Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 4/8 kur. 21-23
  • Je! Nitafute Kazi ya Baada ya Saa za Shule?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Nitafute Kazi ya Baada ya Saa za Shule?
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Nitafanya Nini na Pesa Hizo?
  • Shule na Kazi
  • Kazi na Familia Yako
  • Kazi Yako na Hali Yako ya Kiroho
  • Je! Kazi ya Baada ya Saa za Shule Itanisaidia Nikue?
    Amkeni!—1992
  • Je! Nifanye Kazi Ningali Shuleni?
    Amkeni!—1992
  • Naweza Kuchumaje Pesa?
    Amkeni!—1998
  • Nitapata Pesa Wapi?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 4/8 kur. 21-23

Vijana Wanauliza. . .

Je! Nitafute Kazi ya Baada ya Saa za Shule?

“Amkeni!”: Ni nini kilichokufanya utafute kazi ya baada ya saa za shule?

Eric: Nilikuwa nikiishi nyumbani, nami nilitaka kusaidia wazazi wangu kifedha.

Olga: Ni kujitegemea. Nilitaka pesa zangu mwenyewe.

Michelé: Tayari nilikuwa nikipewa pesa kwa ukawaida, lakini nilitaka ujuzi wa kazi.

Duane: Mimi sikufanya kazi kwa sababu ya pesa. Nilifanya kazi ili nimsaidie mjomba wangu aliyekuwa na biashara ya kupaka rangi, uashi, na kadhalika.

Anthony: Nilifanya kazi kwa sababu nilitaka niweze kununua nguo.

“Amkeni!”: Je, mama yako hakuwa akikununulia nguo?

Anthony: Hakuninunulia aina ya nguo nilizotaka.

JE! WEWE unafikiria kupata kazi ya baada ya saa za shule? Labda ungependa tu kupata pesa za mfukoni zaidi kidogo, na kazi yaonekana kuwa njia ya haraka zaidi ya kuzipata.

Kazi yaweza kuwa na manufaa yazo.a Yaweza kumfunza kijana achukue daraka. Yaweza kutoa ujuzi wenye thamani na stadi zenye kutumika. Hata hivyo, si sehemu zote za kufanya kazi zilizo na manufaa, na kabla ya kuanza kazi fulani, wapaswa uhesabu gharama kwa uangalifu.—Linganisha Luka 14:28; 1 Wakorintho 10:23.

Nitafanya Nini na Pesa Hizo?

Vijana wengi hufanya kazi ili kuwatolea wazazi wao msaada wa kifedha unaohitajiwa. Hata hivyo, David L. Manning mwalimu wa shule ya upili aeleza kwamba “kichocheo cha msingi cha kufanya kazi isiyo ya wakati wote chaonekana kuwa ni kufurahia mapendezi ya kibinafsi.” Kwa kweli sehemu kubwa ya pesa zinazochumwa na matineja hutumiwa hasa, si kwa kuwekea akiba au kwa gharama za familia, bali kwa vitu vya anasa ambavyo ni kuanzia mifumo bora ya vifaa vya kimuziki na tikiti za kuhudhuria maonyesho ya muziki hadi viatu ghali vya kuchezea. Hatimaye, pesa zilizochumwa hutumiwa ovyo mara nyingi.

“Eti nilifanya nini na pesa zangu?” akajibu kijana Michelé wakati ripota wa Amkeni! alipouliza kikundi cha vijana walifanya nini na pesa walizochuma katika kazi zao. “Sijui,” akakiri. “Sikuweka zozote akibani. Nadhani nilizitumia kwa kwenda mahali fulani-fulani. Sinema—nilikuwa nikizienda kila mwisho-juma. Na viatu. Kitu nikipendacho ni viatu. Nimelipa kufikia dola 250 kwa jozi moja.” Kijana Olga alijibu vivyo hivyo: “Nadhani nilitumia pesa zangu zote. Kadiri uchumavyo zaidi ndivyo utumiavyo zaidi. Lakini sijui hata kidogo zilienda wapi.”

“Mtu ana faida gani ya kazi yake yote aifanyayo chini ya jua?” akauliza Sulemani. (Mhubiri 1:3) Na usipokuwa na sababu nzuri ya kufanya kazi, usipokuwa na mpango hususa wa jinsi utakavyotumia—au kuweka akibani—pesa utakazochuma, kazi yako ngumu yaweza vivyo hivyo kuthibitika kuwa bila mazao, ya ubatili.b ‘Lakini kuna madhara gani kuzitumia kwa vitu ninavyotaka?’ huenda ukauliza.

