Vijana Wanauliza. . .
Je! Nifanye Kazi Ningali Shuleni?
SIKU za shule ni zenye shughuli nyingi kwa vijana walio wengi. Mafundisho ya darasa huchukua sehemu kubwa kila siku ya masomo. Kazi ya ziada ya shule na kusoma hubana jioni zote. Na kati ya hayo kuna kazi nyingi za nyumbani ambazo zahitaji uangalifu.a
Katika nchi za Magharibi vijana wenye umri wa shule kwa kawaida wanaweza kutazamia mwisho juma kuwa wakati wa michezo na pumziko. Lakini katika sehemu nyingi za dunia, miisho juma si ya mapumziko hata kidogo. Katika sehemu za mashambani za Afrika, kwa mfano, vijana kwa kawaida hutumia miisho juma yao kuwasaidia wazazi wao katika shamba, kujazia wakati uliopotezwa shuleni wakati wa kwenda shuleni juma hilo. Na miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, vijana wana daraka lililoongezwa la kushiriki katika kazi ya kuhubiri mlango kwa mlango na kwenda kwenye mikutano ya Kikristo.—Waebrania 10:23-25.
Huenda kwa sababu hiyo isionekane kwamba vijana wa Kiafrika wangetaka kuchukua mzigo wa ziada wa kazi ya kimwili. Lakini vijana wengi wa jinsi hiyo wanafanya kazi, tena katika njia mbalimbali: kulima mashamba yao wenyewe na kuuza mazao, kutengeneza nguo kwa kitanda cha mfumi, au kutengeneza vikapu vya kuuza sokoni. Wengine hata wanavua samaki, kuuza magazeti, na kuchuma au kuuza matunda.
Ingawa hivyo, kwa nini vijana hawa wanafanya kazi ya kimwili? Je! inamaanisha kwa lazima kwamba wewe wapaswa ufanye ivyo hivyo?
Sababu ya Wao Kufanya Kazi
Vijana wengine yaelekea inawabidi kufanya kazi kwa sababu ya hali zisizozuilika, kama vile kifo cha mzazi. (Hii yaweza kumwacha kijana bila mdhamini kwa masomo yake.) Kwa upande mwingine, vijana wengine hufanya kazi ili kwa kadiri fulani wawe huru kutotegemea wazazi wao.
Fikiria Kofi, mwanamume kijana katika Ghana. Alipokuwa katika chuo cha ufundi, alifanya kazi akiwa kibarua wa shamba muda wa saa mbili kila siku baada ya shule.b Kofi aeleza: “Wazazi wangu walikuwa wameniandalia mahitaji yangu muda wote wa shule ya msingi. Lakini sikutaka kuendelea kuwategemea kwa kila uhitaji wangu. Kwa hivyo nikaanza kazi ya kimwili. Nilihisi nikiwa mwenye furaha zaidi kuweza kujinunulia vifaa vya kuandikia na kulipia gharama zangu za kusafiri.”
Moses ndugu yake Kofi vilevile alikuwa na kazi. Alipokuwa katika shule ya upili, Moses alifundisha watoto wa shule wachanga faraghani. Lakini ingawa mshahara wa Kofi kwa kufaa ulitumika kwa mahitaji yake mwenyewe, nyingine za pesa za Moses zilitumika kuendeleza familia yao. Kwa nini? Akiwa wa familia ya watoto wanane, alitoa sababu hivi: “Kufanya kwangu kazi ya nusu wakati kuliwapa wazazi wangu kadiri fulani ya msaada katika kuwatunza wengine wa ndugu na dada zangu.” Anakubali pia ile hisi ya kuridhika ya kuweza kujinunulia vitu mwenyewe.
Kuwasaidia wazazi wako kifedha wakati kuna uhitaji kikweli kunaweza kuwa njia moja ya kutoa heshima inayowastahili. (Waefeso 6:1, 2) Ingawa hivyo, wakati ule ule, hakuna ubaya wa kufanya kazi ili kutumia pesa zako mwenyewe.
Kuwa na kazi pia kwaweza kuingiza polepole hisi ya daraka kwa kijana. Kunaweza kusaidia kijana ajifunze ustadi ambao baadaye unaweza kutumiwa kutegemeza familia. Yesu Kristo mwenyewe, kwa mfano, yaonekana alijifunza kazi ya seremala alipokuwa kijana pamoja na baba yake mlezi. (Mathayo 13:55; Marko 6:3) Hata hivyo, “muda ubakio si mwingi” kwa ulimwengu huu, na kijana mwenye hekima anahakikisha kwamba wakati wake unatumiwa kwa njia yenye faida. (1 Wakorintho 7:29; Waefeso 5:16) Kwa hiyo kabla ya kuanza kazi fulani, ni lazima upime mambo yote yanayohusika—kutia ndani na madhumuni yako mwenyewe.
Kuihesabu Gharama
Maswali fulani unayopaswa kufikiria ni: Wazazi wangu wanahitaji kikweli au hata wanataka usaidizi wangu wa kifedha? Au wako tayari kutosheka na machache kifedha ili nifanye kazi yangu ya shule na maendeleo ya kiroho? Je! kweli nahitaji fedha za ziada, au ninaitikia “tamaa ya mwili na tamaa ya macho na wonyesho mshaufu wa mali za maisha za mtu”?—1 Yohana 2:16, NW.
Mtu mwenye hekima sulemani aliona hivi: “Nimejifunza pia kwa nini watu hufanya kazi ngumu ili kufanikiwa: ni kwa sababu wanaonea wivu vitu ambavyo jirani zao wanavyo. Lakini ni bure. Ni kama kufukuza upepo. . . . Ni afadhali kuwa na vichache tu, pamoja na amani ya akili, kuliko kushughulika wakati wote kwa mikono yote miwili, kujaribu kushika upepo.”—Mhubiri 4:4-6, Today’s English Version.
Jambo lingine la kufikiria ni matokeo ambayo kazi italeta juu ya masomo yako. Kofi, aliyetajwa mapema, akumbuka hivi: “Katika kipindi cha mwaka wangu wa kwanza katika shule ya ufundi wakati ambapo sikufanya kazi ya kuajiriwa, masomo yangu shuleni yalikuwa na matokeo mazuri ajabu. Halafu ukaja mwaka wa pili ambapo nilianza kazi ya kuajiriwa, na ubora wa kazi yangu ya shule ukaanza kushuka. Bado niliweza kuwa juu ya wastani, lakini ilikuwa yenye kuchosha sana.” Lenye kupendeza, uchunguzi mmoja wa utafiti ulioongozwa huko United States ulipata ya kwamba “kufanya kazi huongoza kwenye mshuko wa matokeo ya shule na hupunguza utendaji wa vijana shuleni.”
Unamkumbuka Moses ndugu ya Kofi, ambaye alikuwa na kazi ya kufundisha? Yeye akubali: “Mtu asipokuwa mwangalifu sana, anaweza kuanza kuchukua wanafunzi wengi zaidi ya wanaoweza kufundishwa katika kiwango cha wakati unaopatikana.” Mawuli, mwanamume mwingine Mwafrika, alifanya kazi ya nusu siku akiwa mvuvi. Anasema hivi: “Kulikuwa na shawishi kubwa wakati samaki wengi walipovuliwa kwenye ufuo. Shawishi lilikuwa ni kuacha vitabu na kwenda kuchuma pesa zaidi. Wavulana wengi kijijini walifanya hivyo na wakaacha shule.”
Shule pamoja na kazi zaweza kuondoa nguvu ya kijana hata kufikia kumwathiri vibaya kiroho. Inaweza kuwa vigumu kwa yeye kuhudhuria mikutano ya Kikristo au kukaza fikira anapokuwa huko. Funzo la kibinafsi la Biblia na vichapo vyenye msingi wa Biblia laweza kuwekwa kando.
Kuendeleza Usawaziko Wako
Hata hivyo, baada ya kupima mambo yote, wewe na wazazi wako huenda mkaamua kwamba kufanya kwako aina ya kazi fulani kungekuwa na manufaa. Unaweza kuitumiaje hali hiyo kwa faida bora?
Kujipa nidhamu ni muhimu sana. Mtume Paulo alinena juu ya jitihada zake, akisema: “Nautesa mwili wangu na kuutumikisha.” (1 Wakorintho 9:27) Itahitaji kujitia nidhamu ili wewe uweke akiba—wala si kutapanya—pesa unazochuma. Pia itahitaji kujitia nidhamu ili utumie ifaavyo wakati wako uliobaki. Bila shaka, starehe na pumziko la kutosha zinafaa na zinaweza kuongezea kazi yenye matokeo. Lakini angalia mapendezi yako ya kupishia wakati na vitumbuizo yasije yakasonga masomeo-nyumbani uliyopewa shuleni na hata mambo ya kiroho.
Utahitajiwa basi kufanya orodha yenye mafaa halisi ya vipindi vya kujifunza—na kuifuata kabisa. Kwa mfano, inaweza kuwa bora zaidi kuanza masomeo-nyumbani uliyopewa shuleni mara tu iwezekanapo baada ya kurudi kutoka kazini, si kungojea hadi baada ya chakula cha jioni wakati ambapo huenda ukahisi ukisinzia mno. Wengine hupendelea kwenda kulala mapema na kuangalia masomo yao mara tu asubuhi ifikapo. Hata iweje, fanya masomo yako yawe yenye matokeo iwezekanavyo. Epuka kufungulia muziki au kujiingiza katika shughuli nyingine zenye kukengeusha fikira. Masomeo-nyumbani uliyopewa shuleni huenda yakanyooka pia ikiwa utasikiliza kwa uangalifu darasani, kuandika mambo makuu na habari zenye kutegemeza.—Linganisha Luka 8:18.
Jambo la maana zaidi ya yote, hata hivyo, ni mahitaji yako ya kiroho. (Mathayo 5:3) Ili haya yatimizwe, ni lazima uweke kando wakati pia wa funzo la kibinafsi la Biblia, wa mikutano ya Kikristo, na wa kushiriki huduma ya peupe. Ni kweli, kufanya kazi na kwenda shule kwadai mambo mengi. Lakini ikiwa ni lazima ufanye yote mawili, weka mambo ya kiroho kwanza. Sali daima kwa Yehova ili akusaidie ushike usawaziko wako wa kiroho. Ikiwa kazi yaamuliwa ifanywe, kwa kuongezea ile ya shule, yeye anaweza kukusaidia uiweze mibano ya hali hiyo.—Isaya 40:29-31.
[Maelezo ya Chini]
a Makala hii inashughulika hasa na hali inayokabiliwa na vijana katika nchi zinazoendelea kustawi. Hata hivyo, madokezo yaliyo hapa yana msingi wa kanuni za Biblia na hivyo zitathibitika kuwa zenye msaada kwa vijana wote kuzunguka ulimwengu.
b Katika nchi nyingine, baada ya shule ya msingi kijana ana chaguo la kuingia katika shule ya upili (ambayo hufunza masomo mengi mbalimbali) au katika shule ya ufundi.
[Picha katika ukurasa wa 28]
Vijana fulani Waafrika hufanya kazi za baada ya shule. Lakini ni nini faida na hasara za kufanya hivyo?