Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 4/8 kur. 15-17
  • Je! Kazi ya Baada ya Saa za Shule Itanisaidia Nikue?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Kazi ya Baada ya Saa za Shule Itanisaidia Nikue?
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kufanya Kazi—Manufaa
  • Mtu kwa Kweli Hujifunza Kiasi Gani?
  • “Usitawi wa Kabla ya Wakati Unaofaa”
  • Je! Nitafute Kazi ya Baada ya Saa za Shule?
    Amkeni!—1992
  • Je! Nifanye Kazi Ningali Shuleni?
    Amkeni!—1992
  • Naweza Kuchumaje Pesa?
    Amkeni!—1998
  • Kuna Ubaya Gani Kuchuma Pesa?
    Amkeni!—1997
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 4/8 kur. 15-17

Vijana Wanauliza. . .

Je! Kazi ya Baada ya Saa za Shule Itanisaidia Nikue?

WAWILI kati ya watatu—hiyo ndiyo idadi ya matineja katika United States ambao wanafanya kazi kwa wakati huu. Nao wanafanya kazi kati ya saa 16 hadi 20 kila juma!a

Kwa nini vijana walio wengi mno wanamiminikia kazi? Brian mwenye umri wa miaka 16 aeleza hivi: “Katika hali yangu ni lazima nifanye [kazi]. Mamangu na babangu wametalikiana na ni lazima nisaidie mamangu kwa njia yoyote niwezayo.” Familia nyingi hali kadhalika zinahitaji msaada wa kiuchumi. Na hata kama kijana hachangii moja kwa moja gharama za kinyumbani, akilipia tu nguo zake mwenyewe au vitu vinginevyo vya kibinafsi, kwa kufaa hilo laweza kuwaondolea wazazi wake kadiri fulani ya mbano wa kiuchumi.

Ni kweli, vijana wengi hufanya kazi ili kujifurahisha kwa nguo ghali, viatu, au vyakula vinavyotayarishwa upesi. Lakini kwa vijana fulani, kazi humaanisha hasa hatua kubwa kuelekea ukomavu. Suzanne mwenye umri wa miaka 19 aliandika hivi kwenye gazeti Seventeen: “Ninafanya kazi kwa sababu ninaonea shangwe kujitegemea. Si lazima nitegemee wazazi wangu wanilipie mahitaji yangu . . . Wazazi wanaweza kuwapa watoto wao pesa, lakini hawawezi kuwapa hisia ya uradhi inayotokana na kuchuma kitu.” Na labda unahisi jinsi iyo hiyo—kwamba kuwa na kazi kungekuwa ono zuri, kwamba kutakusaidia uwe mtu mzima kwa haraka zaidi. Lakini je, kutafanya hivyo kweli kweli?

Kufanya Kazi—Manufaa

Biblia hulaumu uvivu. “Nafsi ya mtu mvivu hutamani asipate kitu,” yasema Mithali 13:4. “Bali nafsi ya mwenye bidii itanenepeshwa.” Kwa hiyo ukihitaji kweli kweli kitu ambacho kinagharimu zaidi ya kile wazazi wako wataka, au waweza, kulipia, huenda wazo hilo la kufanya kazi kwa bidii ili uweze kukinunua mwenyewe likawa linafaa.

Juu ya hayo wengine hutoa hoja kwamba kufanya kazi kunaweza kufundisha kijana kuhusu maisha katika ulimwengu halisi. Ellen Greenberger na Laurence Steinberg wamefanya utafiti mpana na unaojulikana sana juu ya habari ya wanafunzi wanaofanya kazi. Walipata kwamba vijana kama hao “hujifunza juu ya uendeshaji wa biashara, matumizi ya pesa, na jinsi ya kuhesabia wateja.” Kazi yaweza pia kufunulia kijana si jinsi ilivyo tu kufanya kazi pamoja na watu wazima bali pia jinsi mibano na madaraka ya watu wazima ilivyo. Huenda akapaswa kujifunza jinsi ya kufanya kazi chini ya bwana mkubwa ‘aliye mgumu kufurahishwa’ au mwenye hasira mbaya, au jinsi ya kushughulika kwa fadhili pamoja na wanunuzi wakali—na wafanyakazi wenzi. (1 Petro 2:18) “Nilikuwa kijana mchanga zaidi kazini,” akumbuka Anthony, “na kila mtu alinitatiza sana. Lakini nilijifunza jinsi ya kushughulika na watu.”