Ni jambo moja kufanya kazi kwa ajili ya mahitaji ya kikweli. Lakini kufanya kazi kwa muda mrefu na kwa bidii nyingi kwa ajili ya tamaa zisizo za maana ni mtego. Kwaweza kusababisha tamaa ya vitu vya kimwili isiyoleta afya njema. (Linganisha 1 Timotheo 6:8, 9.) Kwaweza kukuza roho ya kujifikiria mwenyewe, ya mimi-kwanza ambayo huenda kinyume cha roho ya Kikristo ya kutoa. (Matendo 20:35) Kwa hiyo kabla ya kutafuta kazi, je, isingekuwa bora zaidi kuthibitisha kama inahitajiwa kikweli?

Shule na Kazi

Jambo jingine la kufikiria ni vile kufanya kazi kungeathiri masomo yako. “Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili,” akasema Yesu. (Mathayo 6:24) Kanuni hiyo hutumika kwa wanafunzi wengi ambao hujipata wenyewe katika mgongano baina ya shule na kazi.

Utafiti mbalimbali huonyesha kwamba vijana wanaofanya kazi huelekea zaidi kutokuwa shuleni kuliko wale wasiofanya kazi. Na wakati wapo shuleni, wao mara nyingi si wasikivu. “Nilikuwa natoka shuleni saa sita nami nilifanya kazi ya ukarani kuanzia saa saba hadi saa kumi na moja,” aeleza kijana Olga. Tokeo? “Nilichoka. Shule na kazi zakuchosha.” Si ajabu basi, kwamba alama za mitihani za wanafunzi wengi hushuka vibaya wanapoanza kazi. Wengine hata huanguka.

“Nilipaswa kwenda kwenye shule ya kiangazi,” akumbuka Anthony, aliyeanguka mtihani alipokuwa akifanya kazi kwenye kiwanda baada ya shule. Hata hivyo, Anthony aliendelea kufanya kazi muda wote wa kiangazi. Tokeo? “Nilianguka mtihani shule ya kiangazi pia nikahitaji kurudia darasa moja.” Ni kweli, wanafunzi fulani werevu wanaweza kudumisha alama nzuri za mitihani. Michelé akumbuka hivi: “Nilikuwa tu nikimsikiliza mwalimu wangu na kushika yale aliyokuwa akisema, na kupita. Sikulazimika kamwe kujifunza [kwa bidii].” Hata hivyo, kuna tofauti kubwa kati ya kuweza tu kupitia shuleni na kujiingiza kabisa katika kujifunza kweli kweli.—Linganisha 1 Timotheo 4:15.

Kwa hiyo kama unafikiria kuajiriwa kazi, jiulize hivi: ‘Je, nitaweza kutoa wakati wa kutosha kwa kazi za shule ambazo nimegawiwa kufanya nyumbani? Je, nitaweza kupata wakati wa kutosha wa kupumzika na kulala?’ (Mhubiri 4:6) Mengi yatategemea aina ya kazi na ratiba. Lakini kazi ikizuia masomo yako, je, kwa kweli inafaa?

Kazi na Familia Yako

Jambo la kuhangaikia pia ni jinsi kufanya kazi kutakavyoathiri uhusiano wako na washiriki wa familia yako. “Utafiti wetu wenyewe unaonyesha . . . kwamba wabalehe wanaofanya kazi huwa na wakati mchache katika utendaji mbalimbali wa familia kuliko wenzao wasiofanya kazi,” wasema wachunguzi Laurence Steinberg na Ellen Greenberger. Kwa mfano, “vijana wengi wanaofanya kazi huripoti kwamba wao hula chakula cha jioni pamoja na familia zao mara chache zaidi (hivyo wakipoteza mojawapo kati ya zile nyakati chache ambazo katika hizo wazazi na watoto huweza ‘kujuliana hali ya sasa’ kuhusu shughuli za mmoja na mwenzake).”

Wakati wa chakula ulikuwa sehemu ya maana ya maisha ya familia katika nyakati za Biblia na huendelea kuwa hivyo miongoni mwa watu wa Mungu leo. (Linganisha Mithali 15:17.) Miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, familia nyingi hutumia chakula cha asubuhi au cha jioni kuwa pindi ya kuzungumzia mambo ya kiroho. Je, kazi ya baada ya shule itakuzuia usishiriki?

Vijana wenye kufanya kazi huenda pia wakaanza kuhisi kutowategemea wazazi wao sana. Wengine hata husababu kwamba kwa kuwa wana pesa zao wenyewe, wanaweza kupunguza ujitiisho wao chini ya mamlaka ya wazazi wao. Hata hivyo, hundi ya malipo haikuweki huru kutoka wajibu wako wa Kimaandiko wa ‘kusikiliza nidhamu ya baba’ au ‘kutii sheria ya mama yako.’ (Mithali 1:8, NW) Wazazi, kwa mfano, wana haki yote ya kuamua ni kiasi gani cha pesa zako zilizochumwa kwa kazi ngumu chapaswa kitumiwe kwa gharama za familia. Vyovyote iwavyo, karibu pesa zao zote zatumiwa hivyo.

Ukiamua kufanya kazi, kwa nini usionyeshe ukomavu wako na kupendezwa kwako katika masilahi ya familia kwa kuwauliza wazazi wako kiasi unachoweza kuchangia mambo ya fedha ya familia?

Kazi Yako na Hali Yako ya Kiroho

Jambo la kufikiriwa zaidi ya yote ni jinsi kufanya kazi kwaweza kuathiri hali yako ya kiroho. Steinberg na Greenberger wanaripoti kwamba kuwa katika mahali pa kufanyia kazi mara nyingi hutokeza namna mbalimbali za ‘tabia ya kuasi’ za vijana, kama vile kuiba kazini au kuwa mdanganyifu shuleni. Vijana wengine hata hujitiisha kwa msongo wa marika na kupunguzia marafiki bei za bidhaa bila ruhusa, au kuiba kwa ajili yao. Misongo ya kazi (na kuwa na pesa taslimu) huwasukuma vijana wengi kwenye matumizi mabaya ya vileo na dawa za kulevya.

Ni kweli, ukiwa na kanuni za Kikristo, hata hungefikiria kamwe kufanya mambo kama hayo. Hata hivyo, kuwa na kazi kwaweza kufunua kijana kwa “mashirika mabaya” kwa kiasi kikubwa sana. (1 Wakorintho 15:33, NW) Je, wewe uko tayari kushughulikia msongo kama huo? Wakati unapokuwa shuleni, je, wewe umekuwa ‘ukienenda kwa hekima mbele yao walio nje’ kwa kuepuka ushirika usiojenga? (Wakolosai 4:5) Ikiwa umeonyesha udhaifu fulani kuhusu jambo hilo, je, wewe kwa kweli uko tayari kukabili misongo mikubwa zaidi ya kazini?

Ratiba ya kazi yenye kuhitaji juhudi sana huenda pia ikafanya iwe vigumu kwako kuifuata kawaida ya Kikristo ya mikutano, funzo la Biblia la kibinafsi, na kushiriki katika huduma ya Kikristo. “Nimekosa mikutano kwa sababu nilikuwa nimechoka baada ya siku ya shule na kazi,” asema Michelé.

Hivyo uamuzi wa kupata kazi ya kufanya baada ya saa za shule ni mzito. Ni lazima mambo yote yanayohusika yafikiriwe kwa uangalifu. Ongea mambo pamoja na wazazi wako au pamoja na Mkristo mkomavu. Kama inaonwa kwamba ni lazima ufanye kazi, jaribu sana kudumisha usawaziko wako. Fanya ratiba inayokuruhusu utoe uangalifu wa kutosha kwa masomo yako na kwa ukuzi wako wa kiroho. Kama hiyo haiwezekani, fikiria njia nyinginezo za kuchuma pesa. Labda kuna kazi kubwa za nyumbani ambazo huenda wazazi wako wangekuwa tayari kukulipa uzifanye. Vijana wengine huanza biashara ndogo, kama vile kukata nyasi au kutunza watoto, zinazowaruhusu wachume pesa kwa wakati wao wenyewe ufaao.

Lakini vipi vijana katika nchi zilizo maskini zaidi ambao hawana hiari ila kufanya kazi? Makala ya wakati ujao itazungumzia hali yao.

[Maelezo ya Chini]

a Ona makala “Je! Kazi ya Baada ya Saa za Shule Itanisaidia Nikue?” katika toleo hili.

b Ona matoleo Desemba 8, 1989, na Januari 22, 1989 (la Kiingereza) ya Amkeni! kupata madokezo juu ya jinsi ya kushughulikia pesa.

[Blabu katika ukurasa wa 23]

“Kichocheo cha msingi cha kufanya kazi isiyo ya wakati

wote chaonekana kuwa ni kufurahia mapendezi ya kibinafsi”

[Picha katika ukurasa wa 22]

Je! unafanya kazi ili ulipie gharama za kikweli au ili utosheleze upendo wa vitu vya kimwili?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki