuwavutia makasisi na watu wa kawaida wenye mwelekeo wa kufuata mapokeo ili warudi, na juu ya yote kukazia upya mamlaka na thamani za Kikatoliki mahali ambapo zinafanyiwa ushindani wa peupe, hasa Ulaya ya Magharibi na Amerika ya Kaskazini?”
Wanatheolojia Wasiopatana
Katika Januari 1989, wanatheolojia Wakatoliki 163 kutoka Ujeremani ya Magharibi, Uholanzi, Austria, na Uswisi walitokeza taarifa ambayo sasa inajulikana kuwa Julisho Rasmi la Cologne. Katika majuma yaliyofuata, waliungwa na mamia ya wanatheolojia Wakatoliki kutoka nchi nyinginezo, kutia na Italia. Wimbi la kutopatana lilifyatuka wakati Vatikani ilipomweka rasmi kasisi mmoja anayeshikilia desturi za zamani awe askofu mkuu Mkatoliki wa Cologne, Ujeremani, kinyume cha mapenzi ya baraza la viongozi wa mahali hapo. Lakini mateto yalikuwa zaidi ya kuwekwa rasmi kwa maaskofu wa bawa la kulia (wasiotaka mabadiliko). Yalihusisha hatua za nidhamu za Vatikani ili kunyamazisha wanatheolojia walioonyesha “fikira ya kitheolojia ambayo Baraza la Vatikani la Pili lilikazia.” Pia wanatheolojia hao walitilia shaka haki ya papa ya kulazimisha maoni yake “katika mambo ya mafundisho,” hasa kuhusu kudhibiti uzazi.
Akiitikia julisho rasmi hili, Kadinali Ratzinger alisema wazi kwamba wale wanaokataa maoni ya Vatikani juu ya kudhibiti uzazi na talaka wanatoa fasiri yenye makosa juu ya “dhamiri” na “uhuru” na wanachafua fundisho la kanisa la kimapokeo. Hivi majuzi alikumbusha makasisi wa United States kwamba hawapaswi kuacha fundisho lao liongozwe na “tamasha isiyopatana” ya wanatheolojia.
Wakatoliki Wengi Wamefadhaika
Mwanatheolojia mmoja Mfaransa alijulisha rasmi hivi katika mahoji mamoja pamoja na Le Monde: “Lingekuwa kosa kudai . . . kwamba mzozo huu unahusu wanatheolojia peke yao. Wao wanaeleza tu wasiwasi wa kina kirefu wa Wakatoliki wengi sana.”
Wakatoliki wengi wenye moyo mweupe wanashangaa kama haikuwa kwamba askofu mkuu mwasi Lefebvre, ingawa aliondoshwa katika ushirika, ‘alishindwa pigano moja lakini akaishinda vita.’ Kwa uhakika, miruhusio fulani inafanywa kwa wafuasi wa Lefebvre kwa jitihada ya kuwavuta warudi ndani ya zizi. Misa inasemwa tena kwa Kilatini katika makanisa mengi ya Kikatoliki, na maaskofu wanaoshikilia desturi za zamani wanawekwa kwenye vyeo. Kwa kupendeza, Wakatoliki watetea mapokeo wanauliza hivi: ‘Kwa nini Monsinya Lefebvre aliondoshwa katika ushirika na hali mapadri Wakatoliki katika Uholanzi wanaobariki “ndoa” za wagoni-jinsia-moja na mapadri wa Amerika ya Kusini wanaotetea theolojia ya ukombozi wa kufanya mapinduzi wangali sehemu ya kanisa?’
Yote haya yanaacha Wakatoliki wengi wakiwa wamevurugika. Mkatoliki Mfaransa mmoja aliliandikia hivi gazeti la kila siku la Kikatoliki La Croix (Ule Msalaba): “Wakristo wa kawaida, kama mimi mwenyewe, wanateseka kwa sababu wale wanaohusika [katika migawanyiko ya kanisa] hawazungumzi mambo na kufikia makubaliano. Watu fulani wanaondoka pole-po-o-le kwenye zoea la kidini, ikiwa si kutoka kwenye Kanisa.”
Bila shaka, watu hao hawawezi kuelewa kwa nini lile ambalo wanalifikiria kuwa ndilo kanisa moja la kweli limegawanyika sana. Hata padri Mkatoliki René Laurentin aliuliza hivi: “Kwa nini migawanyiko hii miongoni mwa Wakristo?” Acheni tufikirie kifupi sababu fulani za kuwako kwayo.
[Blabu katika ukurasa wa 7]
“Watetea mapokeo wanabisha kwamba ama kanisa lilikosea kabla ya lile baraza, ama linakosea sasa, lakini haliwezi kuwa sawa njia zote mbili.”—International Herald Tribune.