Kufanya kazi kwaweza pia kufunza kijana stadi za kufanya mambo na mazoea ya kazi, kama vile kutochelewa, jambo ambalo laweza kusaidia baadaye maishani. (Linganisha Mithali 22:29.) “Nilijifunza kuchukua madaraka,” asema kijana mwanamume aitwaye Eric. “Kufanya kazi pamoja na mjomba wangu kulinifunza kufanya kazi yenye ubora,” aongeza Duane. “Yeye alikazia unadhifu, na ikiwa kila kitu hakikutokea kikamilifu, tulikirudia.” Olga, aliyefanya kazi ya ukarani alipokuwa shuleni, aongeza hivi: “Nilipata ujuzi mzuri wa kazi. Na kulazimika kuongea sana kwa simu kulinifunza kutumia usemi mzuri.”

Kufanya kazi kwaweza pia kukufunza fahari inayotokana na kutimiza jambo. Mfalme Solomoni mwenye hekima alisema hivi: “Mwanadamu hapati jema kupita kula na kunywa, na kuiburudisha roho yake kwa mema katika kazi yake. Hayo nayo naliona ya kwamba hutoka mkononi mwa Mungu.”—Mhubiri 2:24.

Mtu kwa Kweli Hujifunza Kiasi Gani?

Hata hivyo, wengi huamini kwamba kazi za leo hazisaidii kijana sana akue. Katika nyakati zilizopita, vijana wafanya kazi walijifunza kazi fulani au angalau stadi zenye mafaa. Hata hivyo, leo, vijana wengi (hasa katika United States) hufanya kazi katika mikahawa yenye vyakula vinavyotayarishwa upesi au katika sehemu nyinginezo za kuhudumia watu ambapo kazi inahusika na shughuli kama kujaza hambaga katika visanduku au kujumlisha pesa za mauzo katika vitabu vya fedha. Wengi hushuku thamani ya kudumu ya kazi kama hiyo. Greenberger na Steinberg waomboleza hivi: “Kijana wa kawaida hutumia chini ya asilimia 10 ya wakati wake kazini—karibu dakika 5 tu kwa kila saa—katika utendaji mbalimbali kama vile kusoma, kuandika, na hesabu. . . . Kazi zilizo nyingi kwa kawaida huwa bila shughuli tofauti-tofauti, huwa na utendaji wa kufuata kawaida mno, na huwa zenye shughuli za kurudia-rudia daima zisizopendeza kabisa.”

Makala katika The Wall Street Journal inataarifu hivi: ‘Walio wengi wa matineja wanaofanya kazi hawajifunzi kitu chochote zaidi ya kuwapo tu kazini. Tekinolojia imewageuza kuwa karibu watu wafanyao kazi bila kufikiri wala kutumia akili. Mashine za kukagua hesabu na mashine za hali ya juu huhesabu pesa na kurudisha chenji. Kwenye mahali pa vyakula vinavyotayarishwa upesi, vyombo vya kujipikia na kujiwekea wakati vyenyewe huondoa uwezekano wowote kabisa wa kijana kujifunza ustadi wowote wa upishi.’ Kazi kama hizo bila shaka huandaa huduma zenye kuhitajika na zenye thamani. Hata hivyo, huenda zisisaidie sana kumtayarisha kijana kwa kazi za watu wazima.

Lakini vipi juu ya ustadi wa kufanya kazi pamoja na watu wazima? Greenberger na Steinberg husema hivi: “Mahali pa kazi ambapo vijana huajiriwa kazi pamekuja kuwa penye ubaguzi wa umri kwa kadiri yenye kuongezeka. Badala ya kufanya kazi pamoja na watu wazima, . . . inaelekea sana kwamba vijana wa leo watafanya kazi pamoja na wabalehe wengineo.” The Wall Street Journal huita mahali pa kazi kama hapo “mitaa ya wabalehe.”

“Usitawi wa Kabla ya Wakati Unaofaa”

Vijana wengi katika United States huchuma zaidi ya dola 200 kila mwezi kazini mwao. Je! kushughulika na pesa kama hizo hakungekuwa ustadi wa thamani? Fikiria utafiti wa wanafunzi wa shule za sekondari kutoka shule tofauti-tofauti zaidi ya elfu moja walioajiriwa kazi. Iligunduliwa kwamba robo tatu yao hawakuchanga chochote kwa fedha za familia! Karibu asilimia 60 yao hawakuweka chochote akiba! Bila kulemewa na malipo ya kodi ya nyumba, bima, na milo, walio wengi walitumia kile walichochuma kuwa pesa za kununulia vitu vidogo-vidogo—kutumia jinsi walivyopenda.

Jerald G. Bachman wa Taasisi ya Uchunguzi wa Kijamii asema kwamba wakati “matineja wanapokuwa na pesa nyingi za kutosha kutumia wapendavyo,” huo ni “usitawi [au utajiri] wa kabla ya wakati unaofaa.” Kwa sababu gani hivyo? Bachman aeleza hivi: “Wanafunzi wengi wa shule ya sekondari wanapangia pesa vitu vya anasa ambavyo huenda ikawa hawataweza kuendeleza miaka mitano baadaye, wakati mapato wanayochuma yatapasa kutumiwa kwa vitu visivyo vya anasa kama chakula na kodi ya nyumba.” Ndiyo, badala ya kufunza kijana madaraka ya kifedha, kuwa na pesa nyingi mno kwaweza kufunza kinyume kabisa cha jambo hilo. Huenda kukaanzisha tamaa ya anasa isiyo ya halisi na kuifanya ile hatua ya kuacha ujana kuingia katika ulimwengu halisi wa watu wazima iwe yenye kufadhaisha zaidi.

Biblia inaendelea kuonyesha kwamba kufanya kazi kwa bidii sana kwa ajili ya utajiri ni ufuatiaji wa ubatili. Husema hivi: “Usijitaabishe ili kupata utajiri; . . . Je! utavikazia macho vile ambavyo si kitu? Maana bila shaka mali hujifanyia mabawa, kama tai arukaye mbinguni.”—Mithali 23:4, 5.

Kama kazi itathibitika kuwa ono la kujifunza lenye thamani itategemea aina ya kazi inayohusika, aina ya watu unaofanya kazi nao au unaofanyia kazi, na jinsi unavyojitahidi kazini. Kusudi lako la kufanya kazi na jinsi unavyoshughulikia pesa unazochuma litafanya tofauti kubwa zaidi ya kama kufanya kazi kutakusaidia au kutakuumiza.

Lakini ikiwa kukua ndilo jambo unalopendezwa nalo kweli kweli, angalia jinsi Greenberger na Steinberg walivyokata maneno: ‘Kuna utendaji mbalimbali unaopatikana ambao huenda ukawa wenye manufaa kuliko kufanya kazi. Utendaji huo mbalimbali unatia ndani kusoma na kujifunza nje ya shule na kuchukua madaraka ya kazi ya hiari isiyolipiwa au utumishi wa kijumuiya.’ Nina, kwa mfano, akiwa mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, hufanya utumishi wa kijumuiya wenye thamani sana baada ya shule. Asema hivi: “Nilipanga pamoja na mshauri wangu wa shule mwenye kutoa mwongozo, ili niwe na siku fupi shuleni na hivyo nitoke shuleni karibu saa sita. Jumatatu hadi Jumatano mimi hufanya kazi ya kuhubiri peupe. Ninapenda kufanya hivyo. Ninaipenda sana sana!” Je! ratiba na hali zako za kibinafsi zingekuruhusu kufanya hivyo hivyo? Kusitawisha “ujitoaji kimungu” katika njia hiyo kungethibitika bila shaka kuwa na manufaa kuliko kufanya kazi mahali fulani!—1 Timotheo 4:8.

Lakini huenda vijana wengine wakataka, au wakahitaji, kufanya kazi kwa sababu za kifedha. Makala za wakati ujao zitachunguza faida na hasara za kufanya hivyo.

[Maelezo ya Chini]

a Idadi inayoongezeka ya wanafunzi wanaofanya kazi imeitwa “ajabu ambayo ni ya Kiamerika hasa.” (When Teenagers Work, ya Ellen Greenberger na Laurence Steinberg) Vijana katika mabara mengineyo huwekelewa mizigo ya kielimu, na mara nyingi nafasi za kazi ni chache. Walakini, makala hii bila shaka itapendeza vijana wengi katika mabara yaliyo na nafasi za kazi. Makala ya wakati ujao itashughulika na hali katika mabara yanayoanza kusitawi.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Kazi inaweza kufunza kijana jinsi ya kushughulika na waajiri wa kazi na wafanyakazi wenzi katika njia ya watu wazima

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki